Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwenye taarifa hizi mbili, kuna mambo yanayohusu maboma na mimi nimepewa dhamana ya kusimamia elimu upande wa TAMISEMI kama Naibu Waziri, lakini nataka niseme tu kwamba huwezi kuwa unakula keki wakati huo huo tena unataka ibaki kama ilivyo. Kwa hiyo, kama unaamua kufanya miradi mikubwa kama kununua ndege sita, mradi wa umeme wa maji kule Rufiji, reli ya umeme na vitu vingine, lazima kuna baadhi ya mambo yapungue, tukubaliane hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, nilitaka niwaombe Waheshimiwa Wabunge, maboma ni kweli kazi imefanywa na Ofisi ya TAMISEMI, tuna maboma nchi nzima zaidi ya 8,110, ambayo inahitaji takribani shilingi bilioni 140. Kazi imefanyika na mipango ya Serikali sasa ni kupeleka fedha kukamilisha maboma haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, maelekezo yametoka kwenye Halmashauri zote kwamba kila Halmashauri na ndugu yangu Mheshimiwa Silinde alikuwa anazungumza Momba imeelekezwa asilimia 40 ya fedha ya mapato ya ndani ziende kwenye huduma za kijamii ikiwepo elimu. Sasa Mheshimiwa Mbunge angetusaidia yeye amesimamia imeenda asilimia ngapi katika eneo lake. Kwa hisani ya Mheshimiwa Rais Magufuli, Momba imeongezeka uandikishaji darasa la kwanza kutoka asilimia 61 mpaka asilimia 83.1. Analeta fedha nchi nzima kila mwezi, zaidi ya shilingi bilioni 9 shule ya msingi, zaidi ya shilingi bilioni 20 sekondari, shilingi bilioni 5 ni posho ya watendaji kwa maana ya Wakuu wa Shule, Walimu Wakuu na posho ya madaraka kwa watendaji. Serikali hii pia imepeleka pikipiki kila Kata karibu nchi nzima ili wakasimamie elimu na kuboresha ubora wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa wanapozungumza habari kwamba kuna miradi imekwema, tumekataa misaada na mikopo ya masharti. Tutapokea mikopo ile ambayo haitutwazi utu wetu na haitudhalilishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunavyozungumza tangu tumeanza Mradi wa EPforR zimeshaenda fedha zaidi ya shilingi bilioni 98. Mwezi huu Waheshimiwa Wabunge mtaangaliaangalia kwenye Majimbo yenu, tumepeleka fedha shilingi bilioni 53.34 kwenye EPforR kujenga madarasa, mabweni, nyumba za walimu na vitu vingine kadha wa kadha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza tuna miradi mbalimbali nchi nzima inayotekelezwa na wafadhili na mabilioni ya fedha yanakuja mfano Mradi wa Tusome Pamoja na kadhalika. Wafadhili hao ni World Bank, Uingereza na Sweden ambapo wametoa fedha na tunaenda nao sawasawa. Kwa hiyo, miradi iliyopangwa chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe itakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niseme hapa jambo la msingi sana. Waheshimiwa Wabunge, mimi nimesikiliza michango hapa, hizi ni Kamati za Bunge na niwashauri ndugu zangu wa Upinzani na mnisikilize vizuri yako mambo ambayo ukiyasema vizuri Serikali itapokea lakini ukianza vibaya utamaliza vibaya, ukianza vizuri utamaliza vizuri. Unaweza ukawa na hoja nzuri sana lakini namna ambavyo unai-present kwa kukashfu haitapokelewa, watu wataipinga, ndiyo maana watu wana-react kwa sababu ya hoja ambazo zinakuja upande wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi katika hali ya kawaida kwa Mtanzania yeyote na hii lazima muifanyie kazi, kwa kazi ambazo anafanya Mheshimiwa Magufuli Watanzania wote wameshakubali mmebaki nyie tu na nyie ni wachache. Kwa mfano, alipokuwepo Mheshimiwa Kikwete alisemwa vibaya kama mnavyozungumza leo, leo mnasema Mheshimiwa Magufuli na wenzake wakitoka wataenda mahakamani haya maneno ni maneno ya kawaida, kelele za chura hazimnyimi ng’ombe kunywa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Wabunge wa Chama cha Mapinduzi, hoja za upinzani zimeisha nchi hii, sasa hoja ni za kuungaunga, tuchape kazi, tujipange, tujifungie, tupokee maoni ya Kamati tukatekeleze. Tukienda kwenye uchaguzi tunataja hoja mnatoa maneno, Watanzania watapanga wanachagua maneno au wanachagua vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naomba niwasilishe. (Makofi/Vigelegele)