Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nitumie nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru Mungu ambaye anatupa uzima, pia nitumie nafasi hii kuzishukuru na kuzipongeza Kamati zote mbili ile ya Kilimo pamoja na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, ningeomba kuchangia kwenye maeneo machache. Ningeomba nichangie kidogo kwenye utalii na baadaye nitaenda kuchangia kidogo kwenye eneo la ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la utalii, tulipokuwa kwenye Kamati tumepata taarifa na tumetembelea Mradi huu wa REGROW. Ni mradi mzuri ambao utasaidia nchi yetu kuinua utalii kwenye maeneo ya Kusini mwa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba kushauri tu, ilizungumzwa asubuhi hapa, tunapotaka kuinua watalii kwenye maeneo ya Kusini lazima twende sambamba na kuangalia namna ya kuboresha na kusimamia uhai wa hizi hifadhi zetu. Imezungumzwa kuhusu Hifadhi ya Taifa ya Mikumi kuhusu ile barabara, barabara ile ina madhara mengi. Kwa haraka haraka kuna changamoto kama nne zinazosababishwa na barabara hii. Changamoto ya kwanza inarahisisha sana shughuli za ujangili na inasababisha uwepo wa takataka ambazo nyingine ni hatari kwa maisha ya wanyama wenyewe. Taarifa tuliyopewa ni kwamba kuna wastani wa kilo 318 za takataka kwa siku ambazo zinazalishwa kutokana na kuwepo na barabara katikati ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni kugongwa kwa wanyama. Mwaka 2015/2016 wanyama 361 wamegongwa, mwaka 2016/2017 wanyama 218 na mwaka jana Julai mpaka Desemba 2018 ni wanyama 130. Ukichukua mwaka wa fedha wa 2013/2014 mpaka 2017/2018 ni wafanyama 1,062 wamepoteza maisha kwa sababu ya barabara ile. Idadi hii ni kubwa, ni lazima tufanye maamuzi mazito na magumu.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba barabara hii ni ya kimataifa na inawezekana kuna mikataba ya kimataifa ambayo inatuongoza kutumia barabara ile. Lazima ifike mahali Serikali au nchi tuamue na tukapokuja kuamua mambo mazito kwa ajili ya maslahi na ustawi wa nchi yetu haswa maslahi ya hifadhi zetu hatuna haja ya kuangalia sana makele yanayotoka huko nje na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, tumeona hili kwenye Stiegler’s, watu wamepiga kelele nyingi sana lakini tumesema kama Taifa tunahitaji kuwa na uchumi wa viwanda na ili tuwe na uchumi wa viwanda tunahitaji kuwa na umeme wa uhakika. Tumeamua hakuna namna nyingine lazima nchi kutekeleze mradi huu kwa ajili ya kupata umeme wa kutosha kwa maendeleo ya nchi yetu. Kama Mheshimiwa Rais alivyoamua chini ya Serikali yake kuendesha mradi ule, naishauri Serikali iangalie kwa jicho la haraka na la dharura juu ya barabara hii ili tuendelee kulinda maisha na uhai wa Hifadhi ya taifa ya Miukumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze kidogo kwenye sekta ya ardhi. Nitumie nafasi kwa dhati kabisa kumpongeza sana Mheshimiwa wa Ardhi na Naibu wake, wanafanya kazi kubwa tunawaona wanavyoangaika kwenye maeneo mbalimbali ya nchi kutatua migogoro ya ardhi. Nachoomba kuwashauri kama Wizara waendelee kutengeneza utaratibu maalumu na mahsusi wa namna gani ya kuondokana na changamoto za ardhi ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwenye jambo hili la ardhi nilisikia asubuhi watu wanazungumza hapa na ziko dhana na hisia kwamba kuna watu wanaonewa kwenye mchakato wa kufuta mashamba. Kwanza niseme, nilimshangaa sana kumsikiliza ndugu yangu mmoja akisema kwamba tulikubaliana kwenye Kamati lakini anashangaa huko haikusomwa. Mimi ni Mjumbe wa Kamati na kama ndugu yangu yule angekuwa ni Mtumishi wa Mungu kama nilivyo mimi nisingesema hapa tungeenda kuzungumza kiroho lakini kwa sababu si Mtumishi wa Mungu lazima nitumie nafasi hii kusema, hatukukubaliana jambo la namna hiyo kwenye Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili ya Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Rais hafuti tu mashamba kwa kukurupuka, mashamba yanafutwa kwa mujibu wa sheria zilizotungwa na Bunge hili. Bahati nzuri ni Mwanasheria na nimepata nafasi ya kufanya kazi kwenye Wilaya zenye migogoro mikubwa sana ya ardhi na nimewahi kuwa Wakili wa watu waliokuwa na kesi dhidi ya Serikali kwa ajili ya kufutiwa mashamba, nafahamu changamoto ilipo. Kama kuna watu wanaobebembelezwa ni watu wenye mashamba, anapewa onyo, anapewa notice ya siku ya 90 ili ku-remedy breach za conditions za hiyo right of occupancy aliyoipewa, hawafanyi. Technique ambayo inatumika mara nyingi unakuta mtu anakuja dakika za mwisho, siku 90 zimekwisha anaanza kwenda kugusagusa sehemu ndogo anaondoka halafu anasema nimeendeleza, si sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii niseme kwamba nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi aliyoifanya ya kufuta hati za shamba ya baadhi ya wawekezaji kwenye nchi yetu. Ukienda Korogwe leo wananchi wamemwelewa sana Mheshimiwa Rais na wamemshukuru. Bunge hili waliokuwepo muda mrefu ni mashahidi, mtangulizi wangu Profesa Maji Marefu alikuwa kila akisimama analia na mashamba yasiyoendelezwa Korogwe. Leo Mheshimiwa Rais amefuta mashamba watu wanapiga kelele kwa maslahi ya nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Korogwe tunamshukuru Mheshimiwa Rais na tumuombe Waziri wa Ardhi bado kuna mashamba mengine ya akina Chavda yamekaa ni mapori, mpelekeeni Mheshimiwa Rais atafutie wananchi wapate maeneo. Ukienda kule Magoma na Kwa Shemshi kuna ardhi kubwa mashamba yamekaa, hayaendelezwi yamekuwa mapori na wengine wanakodisha, mpelekeni Mheshimiwa Rais atufutie ili wananchi wapate maeneo ya kilimo na makazi. Mimi nawapenda sana wawekezaji lakini lazima tuwe na wawekezaji ambao wanatutendea haki na wanatendea haki masharti ya umiliki waliyopewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia vizuri watu wanalaumu lakini kama kuna mtu anamwelewa Rais ni mimi, ni Rais anayependa haki na ni asiyemuonea mtu. Mimi ninao ushahidi wa baadhi ya mashamba, kwa sababu michakato inaanzia kwenye Halmashauri, yako baadhi ya mashamba ambayo wenzetu kwenye Halmashauri waliwahi kutengeneza na kupeleka kwa Rais yakafutwe. Hata hivyo, yalipofika Wizarani na Mheshimiwa Rais wakaona utaratibu umekiukwa yalirudishwa na Mhesimiwa Rais, tunataka haki ya namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nenda Wilaya ya Arumeru, Mheshimiwa Lukuvi anafahamu liko shamba la Karamu Coffee Estate, Halmashauri, Mkoa kote tulipeleka lakini lilipofika juu Rais akasema utaratibu unaonekana hauko sawasawa rudisheni mkarekebishe. Achana na hilo, nenda Kilombero, yuko mtu mmoja alikuwa na nafasi kubwa sana kwenye nchi hii sitamtaja, sasa hivi ni marehemu, Halmshauri walipitisha wakataka yale yafutiwe hati wakapeleka kwa Mheshimiwa Rais akasema hapa kuna uonevu rudisheni, tunataka Rais wa namna gani, tunataka Rais afanye nini tena? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona hapa watu wanasema ooh watu wanaonewa, wanasumbuliwa, wameendeleza, nataka niwaambie ndugu zangu kama kuna Rais tunamshukuru watu wa Korogwe ni Mheshimiwa Rais Magufuli. Sisi watu wa Korogwe hatusimuliwi, tumeona wenyewe, mwacheni Mheshimiwa Rais afanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote tunawataka wawekezaji lakini waacheni wawekezaji hao wafuate taratibu, sheria na kanuni za nchi yetu na yule ambaye atakiuka achukulie hatua kama ambavyo hatua zimeendelea kuchukulia. Mheshimiwa Lukuvi nakukumbusha tu tunakuomba Korogwe mashamba ya Chavda, Kwa Shemshi na Magoma mwende mkampelekee Mheshimiwa Rais, tufute tuwapelekee Watanzania wakatumie ardhi ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna mtu anayepewa haki bila kuwa na wajibu. Sheria ya Ardhi inayowapa watu haki ya kumiliki ardhi inawapa na masharti na mtu asipokiuka masharti nimesema anastahili zake, stahili ni pamoja na hizo. Kwenye suala la mashamba, mimi kama Mjumbe wa Kamati, kama Mwakilishi wa watu wa Jimbo la Korogwe Vijijini tuko na Mheshimiwa Rais na tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa jambo kubwa alilolifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeuona ule Mradi wa Kurasimisha na Kumilikisha Ardhi uliokuwa unatekelezwa kwenye maeneo ya kule Malinyi, Kilombero na Ulanga, ni mradi mkubwa. Nimefarijika mradi ule, niliambiwa hata Mheshimiwa Waziri kuwa unasimamiwa na vijana, wamefanya kazi kubwa. Hatusemi kwamba wazee hawafanyi kazi kubwa lakini wale vijana kwenye mradi ule wameutendelea haki wanastahili kupewa pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Wizara, tuwe na utaratibu wa kuendeleza mradi huu kwenye maeneo mengine. Safari hii tumepata hela za wafadhili hatujui mbele ya safari tutakuwa na hela za wafadhili au tutazikosa. Kwa vyovyote itakavyokuwa mradi ule ni wa muhimu kutusaidia kupunguza migogoro ya ardhi ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba nizungumze kidogo kuhusu Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Hifadhi hii ni kubwa, ndiyo hifadhi ya kwanza kwa ukubwa kwenye nchi yetu na Afrika Mashariki. Ni miongoni mwa hifadhi chache ambazo hazijaathiriwa na shughuli za kibinadamu. Kamati imesema kwenye taarifa yake kwamba changamoto kubwa ni kuelekea kukakuka kwa Mto Ruaha Mkuu ambao ndiyo roho ya hifadhi ile. Niiombe Serikali kwenye jambo hili la Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ili tunusuru hifadhi ile tunahitaji kunusuru Mto Ruaha Mkuu.

Mheshimiwa Spika, tukisema kunusuru Mto Ruaha Mkuu watu wanafikiria kwenda kuwafukuza watu wanaolima kule kwenye Bonde la Usangu na maeneo mengine. Kama alivyosema mzee wangu, Mheshimiwa Jitu, tunazo teknolojia za kisasa zitumike. Pia changamoto kubwa ukienda kule Mabarali si tu kwamba wanalima mpunga kwa kutumia yale maji, hapana, lakini watu wanashilikia maji kwa kuzua magugu na vitu vingine hata baada ya muda wa kilimo cha mpunga. Wizara ya Maliasili ishirikiane na watu wa Ardhi na watu wa Kilimo tuwe na teknolojia nzuri ili yale maji yakimaliza kufanya shughuli za kilimo basi yaachiwe yaendelee kutiririka kwenye mto ili usiendelee kukauka. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeisaidia sana Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja za Kamati zote mbili na mapendekezo yake, ahsante. (Makofi)