Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii muhimu kuchangia hoja tuliyonayo ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa, lakini pia na kwa maendeleo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia kwa kueleza dhana moja; na niseme kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati. Kwa hiyo, hoja ambayo napenda kuanza nayo ni kwamba ukiangalia taarifa mbalimbali za Benki ya Dunia, ukaangalia taarifa mbalimbali zinazotolewa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) na taarifa mbalimbali ambazo tumepokea kwenye Kamati, zinabainisha kwamba uchumi wa Tanzania na baadhi ya nchi nyingine ndani ya Sub-Saharan Africa umekuwa ukikua kwa kasi kati ya chumi zinazokuwa kwa kasi. Ni jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wachumi tunafahamu kwamba katika uchumi huwa jambo moja likiwa jema huwa inamaanisha usiangalie hilo tu, huenda kuna jambo lingine jema zaidi. Sasa hatari ya uchumi, ukijikuta sana kufurahia jambo ambalo unaona ni jema ukasahau kwamba kuna lingine ambalo ni jema zaidi, basi unaweza ukajikuta unaendelea kuwa pale pale unafurahia na hilo dogo ambalo unafikiri ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kazi ya Bunge ni kushauri. Kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali kwamba pamoja na ukweli kwamba uchumi wetu ni kati ya chumi zinazokua kwa kasi zaidi, lakini lazima tujue kwamba suala la uchumi kukua kwa kasi zaidi ni jambo moja, lakini kuna suala lingine uchumi huo una ukubwa kiasi gani? Kwa lugha nyepesi tunasema, the size of the economy matters more. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili ili tuelewane, nitalieleza vizuri. Ukiangalia uchumi wa Marekani kwa mfano, GDP yao size ni 22 trillion US Dollars. Ukiangalia Ubelgiji, nchi ambayo ni ndogo, ukubwa wake ni square kilometers 36,000; ukiangalia Tanzania, ukubwa wa nchi yetu ni karibu 945,000 square kilometers. Kwa hiyo, utaona Wabelgiji wao GDP yao ni 540 billion US Dollars. Tanzania tunajitahidi, lakini ni 60 billion US Dollars.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uchumi wa Ubelgiji ukikua hata kwa asilimia moja, maana yake kwao ni jambo kubwa. Uchumi wa Marekani hata ukikua kwa asilimia 0.5, maana yake hilo ni jambo kubwa. Kwa hiyo, hizi sifa za Benki ya Dunia na mashirika ya fedha duniani na wachumi wengi waliobobea wakikwambia wewe uchumi wako unakua kwa kasi na wewe ukafurahia ukapumzika, inawezekana ukawa haufikirii sawa sawa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachumi tuko ndani ya Bunge hili kushauri, ni lazima tuikumbushe Serikali kwamba ni vyema uchumi ukue vizuri, ni jambo jema, lakini kuna jambo lingine tunaweza tukafanya zaidi. Jambo hili ni lipi? Tuangalie size ya uchumi wetu, tuangalie radical changes zipi tunaweza tukafanya ili walau ku-double uchumi wetu. Tunasema, radical changes. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa kuna neno mara nyingi linaitwa continuous improvement. Mimi sio muumini wa continuous improvement kwa sababu mtu akikwambia uendelee kufanya continuous improvement, maana yake anakwambia uendelee kuonekana unaboresha kidogo kidogo lakini uendelee kukaa pale pale. Tunachohitaji ni kitu kinaitwa radical change. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa radical change mojawapo ambayo tumeanza kufanya ambayo nitaomba niipongeze Serikali, kwa mfano, kufanya maamuzi ya makusudi kabisa kwamba sasa tunataka tuwekeze kwenye Stiegler’s Gorge tuzalishe Megawati 2,100, huo uamuzi ni radical change. Hawa rafiki zetu wa Benki ya Dunia, hawatakaa wakupongeze. Hawa watu wa Mashirika ya Fedha Duniani hawatakaa wakupongeze. Hawa wataalam wetu, wachumi wazuri sana wa huko pengine, hawatakaa wakupongeze, kwa sababu wanajua unachokifanya ni radical change. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine ni standard gauge. Niseme tu, nilipata bahati wakati fulani kuwa Mwenyekiti wa Mawaziri wa Afrika Mashariki, sasa Wajapani tuliwapa kazi ya kutushauri kwamba je, hii standard gauge nchi za Afrika Mashariki tunaweza kufanya au tusifanye? Basi wakatoa fedha za kufanya utafiti ule; Wajapani hao, wakaja na utafiti wakasema, hizi nchi za Afrika Mashariki standard gauge ninyi bado sana. Mwendelee tu na hizo reli zenu mlizonazo msonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikamwuliza Mheshimiwa Rais, unajua ukiwa Waziri wa Afrika Mashariki au Mambo ya Nje, wewe siyo Waziri; Waziri ni Rais. Kwa hiyo, huwezi ukafanya jambo bila kumwuliza Rais wako. Nikamwuliza, tunaenda kufanya uamuzi, tufanyeje? Akaniambia msimamo wa Cabinet si unaujua? Nikasema ndiyo. Akasema, ni standard gauge, hao Wajapani wasiwadanganye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilipofika pale kwenye kikao nikatumia Uenyekiti wangu vibaya, nikamwita Waziri wa Kenya nikamwambia unajua ni standard gauge. Unasemaje? Bwana yule akasema Mheshimiwa, lakini standard gauge nadhani Wajapani hawa wametupa hela, wamefanya na utafiti; nikasema sikiliza, hiyo siyo sahihi, ni standard gauge. Kwa hiyo, tulipoingia kwenye kikao, nilichofanya, nikawapeleka haraka haraka, wala sikuhoji sana, nikapitisha uamuzi ukaja wa standard gauge. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo napenda nichangie ni kuhusu matumizi ya fedha za maendeleo. Ukiangalia taarifa tuliyopokea ya fedha za maendeleo jinsi zinavyotolewa, ukisoma vizuri na ukawa mkweli, lazima ushauri kwamba utolewaji wa fedha za maendeleo zinavyotolewa hazitolewi sawa sawa. Kwa nini? Ukiangalia fedha za maendeleo, kwa mfano, Wizara ya Mambo ya Ndani imepata asilimia 202 ya kile kilichokusudiwa. Sasa ni jambo jema ukiipa asilimia 202, sitaki kuuliza wamefanya nini Mambo ya Ndani, lakini sasa unapoanza kuangalia sekta nyingine ambazo unaona ni muhimu, unaona fedha za maendeleo hatujawapa kama ambavyo tulitarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Maliasili na Utalii hatujawapa hata shilingi moja za fedha ya maendeleo; siyo jambo jema hilo. Ukiangalia Wizara ya Afya tumewapa asilimia 14 peke yake, fedha za maendeleo; siyo jambo jema sana; ukiangalia Biashara na Viwanda tumewapa asilimia 6.96. Sasa kama tunajenga Tanzania ya Viwanda, mtu yeyote angetarajia sasa kwenye viwanda fedha ya maendeleo utapeleka nyingi. Siyo jambo jema pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia energy, Wizara ya Madini, tumewapa asilimia 10, siyo jambo jema pia; ukiangalia National Land Use Planning, kitu ambacho ni muhimu, tumewapa asilimia sifuri, siyo jambo jema. Sasa nafikiri kama Mbunge na kama mtu unakuwa mkweli, ni vizuri kuyasema haya. Hatujamaliza mwaka wa fedha, tuna miezi sita mingine inayokuja, basi tumshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha aangalie afanye itakavyowezekana ili hizi sekta muhimu ambazo hazijapata chochote basi ziongezewe zipewe fedha nyingi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lugola nadhani yuko humu ndani, ni rafiki yangu ananifahamu, tumefanya wote kazi, hizi asilimia 202 ulizopewa, mimi nadhani zinatosha, hebu sasa tupeleke fedha kwenye sekta nyingine ili tuweze kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambali napenda nilichangie, ni muhimu sana. Ukisoma taarifa tulizopokea, kwenye ongezeko la mikopo, tunasema fedha za mikopo imeongezeka kwa asilimia 63 kwa sekta binafsi, kwenye madini imeongezeka kwa asilimia 9.8 na kwenye viwanda imeongezeka asilimia 4.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake ni nini? Ukiangalia hii asilimia 63 iliyoongezeka kwenye mikopo binafsi, hii ni mikopo kwa sababu watu ni wafanyakazi wanapewa mikopo ile ya mishahara; na ukiangalia hawa siyo kwamba wanakwenda kuwekeza. Hii ni mikopo ya kujikimu. Sasa kama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)