Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi na mimi niweze kujibu majibu ya Serikali kupitia mawasilisho ya Kamati hizi mbili; Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC).

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa michango mingi ambayo Wabunge wamechangia lakini nianze kwa kusema kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko makini na imejipanga. Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli inatambua ilipo, inatambua Tanzania iko wapi, inawajua Watanzania wote na mahitaji yao, inatambua inatoka wapi na inakwenda wapi lakini pia inatambua mahusiano ya nchi yetu ya Tanzania na dunia. Hilo huwezi kulijua kama utabaki huko uliko. Nimpongeze sana Mbunge wa Jimbo la Serengeti, Mheshimiwa Chacha Ryoba ni muda mfupi amekuja na ameshatambua tatizo alilokuwa nalo akiwa huko na sasa yuko huku anaelewa maana ya nchi nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Bunge ni kutunga sheria na sheria hizi utekelezaji unafanywa na Serikali. Pia kazi ya Bunge ni kusimamia na kushauri Serikali lakini inatekeleza hayo kupitia kwenye miundo ambayo imewekwa na Bunge lenyewe. Sasa hivi tunajadili Kamati hizi mbili na taarifa tunayoijadili iko ndani ya vitabu hivi vya Kamati, jana tulichambua taarifa za CAG. Sasa wakati mwingine unaona mtu anajadili kitu ambacho hakipo ndani ya hizi taarifa lakini ni kwa sababu tu ungekuwa umeshakuja huku haya usingeyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wameshayazungumza kwenye umma, basi nitayajibu. Nianze na ATCL. Wabunge wa Chama cha Mapinduzi nashukuru sana kwamba mmesaidia kulizungumza hili. Kwa sababu Shirika la Ndege usiliangalie kwenye kitu kimoja tu kwamba halijaleta faida, tena faida yenyewe bado haijapitiwa na CAG ili uweze kupewa taarifa kwamba kuna faida au kuna hasara. Shirika letu la Ndege limejipanga lina Business Plan na waendesha ndege (pilot) mpaka sasa hivi tunao 50 na ni ndege zote kuanzia kwenye Dreamliner mpaka Bombardier Airbus. Tutaendelea na ununuzi wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwape tu faida, kila ndege tunayonunua mikataba tunayoingia ni pamoja na ufundishaji wa ma-pilot. Kwa hiyo, tuna mpango ambao ni endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewaambia kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi imejipanga. Ndiyo maana sasa hivi inakarabati gereji ya KIA ambayo itakuwa gereji kwa ajili ya matengenezo ya ndege. Serikali ya Chama cha Mapinduzi imejipanga ndiyo maana Chuo cha NIT tunajenga ndiyo kiwe Chuo Kikuu cha Aviation ambapo mafundi wa kutengeneza ndege watafundishwa (maintenance engineer) lakini pamoja na ma-pilot.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ester Bulaya ametoa taarifa sijui amezipata wapi…

MBUNGE FULANI: Kwako.

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Wewe shemeji yangu Mheshimiwa wewe, hatuchukui mambo ya mitaani, bado hatujaenda kutengeneza hizi ndege ili tuweze kujua tumetumia shilingi ngapi lakini bado CAG hajapitia haya ili tuweze kujua kama kuna faida ya shilingi bilioni 4, umeyapata kutoka kwenye kitabu kipi, hata mimi mwenyewe Waziri sijui. Haya ni mambo ya mitaani na wewe ni Mbunge mzoefu siyo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na taaarifa nazo naona kama ni za kutoka mitaani, watu wanazungumzia PUMA. PUMA sina taarifa kwamba yeye ndiyo ana monopoly ya biashara ya mafuta duniani. Vivyo hivyo sina taarifa kwamba PUMA ana monopoly ya mafuta Tanzania. Waheshimiwa Wabunge, Bunge limetunga sheria na sheria hizo zinatekelezwa na Serikali kwamba mtu anayepewa mkataba wa ku-supply mafuta ya ndege anapewa muda, kuna siku ya kwanza mpaka siku ya mwisho na ikifika siku ya mwisho anafanyiwa evaluation kama anaenda vizuri ataendelea, kama haendi vizuri basi sheria ndiyo zinazosema kwamba hawezi kuendelea. Sasa nitashangaa kama Bunge au Mbunge ndiyo anayesimamia kwamba PUMA apewe leseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Waheshimiwa Wabunge acheni Serikali ifanye kazi yake, na Serikali hii ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, iko makini kama mnavyoona Mawaziri wake hawalali, kila mtu anafanya kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Engineer Kamwelwe, kabla ya…

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, taarifa zote mbili.