Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja zetu hizi ambazo ni muhimu sana zilizoko mezani. Jambo la kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazofanya yeye pamoja na wasaidizi wake, lakini pia niwapongeze Mawaziri walioko katika Wizara hizi ambazo leo ajenda hizo ziko mezani hapa Bungeni kwako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia nimesikiliza pia hata hoja za wachangiaji wengine. Tunapoongea masuala makubwa hasa ya kitaifa ni vizuri sana tukawa tunapata tafsiri zilizo sahihi, kwa sababu usipopata tafsiri zilizo sahihi zinaweza zikasababisha taharuki kwenye mambo ambayo hayapo. Nilikuwa namsikiliza shemeji yangu Mheshimiwa Komu pale ameongelea kipengele kimoja cha balance of payment (BoP).

Waheshimiwa Wabunge jambo alilokuwa analisemea Mheshimiwa Komu ni jambo la kiuchumi na unapoangalia performance ya uchumi katika Taifa huangalii kigezo kimoja na ambacho mabadiliko yake yanabadilika majira kwa majira, unaangalia vigezo ambavyo vinatokana na utekelezaji wa kisera per se. Kwa mfano, huwezi ukasema uchumi wetu umeyumba kwa kuangalia kigezo cha BoP kwamba imerekodi deficit katika majira ambayo katika Taifa letu si majira ya uvunaji, si majira ya mavuno, ni majira ambayo kwa vyovyote vile hata ukiangalia katika miaka mingine katika Taifa lolote katika majira ambayo si ya mavuno utakuta BoP ina-deteriorate kutokana na kwamba si majira ya kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia vigezo kama mfumuko wa bei ambacho ni kitu cha kisera, ukaangalia vigezo kama akiba ya fedha katika Taifa ambacho ni kigezo cha kisera Tanzania imevunja rekodi na tumepata taarifa kwamba zile minimum requirement…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Nimeshasema taarifa hamna tena kaa chini na Mheshimiwa Zitto, Mheshimiwa Zitto, rudi kwenye kiti chako

MBUNGE FULANI: Zitto ndiyo Mwalimu wenu.

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Imezidi miezi mitatu, iko zaidi kwa mbali kabisa miezi mitatu ambayo huwa inapimika katika importation lakini na mfumuko uko chini kwa muda mrefu, yaani siyo mfumuko ambao unayumbayumba ambao mwekezaji yeyote angetakiwa kuangalia katika Taifa aone jinsi suala lilivyo. Hivi vigezo vingine ambavo amevisemea vinavyohusiana na indicators za ufanyaji wa biashara, labda nimwombe kwenye hili Mheshimiwa Waziri na Wizara yake watafute copy ya vitabu vile vya blue print ambayo ilishapitishwa na Serikali na ilishakuwa tayari kwa ajili ya utekelezaji na baadhi ya mambo tayari yameshaanza kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo yale hata siku ambapo Mheshimiwa Rais alikutana na wafanyabiashara ni mambo yaliyotolewa ufafanuzi na wafanyabiashara waliondoka wakiwa wameridhika. Siku ile wao wenyewe ni mashahidi kwa sababu jambo hilo halikuwa kifichoni, lilikuwa live. Wafanyabiashara walipopewa mambo ambayo Serikali ya CCM imeshafanya, waliona kazi iliyofanyika. Hii blue printing ambayo tayari ilishapitishwa inatoa majibu mengi ya vitu hivi vilikuwa vinasema ranking yake ambavyo anavisemea vinashusha ranking ya nchi yetu katika ufanyaji wa biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni utamaduni hasa hasa wa kiafrika kupenda kusema mabaya ya kwako na kudhania kwingine kuko vizuri. Ukienda nchi nyingi za Afrika wao wanatolea mfano mambo mazuri ya Tanzania, ukienda kwenye SADC watatolea mfano Tanzania, ukienda EAC watatolea mfano Tanzania, ila ukirudi Tanzania watasema tume-stack. Sasa ni utaratibu wa kutokujisomea labda kujua wengine wanafanyaje? Haya ambayo tunaweza tukayasema ambayo Mheshimiwa Lema alisema purchasing power ni utaratibu wa kujua unaanzia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Taifa ni lazima ufanye utaratibu wa kuondoka kwenye vicious circle lazima uvunje ile circle, ukiamua kutokuvunja vicious circle kutokutoka kwenye mduara ule wa umaskini utaendelea kuwa kwenye umaskini. Natoa huo mchango na kwa sababu tunaongelea mambo ya viwanda nasema lazima utoke kwenye vicious circle ili hili somo waweze kulielewa. Makofi

Mheshimiwa Mwenyekiti, unatokaje kwenye vicious circle ili uweze kwenda kwenye viwanda, lazima kwanza uweke miundombinu ambayo ni very solid na niipongeze Serikali kwenye hili, haisemei tu kwenye matamko ama kauli mbiu kama mchangiaji mmoja alivyosema, hatua tunaziona ambazo zinaenda kwenye miundombinu ambayo ni very solid kwenda kwenye viwanda. Moja ya kitu kinafanyika ni kuwa na umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni requirement ya msingi sana katika nchi yoyote inayotaka kwenda kwenye viwanda. Ukiamua kuwa na vile walivyokuwa wanafanya babu zetu kusaga kwa mawe au unaweza usihitaji umeme lakini kama unataka kwenda kwenye solid foundation ya viwanda lazima uwe na umeme wa uhakika. Jambo hili Serikali imefanya tena kwa makusudi na halijafanyika mafichoni, mnaona maeneo ambayo uwekezaji kwenye umeme unaenda na mambo haya yataenda mpaka vijijini. Kwa hiyo, kwenye hili la solid foundation kwenye miundombinu moja ni umeme; la pili ni maji; lakini la tatu hata hii miundombinu mikubwa ya usafirishaji, tumeona kwenye reli, lakini tumeona kwenye barabara na kwa sababu ili uchumi uwe inclusive inaenda mpaka kwenye barabara za vijijini na huko kuna TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo machache ambayo napenda kushauri; jambo la kwanza kwenye ushauri; kwa sababu tunatengeneza miundombinu ya miaka mingi itakayohimili uchumi wa viwanda, ni vizuri sana kwa sasa hivi kila mkoa jambo ambalo Mheshimiwa Raisi ameshalisisitiza mara nyingi likafanyiwa kazi la kuwa na industry tax, watu wanaotaka kuwekeza kwenye viwanda wasije wakawa wanaenda kuuziana maeneo na wenyeji, mwisho tunakuja kujikuta kuna kiwanda kipo kwenye makazi na hiyo inatokea utiririshaji maji machafu pamoja na vitu vingine katika makazi, jambo hili limesemwa sana kwa hiyo wenzetu waliopo kwenye kule mikoani lakini pia na Idara zinazohusika ni vyema sana wakalizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni vizuri sana kufanya ile zoning nchi yetu ili kuondoa migogoro kwa sababu population inaongezeka na ardhi ni ile ile ni vizuri sana kama tunataka kulifanikisha jambo hili ambalo limeshaanza kufanyiwa kazi vizuri tukawa na zoning, lazima kuwa na maeneo ambayo yameshajitambulisha yenyewe ili yaweze kupewa kipaumbele katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Kanda ya Kati kuna mambo ya alizeti, lilikuwepo hili jambo la cluster ambalo lilishaanzishwa, ni vema likatiliwa nguvu, kuwe na corridors ambazo ni mahususi kwa ajili ya mchele, hapo tutakapoweza kuwa wauzaji wakubwa wa mchele kidunia, maeneo mengine ya ng’ombe wa nyama, maeneo mengine ng’ombe wa maziwa ili kuondoa mwingiliano kwamba wale wengine wamepanda mchele wale wengine wamepitisha mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kwa sababu nilishaona kingele imegonga na Watanzania kwa ujumla, ni vyema tukaendelea kutambua nguvu tuliyonayo kwenye upande wa soko la bidhaa zetu, matumizi ya bidhaa kwa maana ya kupenda bidhaa zetu. Hili ni jambo ambalo litatusaidia lakini kama tutategemea vya wenzetu na wenzetu wakategemea vya kwao ni dhahiri kwamba sisi vya kwetu vitakosa soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata Bungeni kanuni zetu hizi tulizoweka kama sisi wanaume zinatutambua tu kwamba tunatakiwa tuje tumevaa hizi western suit, mngetafuta siku nyingine mseme Wabunge wa kiume tungeruhusiwa mashati ya vitenge yanayotokana na bidhaa za kwetu hapa, unakuwa nadhifu na shati la Kitanzania, lakini siyo hii ambayo ipo kikanuni kabisa kwamba, lazima uje na suti ya kimagharibi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.