Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nipende tu kusema kwamba naunga mkono hoja hii ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira na nipende kipekee kuwapongeza sana Kamati yetu hii ya Bunge kwa ripoti hii nzuri na niwahakikishie tu kwamba nitafanya nao kazi kwa karibu. Niwashukuru kwa mchango wao na ushauri mzuri walioutoa na yote walioyatoa tutayazingatia. Zaidi pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameweza kuchangia hoja hii hususan katika masuala yanayohusu sekta ya uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nipende tu kuanza kwa kuwapa comfort Waheshimiwa Wabunge, kwamba katika sekta ya uwekezaji Tanzania tumekuwa tukiendelea kufanya vizuri, hususan katika suala zima la kuvutia wawekezaji. Hata ukiangalia katika ripoti ya World Investment Report ya mwaka 2018 ambayo ilitolewa na UNCTAD imeonesha pia kwamba Tanzania katika nchi za Afrika Mashariki tumeongeza katika kuvutia uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mwaka jana tu peke yake takribani dollar za Kimarekani bilioni 1.18 zimetufanya tumekuwa wa kwanza tukifuatiwa na Uganda na Kenya imekuwa ni nchi ya tatu. Kwa hiyo nipende tu kusema kwamba ni vyema tusibeze jitihada mbalimbali zinazofanyika, muhimu tu kwamba tuendelee kushirikiana na kuhakikisha kwamba tunaimarisha uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende sasa kipekee kujibu hoja mbalimbali ambazo zimetolewa na Kamati lakini pia na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza ilikuwa ni kuhusiana na changamoto mbalimbali katika mazingira ya ufanyaji wa biashara. Ukiangalia kwa kiasi kikubwa katika ripoti ya Kamati yetu ya Bunge, lakini pia Waheshimwa Wabunge wengi wamejikita sana katika masuala mazima ya changamoto zinazojitokeza, utitiri wa kodi, mifumo ya udhibiti, kuwa na regulatory authorities nyingi ambapo nyingine unakuta zimekuwa zikikwamisha jitihada mbalimbali. Nipende tu kusema kwamba tayari kupitia Serikali mwaka 2016, ilifanya utafiti na ikafanya uchambuzi wa kuangalia changamoto mbalimbali na kero ambazo zinajitokeza katika mazingira ya kufanya biashara nchini, lakini pia katika masuala mazima ya uwekezaji. Ndiyo maana ukiangalia mwaka 2018, mwezi Mei Baraza letu la Mawaziri kupitia Serikali liliweza kupitisha Blue Print (Mpango) wa kuboresha mfumo wa udhibiti wa biashara. Vile vile tunayo Programme ya Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji na tayari tumeshaanza kuandaa road map pamoja na Mpango Kazi Jumuishi (Comprehensive Action Plan) ya miaka mitatu ambayo tayari tunashirikiana na ESRF katika kuhakikisha kwamba hili linaenda kutekelezwa. Tunaamini wiki ijayo tutaweza kukaa na wadau mbalimbali ili kuhakikisha kwamba utekelezaji wa mpango kazi huu jumuishi unafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kuwatoa hofu tena Kamati kama ambavyo wamekuwa wakitushauri, lakini pia katika maelekezo yao ambayo wametoa katika taarifa hii, kwamba ni vyema sasa wapate taarifa ya utekelezaji, lakini pia waweze kupata namna ambavyo changamoto hizi zimeweza kutatuliwa. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati yetu kwamba suala hili litakapoendelea kufanyiwa kazi tutawaletea taarifa ya utekelezaji ya mpango wetu huu jumuishi wa kuboresha mazingira ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja nyingine ya sheria za kodi. Kimsingi Kamati imekuwa ikifanya ulinganisho na kodi mbalimbali zinazotozwa hususan katika kodi za forodha katika nchi zingine za Afrika Mashariki na nyinginezo na kwamba vyema sasa katika utozaji wa kodi tukaangalia mazingira yetu tuliyonayo, lakini pia kuangalia wakati tulionao kwa sasa. Nipende tu kusema kwamba Serikali imekuwa sikivu na ndiyo maana kupitia Wizara ya Fedha tumemsikia Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameunda Kamati ya Mapitio ya Kodi au task force kwenye reforms za kodi lakini pia ametoa mpaka tarehe 10 Februari, yeyote ambaye ana mapendekezo kuhusiana na mapitio ya kodi na maboresho basi wanaweza kuwasilisha huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya tatu ilikuwa ni kuboresha au kufanya mapitio ya Sera yetu ya Uwekezaji, pamoja na Sheria ya Uwekezaji. Nipende tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba hili ni eneo ambalo nitahakikisha katika mwaka huu ujao wa fedha suala hili linakuwa limetekelezwa. Niombe tu ushirikiano tutakapoleta Muswada huu Bungeni, basi tuweze kuupitisha kwa kutambua kwamba utakuwa umeondoa changamoto nyingi. Maana ukiangalia hivi sasa katika Sheria yetu ya Uwekezaji kwa mujibu wa kifungu cha 20, unakuta tunao wawekezaji wa miradi maalum (strategic investors), wanavyo pia vivutio mbalimbali vya kodi na vingine visivyo vya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo unakuta upande mmoja vivutio vyao vimetajwa katika Sheria ya Uwekezaji; lakini upande mwingine bado tunazo Sheria zingine za Fedha na Kodi ambazo unakuta zinakwamisha kuweza kuwapatia vivutio kama ambavyo wamepewa mikataba kwa mujibu wa performance contracts. Suala hili nalo pia ni eneo ambalo tutalizingatia tutakapofanya mapitio yetu ya Sera ya Uwekezaji pamoja na Sheria yetu ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja pia ya kuboresha vituo vyetu vya One Stop Center au vituo vya kutolea huduma za pamoja. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba tumeendelea kuboresha huduma za One Stop Center na hivi sasa tumeongeza Taasisi nyingine takribani tano na kuongeza TFDA, tumeongeza NIDA, NBS, NEMC pamoja na OSHA na wenyewe pia sasa hivi wako under one stop shop ya TIC. Vile vile tunaendelea kuongeza idadi ya Watumishi walioko katika Idara yetu ya Kazi, katika One Stop Center ya TIC, lakini pia tumeshaunda mfumo wa kielektoniki wa Tanzania Investment Window ambao unawasaidia wawekezaji wetu wanaotaka kuchakata au kuwasilisha maombi yao kwa ajili ya kupata cheti cha uwekezaji na maombi ya vibali mbalimbali vya kazi. Kwa hiyo, tunawakaribisha wakati wowote, mifumo hiyo ya kielektoniki ipo lakini pia kwa wale watakaotaka kufanya kwa mifumo (manual) huduma hizo pia zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la nne ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumzia ni suala zima la upatikanaji wa ardhi. Kumekuwa na changamoto hususan katika kubadilisha ardhi kutoka katika ardhi ya kijiji kwenda kwenye ardhi ya jumla, lakini pia imekuwa ikichukua muda mrefu na wakati mwingine wamesema miaka miwili, mpaka miaka mitatu. Napenda tu kusema kwamba ni maeneo ambayo tunaendelea kuyafanyia kazi na Wizara ya Ardhi; na kwa kweli wamekuwa wakitupa ushirikiano mkubwa kuhakikisha kwamba kila mara wawekezaji wetu wanapokuja, basi wanaweza kupata ardhi zao kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la zaidi tu, Mheshimiwa Waziri Mkuu pia alishatoa maelekezo kwa Halmashauri zetu, kuhakikisha kwamba wanatenga maeneo maalum ya uwekezaji, lakini siyo kutenga tu maeneo. Katika eneo hili naomba sana Halmashauri zetu, tuweze kusikilizana vizuri. Wako ambao wamekuwa wakitenga maeneo ya uwekezaji, lakini uhakiki unapoenda kufanyika, idadi ya ekari zinazotajwa unakuta ni tofauti na idadi ya ekari hizo ambazo wao wamesema wamezitenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi tunataka maeneo maalum ya uwekezaji ambayo tayari yameshalipiwa fidia, hakuna mgogoro wa ardhi, lakini yameshapimwa na yameshaandaliwa mpango wa matumizi ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia TIC pamoja na EPZA wameendelea kutoa ushirikiano kwa Halmashauri zetu kuhakikisha kwamba maeneo haya yanatengwa na yanakuwa ni maeneo ambayo yametengwa kwa kufuata Sheria zetu za Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni matamko ya viongozi mbalimbali katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Ni eneo ambalo pia Kamati nashukuru na wenyewe wameweza kulizungumzia. Napenda tu kusema kwamba kazi kubwa inafanyika katika kuvutia wawekezaji. Hatuwezi kufikia katika kiwango hicho cha kupata FDI’s za zaidi ya bilioni 1.18 ya Dola za Kimarekani kama hatupeani ushikiano; kama Taasisi mbalimbali za udhibiti na mamlaka nyingine zinazohusika katika kuwezesha uwekezaji, hazitoi ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, Mamlaka za Serikali za Mitaa, tunajua kwamba wao ndio kioo kwetu kule katika Mikoa, Wilaya na Halmashauri zao, basi tujitahidi kuzingatia Sheria na tujitahidi zaidi kuweka mazingira wezeshi ili kuweza kuwavutia wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Viwanda ilishaandaa mwongozo wa namna ya kujenga uchumi wa viwanda, nasi pia kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, tutakaa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia.

WAZIRI WA NCHI, OFISI WA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: …kuhakikisha kwamba tunatoa mwongozo wa kuona namna gani Mamlaka za Serikali za Mitaa kweli zitaweza kuchukua nafasi yao kule waliko katika kuwezesha uchumi lakini zaidi kuhakikisha kwamba tunavutia uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mengi, lakini kwa sasa napenda tu kusema kwamba tutakuja kueleza mengi kadiri siku zinavyozidi kuendelea. Zaidi, naomba sana ushirikiano na Waheshimiwa Wabunge, lakini pia kupata brief profile za maeneo yenu ya uwekezaji ili tuweze kuvutia uwekezaji huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri Mkuu, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)