Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA (K.n.y. MWENYEKITI WA KAMATI YA ARDHI, MALIASILI NA UTALII): Mheshimiwa Spika, ninayo heshima tena kusimama mbele yako na mbele ya Bunge lako Tukufu jioni hii ili niweze kuhitimisha hoja ya Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kutoa muhtasari wa yale ambayo yamejiri katika mjadala ulioendelea hapa, nitumie fursa hii kwa sababu asubuhi nilishikwa na taharuki baada ya kujiandaa kuwasilisha ile ripoti kwa nusu saa nikaambiwa tuna roba saa lakini najua sababu ni nini, kutanguliza shukrani za dhati kwa Kiongozi wa Taifa letu, Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa sababu ya mambo makubwa na ya kupendeza anayoendelea kulitendea Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya jamii ya wafugaji na wakulima, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa tamko lake la juzi la kwamba Wizara husika zikakae ili ardhi zote ambazo zimekaa idle mfano mashamba na maeneo ya hifadhi ambayo yamepoteza hadhi yakapitiwe upya ili wananchi wanaoteseka waweze kupata maeneo ya kulima na kufugia. Kwa kweli amewafariji sana jamii ya wafugaji na wakulima hususani watu wa Kanda ya Kaskazini wamefarijika na wamefurahia sana suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitumie dakika moja kusema ahsante sana kwa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Umwagiliaji kwa taarifa ambayo nimeisikiliza hapa kidogo na Waziri akanigusa katika maslahi mazuri anayowawekea jamii ya kifugaji ya kuhakikisha kwamba masoko ya uhakika na viwanda yanakwenda kuanzishwa ili tuondokewe na hiyo kero ya kupeleka mifugo Kenya. Nimshukuru Waziri kwa operesheni alizozianzisha ambazo zimeleta kilio kikubwa kwa wananchi wa jamii za kifugaji hasa wa Wilaya ya Longido ambako mifugo yote ya Tanzania inayokwenda Kenya inapitia sasa itakuwa imetokomezwa.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri zaidi kwa sababu ameniahidi kwamba tutakwenda kule kujaribu kuwapoza wananchi maana kuna unyanyasaji mkubwa umetokea hivi karibuni kwa namna operesheni ile ya kuzuia mifugo inakwenda Kenya inavyotekelezwa. Kwa sababu nimesimama hapa kutoa shukrani kwa jinsi ulivyotupa matumaini, naomba niishie hapo ili nirejee kwenye hoja yangu ya msingi ambayo nakuja kuhitimisha.

Mheshimiwa Spika, hizi Wizara mbili ambazo Kamati yetu inasimamia, kwanza nianze kuwashukuru wote ambao wamechangia hoja yetu na niwashukuru wajumbe wa Kamati maana wamefanya kazi kubwa na yenye tija ya kuandaa ripoti hii ambayo kwa jinsi mjadala ulivyoendelea inaonekana kwamba kwa kweli kwa asilimia zaidi ya 99 imeungwa mkono hata na wenzetu wa upande huu. Malalamiko yaliyojiri ni madogo sana na nitapitia yale machache ambayo yametamkwa ili nitoe msimamo wa Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi ukiangalia katika Wizara ya Ardhi mambo ambayo yamejiri sanasana ni kuhusu Shirika la Nyumba la Taifa kwamba tulipofanya ziara tulikuta kwamba baadhi ya miradi yake imesimama kwa sababu walizuiwa kukopa fedha na wakawa wameacha miradi viporo. Sisi kama Kamati tulisema kwamba ingefaa sasa Serikali iwaruhusu kama bado wanahitaji hela ya mikopo, maana Waziri hapa ametuambia wana uwezo kabisa wa kulipa wala hakuna tatizo, hiyo miradi viporo imalizwe ili hizo nyumba ziendelee kuleta tija na mapato ya kuwezesha shirika kuendelea kujenga nyumba nyingine hasa zile za bei nafuu ambazo wananchi wanahitaji vijijini.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na mjadala ambao umejadiliwa na wengi kuhusu urejeshwaji wa mashamba makubwa yale yaliyotelekezwa. Hapa ndiyo mjumbe wangu mmoja wa Kamati, ndugu yetu Mheshimiwa Mchungaji Msigwa alikwenda katika hatua ambayo sisi hatukufikia kwenye Kamati ya kutaka kuundwa Tume. Kwa kweli sisi tulichofanya kwenye Kamati ni kuunga mkono tamko la Rais la kusema kwamba hayo mashamba yaliyotelekezwa na maeneo ya hifadhi yaliyopoteza hadhi yaende sasa yakafanyiwe mchakato ili warudishiwe wananchi ambao wanateseka. Huu ndiyo msimamo wa Kamati na yale mengine ambayo alisema tumekubaliana, tulichokubaliana sisi yote yameandikwa katika kijitabu cha taarifa yetu ambayo wote mnayo mkononi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye Wizara hiyo ya Ardhi, suala lingine lililojitokeza ni Programu ya Upangaji, Upimaji na Urasimishwaji wa Ardhi na mradi wa mfano ni ule wa Mkoa wa Morogoro ambapo kuna hizo Wilaya tatu za Kilombero, Ulanga na Malinyi ambazo huo mradi umeendelea kutekelezwa. Hoja iliyotokea kwa mmoja wa wachangiaji anaona kama speed ya hiyo kazi ni ndogo sana. Sisi pia mwanzoni tulishikwa na taharuki kwa sababu tuliona kama mradi hauendi lakini baada ya ziara yetu mwezi uliopita tuligundua kwamba ile timu sasa iko imara, wamepata uzoefu na kazi ile inakwenda kwa speed na hofu yetu ikabakia moja tu ambayo kwa niaba ya Kamati naomba niiseme.

Mheshimiwa Spika, hofu yetu ni kwamba fedha za wafadhili katika ule Mradi wa Upimaji na Umilikishaji Ardhi zimekwenda vizuri sana, wao wameshatoa asilimia 90 ya ile shilingi bilioni 28 ambayo ndiyo walitutengea lakini pesa ya Serikali, ile shilingi bilioni 7 mpaka sasa hivi wao wametoa tu asilimia 10. Kwa hiyo, rai yetu kama wajumbe wa Kamati tunaiomba sana Serikali kwamba wajitahidi na wao watimize ahadi yao, watenge fedha za kutosha kwenye bajeti kwa sababu hii misaada ya wafadhili itakapokoma itatukwamisha. Hofu yetu ni kwamba kwa sababu huu mradi unakwenda kufanikiwa kwa kasi na ufanisi mkubwa katika hizi wilaya tatu ni kwamba hatutaweza kunakili au ku- reduplicate katika Wilaya zote za nchi yetu kama sera inavyosema kwamba kila kipande cha ardhi ya nchi hii kitakwenda kupangwa, kupimwa na kumilikishwa. Sambamba na hilo, tulikuwa tunategemea katika zoezi la upangaji wa ardhi ambapo ni mpango wa matumizi bora ya ardhi kila jamii itatenga maeneo mahsusi ya akiba kwa ajili ya vizazi vya baadaye.

Mheshimiwa Spika, hayo ndiyo mambo makuu yaliyojitokeza katika mjadala kwenye Wizara ya Ardhi lakini pia kulikuwa na suala moja ambalo tuliliweka lakini halikuchangiwa ila naomba niseme kwa niaba ya Kamati kwamba, tulipokwenda kutembelea ile mipaka ya nchi yetu na nchi ya Uganda, tulijifunza kwamba alama zilizowekwa tangu enzi za kikoloni (beacons) pamoja na kwamba ni kubwa na zinaonekana kwa mbali, lakini zimefukiwa, ziko mbalimbali na imesababisha raia wa nchi ya kigeni kuvamia ardhi yetu pengine hata pasipo kujua na kuishi kana kwamba wako katika ardhi ya nchi yao.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa zaidi ambayo naiomba sana Serikali itilie maanani ni changamoto ya barabara za kuimarisha ulinzi wa mipaka ya nchi yetu. Kwa sababu hakuna barabara ya kuzungukia ile mipaka ili kuiweka madhubuti na kuihakiki na kuwasogeza watu wa nchi za jirani wanaovamia. Kwa hiyo, nimeona kwamba hilo ni pengo moja ambalo wachangiaji hawakuliona lakini sisi kama Kamati tumeliweka katika taarifa yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, hayo ndiyo mambo ya msingi katika Wizara ya Ardhi lakini kwenye Wizara ya Maliasili mambo yaliyoibuka sana ni ule Mradi wa Kukuza Utalii wa Kanda za Kusini kupitia Mradi wa REGROW na masuala ya misitu. Hoja kubwa nyingine ambayo Wajumbe pia wamechangia na sisi tuliona ni hili la mtawanyiko wa mamlaka zinazosimamia misitu ya nchi yetu. Sasa hivi tuna karibu aina nne za misitu; kuna misitu ya Serikali Kuu, misitu ya Serikali za Mitaa na kuna misitu ambayo iko chini watu binafsi na mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia misitu tuliyonayo asilimia 52 ziko mikononi mwa Serikali za Mitaa na asilimia 35 ndiyo ziko katika Serikali Kuu. Ukiangalia uharibifu katika misitu yetu, asilimia kubwa inatokea katika misitu iliyo katika utawala na usimamizi wa Serikali za Mitaa. Ndiyo maana Kamati katika ripoti yetu imeweka pendekezo kwamba ingependeza na ingefaa sasa na sisi katika Wizara hii tuanzishe mamlaka kamili ya kusimamia misitu badala ya kuwa na Wakala wa Misitu tuwe na Mamlaka ya Misitu kama tulivyo na Mamlaka ya Wanyamapori yaani iitwe Tanzania Forest Authority.

Mheshimiwa Spika, pia wajumbe walichangia kuhusu tozo za utalii na mazao ya misitu. Wazo kubwa ambalo limeungwa mkono ni hili la kusema kwamba tuwe na one stop payment center na kodi zipunguzwe ili kuvutia utalii. Utalii hapa kwetu sasa hivi kwa kulinganisha na nchi za jirani umekuwa ghali na Tanzania as a tourism destination, imeonekana ni ghali ukilinganisha na nchi za jirani kama Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini na hata wenzetu hapa Kenya.

Mheshimiwa Spika, pia suala la WMA limeibuka katika mjadala na wachangiaji walikuwa wanasisitiza kwamba WMA zitambulike kama ardhi ya jamii, ambapo jamii ndiyo ina mamlaka nayo juu ya matumizi yake na isiwe na utawala unaofanana na ule wa National Parks wa wananchi kufukuzwa na kusukumwa pale ambapo wamependelea kuishi na kufanyia shughuli zao za kibinadamu. Kubwa zaidi katika WMA, Serikali imekaa mbali nazo hata yale mapato ambayo yanakusanywa na Serikali Kuu inachukua muda sana kurudishiwa na hiyo ndiyo imesababisha WMA nyingi hadhi yake kushuka na pengine baadaye zitakuja kupoteza haki ya uhifadhi na kukosesha jamii mapato.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine muhimu ambalo limetajwa ni hili la single entry wakati watalii wanapokuja kwenye hifadhi zinazopakana na maeneo ya jamii yenye utalii wa kitamaduni. Kuna malalamiko kwamba wanapoingia wakatamani kutoka na kurudi wanatozwa tena ada nyingine ambayo inawaumiza na inawakatisha tamaa na kuwakosesha wale walioko nje ya parks fursa ya wao nao kupata mgawo wa mkate wanaoleta watalii wanaokuja. Kwa hiyo, tunaomba sana hilo suala ama double entry fee liangaliwe ama uwepo utaratibu wa biometric, zile mashine za kusoma alama za vidole, mgeni akitoka abonyeze ionekane ametoka na ameingia saa ngapi ndani ya zile saa ambazo zinaruhusiwa.

Mheshimiwa Spika, pia hili suala la kuanzisha Utalii Channel tumeliunga mkono sana sisi kwenye Kamati yetu. Napenda tu kusema kwamba kinachohitajika sasa pale ni kutangaza katika lugha mbalimbali za kimataifa pamoja na lugha yetu ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa pia na suala la urudishwaji wa ardhi karibu na maeneo yaliyohifadhiwa. Kuna mwenzetu mmoja katika Wabunge waliochangia ambaye alikuwa anasema kwamba suala hili liangaliwe kwa makini kwa sababu tutakuja ku-block wildlife corridors, yale maeneo au mapito ya wanyamapori. Naungana naye kusema kwamba hilo ni suala la msingi na la muhimu sisi kama wahifadhi kuliangalia. Ni wazi Rais alivyosema kwamba Wizara zikakae ziweke mchakato pamoja na michakato mingine ni kuhakikisha kwamba wamezingatia maslahi ya maeneo ambayo bado yana hadhi ya uhifadhi, yana mapito ya wanyamapori na hawataweza kupangilia makazi ya watu katika maeneo ambayo bado yanatusaidia katika kudumisha rasilimali yetu ya maliasili.

Mheshimiwa Spika, kati ya wachangiaji wa leo, nimepokea michango ya maandishi wachangiaji wane na pia waliochangia kwa kutoa hoja hapa Bungeni wamefikia 16. Napenda kuwashukuru sana wote kwa sababu wamegusia mambo ya msingi ambayo nasi tulikuwa nayo kwenye ripoti yetu na sijapata mawazo yaliyokwenda kinyume na yale ambayo tumeyapendekeza zaidi tu ya kuboresha na kutilia mkazo na sisi tumepokea maoni yenu na naamini kwamba sisi kama Kamati tutakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kuna moja ambalo limetokea ambalo sisi hatukuwa nalo kwenye ripoti, kuna mchangiaji mmoja ambaye ameleta kwa maandishi suala la hofu yake kuhusu upimaji wa miji katika ardhi ya wakulima. Akasema kwamba ardhi inapopimwa kwa sababu mji unapanuka na mkulima aliyekuwa anaotesha korosho, mahindi au maharage akaambiwa huwezi kulima tena kwa sababu sasa eneo hili linakwenda kuwa sehemu ya mji linaacha pengo ambapo yule mkulima anakosa mahali pa kuegemea maana mara nyingi anajikuta hawezi kuchukua vile viwanja na hapewi ardhi mbadala. Akasema Kamati katika kazi zake za siku zijazo iliangalie sana kwa makini suala hilo na mimi nalichukua tutaenda kulifanyia kazi. Tungefurahi kujua ni maeneo gani ya mashamba ambayo sasa hivi yanapimwa kuwa miji ambayo wakulima au wakaaji wake wameathirika na jambo hili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maoni mengine yaliyotolewa ambayo yanafanana na yaliyopo kwenye ripoti yetu, naomba nihitimishe hoja yangu kutoka Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa kusema kwamba naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. PETER J. SERUKAMBA: Mheshimiwa Spika, naafiki.