Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hii pia na naomba nitoe mchango wangu kwanza kwa kuunga mkono hoja iliyowekwa mbele yetu na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na kuwahakikishia kwamba kwa kuwa tunafanya kazi vizuri na kwa ukaribu, tutaendelea kushirikiana kuhakikisha mapendekezo yaliyotolewa na Kamati yao tunayafanyia kazi kwa wakati muafaka na kwa namna ambayo wenzetu Wajumbe wa Kamati na Bunge litaridhia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba nianze kwanza kwa kuchangia kuhusu mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kufufua Shirika la Ndege, kujenga viwanja vya ndege nchini na namna ambavyo unaungana moja kwa moja na jitihada za kukuza utalii katika Taifa letu. Jana zilizuka hoja nyingi kuhusu Uwanja wa Ndege wa Chato na unaweza ukazielezea kiurahisi sana kama utazungumzia Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kufungua kiutalii Circuit ya Magharibi na Kaskazini Magharibi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkakati huu unaenda sambamba na mkakati wetu wa kufanya ukarabati na utanuzi wa Kiwanja cha Ndege cha Nduli, kilichopo pale Iringa na kujenga viwanja vingine viwili vya ndege pembezoni mwa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, ambayo kwa sasa ni hifadhi ya saba kwa ukubwa duniani na kwa Afrika inashika namba nne na kwa Tanzania ni hifadhi ya kwanza kwa ukubwa. Ndipo mahali pekee kwa haraka haraka ukienda kutembelea unaweza ukawaona predators wakiwa in action. Unaweza ukaona simba wakikimbiza mbogo, wakikamata na kula ni matukio ya kawaida kabisa ukiwa pale Ruaha National Park.

Mheshimiwa Spika, sambamba na mkakati huu, katika Awamu ya Tano tunakusudia kufungua pia Circuit ya Kusini kwa upande wa Selou kwa maana ya kujenga Kiwanja kingine cha Ndege cha kiwango cha sakafu ngumu Kaskazini mwa Pori la Akiba la Selou maeneo ya Matambwe, uzuri wewe ni mwenyeji sana kule ili kufungua utalii wa picha upande huo. Mikakati yote hii kwa ujumla wake inaenda sambamba na mikakati inayotekelezwa na Serikali ya kufufua Shirika la Ndege la Taifa kwa kununua ndege lakini pia kufungua safari za moja kwa moja kwenye masoko mbalimbali ya utalii na kuyaunganisha na Jiji letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikianza na jitihada zetu za kupandisha hadhi Mapori ya Akiba ya Burigi, Biharamulo, Kimisi, Ibanda na Rumanyika kwenda kwenye hadhi ya National Park, muda si mrefu tutafikisha mbele yako mapendekezo ya Serikali baada ya kukamilisha mchakato ambao tupo katika hatua za mwisho ili tupate ridhaa ya Bunge lako Tukufu kupandisha hadhi Mapori haya matatu na kuyaunganisha kuwa National Park moja ya Burigi Chato National Park, ambako itachukua yale maeneo yaliyokuwa Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi na Kimisi, pia kupandisha hadhi Pori la Akiba la Ibanda ili kuwa Ibanda National Park na Pori la Akiba la Rumanyika ili kuwa Rumanyika National Park.

Mheshimiwa Spika, Circuit hii itakamilika kwa kuunganisha na Hifadhi ya Taifa ya Rubondo ambayo iko ndani ya Ziwa Victoria na Hifadhi ya Taifa ya Saanane na tutaweza kuiunganisha na Circuit ya Magharibi pamoja na Hifadhi ya Taifa ya Mahale na Hifadhi ya Taifa ya Gombe. Pia ndani ya Serikali tuko katika mchakato kuona kama tunaweza tukapandisha hadhi eneo la kiini cha Pori la Akiba la Moyowosi, Kigosi na Ugala pale pembezoni mwa mto ili pia yawe Hifadhi ya Taifa na tuweze kufanya utalii wa picha. Circuit hiyo sasa itakamilika kwa upande mmoja. Vilevile Circuit ya Kusini tutaweza kuiunganisha vizuri kwa kuwa na ndege ambazo zitaweza kutua na kufanya safari zake za kawaida kila siku kwenye maeneo ya Msambe, kama nilivyosema, upande wa Kaskazini Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, pia katikati ya Hifadhi ya Taifa ya Mikumi pamoja na hiyo Circuit ya Kaskazini ya pori la akiba la Selou.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ukiangalia kwa undani sana unaweza ukaona tunapowekeza kwenye ndege na viwanja vya ndege ni kama vile tunatupa pesa nyingi sana kwenye jambo ambalo pengine haliwagusi wananchi moja kwa moja. Nimesikia michango ya Waheshimiwa Wabunge, hususan wanaotokea ng’ambo ya pili katika eneo hilo na mimi napenda kupingana nao na pengine kuwapa maelezo kwamba sekta ya utalii inachangia kuingiza pato la Taifa kwa asilimia 17.6 na ndiyo sekta inayoongoza kwa kuingiza fedha za kigeni hapa nchini kwa asilimia 25 ya fedha zote za kigeni zinazoingia nchini. Pia sekta hii inachangia Dola za Kimarekani bilioni 2.4 katika uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Utafiti wa Benki ya Dunia wa mwaka 2014 ulisema kama nchi yetu itafanya vizuri katika eneo la maliasili na utalii kufikia mwaka 2025 tutaweza ku- tap kutoka kwenye sekta hii mapato yanayofikia Dola za Kimarekani bilioni 16,000. Kipindi hicho inakadiriwa kwenye taarifa hiyo kubwa kabisa inayohusu Hali ya Uchumi wa Tanzania ya Benki ya Dunia, kwamba watalii kwa mwaka huo watakuwa wamefikia kiasi cha milioni 8 leo hii tuko hapo karibia milioni 1.5.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, utaona Waheshimiwa Wabunge wengi wanachangia kwamba pengine jitihada za kutangaza vivutio hazijafanyika ipasavyo, pengine tunahitaji kujipanga zaidi; tunakubaliana nao lakini pia Serikali imeshachukua hatua nyingi sana katika kutangaza vivutio vyetu na ndiyo maana idadi ya watalii inaongezeka mwaka hata mwaka. Mwaka jana tu Mheshimiwa Waziri Mkuu alitufungulia channel maalum ya utalii (Tanzania Safari Channel) tumepokea mapendekezo ya Kamati kwamba tujitahidi kuifanya iweze kuonekana nje ya nchi na ndizo jitihada ambazo kweli kwa sasa tunaendelea kuzifanya ili iweze kuonekana kwa wingi zaidi nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwenda kwenye show mbalimbali ambazo tunawakilishwa na Bodi yetu ya Utalii bado tuna mikakati mingine mahsusi ya kukuza sekta ya utalii kwa kutumia watu mashuhuri wanaokuja hapa nchini. Pia kutangaza kwenye michezo kutangaza, vituo vya mabasi na treni kule nje, ni mikakati ambayo tunaiwekea hatua mbalimbali za utekelezaji. Pia kuweka mabango makubwa katika maeneo yote ambayo ni mageti ya kuingia katika nchi yetu kuanzia viwanja vya ndege na hata pale maeneo ya bandarini; tuna mradi huo ambao tuko katika hatua ya kuutekeleza na muda si mrefu kila sehemu utakuwa ukizunguka ukiangalia hivi unaona simba, tembo na kadhalika. Hata kwenye ile round about kubwa ya hapa Dodoma tunakusudia kuweka television kubwa kabisa ambayo itakuwa inaonesha live kila kinachoendelea ndani ya creator. Kwa hivyo, tukifanikiwa kufanya hilo, kila atakaye kuwa anaingia katika Jijini la Dodoma ataweza kuona vivutio vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, napenda pia kuzungumzia kuhusu Mradi wa REGROW ambapo wenzetu wanadhani kwamba unasuasua lakini pia Kamati yetu imezungumzia sana kuhusu ucheleweshaji wa utekelezaji wa mradi huu. Mradi huu unatekelezwa kwa mkopo kutoka Benki ya Dunia ambapo nchi yetu inakopeshwa Dola za Kimarekani milioni 150. Fedha hizi ni nyingi na ni mkopo na mkopo maana yake ni lazima ulipwe.

Mheshimiwa Spika, nilipoteuliwa kuwa Waziri kwenye Wizara hii nilisoma lile andiko la mradi na nikaona kwamba haukukaa zaidi kibiashara. Kwa sababu ukiuangalia unaona haujahusisha ujenzi wa barabara kutoka Nduli Airport pale Iringa kwenda mpaka kwenye geti la Msambe kuingia Ruaha National Park, hakuna mradi wa kuukarabati Uwanja wa Ndege wa Nduli lakini pia ulikuwa ujenge viwanja vidogo vidogo vya hadhi ya changarawe katika maeneo yote hayo ambayo nimeyazungumzia ya Circuit hii ya utalii ya Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe ni Mhifadhi unafahamu, kila mkitaka kukarabati viwanja vya changarawe lazima mchukue material humo humo ndani ya hifadhi yenyewe maana mnazidi kuharibu mazingira lakini pia mnajenga mwaka huu baada ya mwaka mmoja mnaanza ukarabati. Nikasema mradi ulipokuwa designed haukukwa commercially sound kwa kiasi kikubwa, kwa hivyo, tukasema lazima tuufanye huu mradi uwe wa kibiashara. Ili kuufanya mradi ule uwe wa kibiashara tuliona ni lazima pajengwe viwanja vya ndege ambavyo vina sakafu ngumu ambavyo vinaendana na uhifadhi wa mazingira kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tukasema badala ya viwanja 15 bora tupate vinne (4) ambavyo vitadumu kwa muda mrefu, havihitaji ukarabati lakini pia vitatuwezesha tupate watalii ambao kwa sasa wanatukwepa kutokana na masharti mbalimbali yaliyopo katika bima zao za maisha ama bima zao za flight. Mfano, wazee wanaokuja Tanzania hapa ambao wako zaidi ya miaka 65 ni asilimia 5 tu ya watalii wote lakini hili ndilo kundi kubwa ambalo linasafiri duniani kwa ajili ya kupumzika; wazee ambao wako kwenye pensheni, wana pesa za kutosha, wana bima za maisha wanahitaji kwenda kupumzika katika maeneo mbalimbali. Hawa wote wanakwenda Kruger National Park kule South Africa kwa sababu wenzetu wana uwanja wa ndege ambao una sakafu ngumu na sisi tunaishia kupata asilimia 5 tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tukijenga Viwanja vya Ndege kwa sasa maana yake tutaweza kupata hii segment ya soko la watalii ambao wana bima za maisha. Sababu ni moja tu, bima nyingi za maisha zinawataka watalii lazima wasafiri kwenye ndege ambayo ina injini mbili, ma-pilot wawili lakini pia atue kwenye sakafu ambayo ni ngumu, ambapo ikitokea ajali ataweza kulipwa hiyo bimavinginevyo hawezi kupata hiyo bima. Kwa hiyo, sasa tukaona ni bora ili kuufanya mradi uwe commercially viable tujenge viwanja vichache lakini vyenye sakafu ngumu tuweze kupata wageni hao. Kwa hivyo, tuliweka mguu tukasema hapana lazima mabadiliko yafanyike katika mradi huu ili mradi uwe commercially viable, tuongeze idadi ya watalii na pia tupate pesa kwa ajili ya kulipa deni ambalo linatokana na mradi wenyewe.

Mheshimiwa Spika, pia ikatokea maneno kidogo ambayo sasa hivi tungeweza kuyatatua kwamba tutatekeleza mradi katika eneo la Selou, kwa hivyo, tusiutekeleze kule Selou kwa sababu kuna uharibifu wa mazingira. Sisi tukasema hapana mradi utatekelezwa maeneo yote ama usitekelezwe kabisa kwa sababu hatuwezi kutekeleza nusu nusu tukaiacha segment ya mradi ambayo ipo katika Pori la Akiba la Selou. Bahati nzuri Benki ya Dunia sasa hivi wamekubali kwamba tutekeleze mradi na tutekeleze pia mradi wetu wa kufufua umeme katika Bonge la Mto Rufiji. Kwa hivyo, kwa sasa tumebaki tuna negotiate kwenye eneo hili moja la viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo napenda kuzungumzia ni kuhusu uwindaji wa kitalii. Uwindaji wa kitalii umekumbwa na dhoruba nyingi sana tangu mwaka 2008 mpaka leo. Uzuri wewe ulikuwepo Bungeni na ulikuwa kwenye Kamati inayosimamia maliasili hivyo unafahamu kilichotokea, sina haja ya kurudia hapa.

Mheshimiwa Spika, wakati mimi nateuliwa kuwa Waziri kwenye Wizara hii nilikuta mapato yameshuka mpaka chini ya bilioni 10 kwa mwaka sasa hivi tumeweza kuyapandisha mpaka zaidi ya bilioni 40 na mwaka huu tunakusudia kuweka bajeti zaidi ya bilioni 60. Mapinduzi ambayo tumeyafanya kwenye sekta ya uwindaji wa kitalii ambayo mashuhuri yanajulikana kama Hunt More for Less yatatupeleka kuifufua sekta ya uwindaji wa kitalii na kupata mapato makubwa zaidi kuliko ilivyo sasa na pengine uwindaji wa kitalii nao ukachangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja ya Kamati. (Makofi)