Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa rehema zake na neema zake, mimi na wenzangu humu ndani hatujambo na tunaendelea na wajibu wa kuwakilisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Makamu wake kwa maana ya Naibu Waziri kwa kadri wanavyofanya kazi na wanavyosimamia masuala ya uchumi wa nchi yetu. Niseme awali kabisa napongeza mpango huu naunga mkono pia hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze na suala la kilimo. Ukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa saba, kuna mahali anaonyesha kwamba mfumuko wa bei uko chini ya numeral asilimia tano. Sasa mfumuko huu wa bei wote tunajua kwamba kinachosababisha mfumuko wa bei uwe katika hali hiyo katika nchi yetu ni upatikanaji wa uhakika wa chakula kwa maana ya mahindi na mchele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama kweli tunataka wananchi wa nchi hii pamoja na mfumuko wa bei hii, kuwa chini namna hii waishi maisha yenye furaha basi tuwasaidie wakulima hawa. Wakulima hawa wanaishi maisha ya dhiki sana, mahindi yao hayana soko, pamoja na kwamba mahindi haya ndio yamewezesha nchi hii sasa mfumuko wa bei kuwa chini, lakini hali ya mbolea ni mbaya sana na hali ya pembejeo ni mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia mahali pengine nimeona kwenye mpango anaeleza kwamba kutakuwa na uunganishaji wa matrekata ya kutosha, lakini ukifanya utafiti mdogo tu makampuni yote ya matrekta yaliyopo Tanzania unayoyafahamu, hakuna kampuni inayouza trekta zaidi ya 200 kwa mwaka mzima. Na leo hii pale Kibaha, kuna yale matrekta mekundu yale wanalalamika kwamba hawajui watayauzaje kwa jinsi yalivyo mengi. Hebu tujaribu kuona tunalinganishaje mahitaji wa wakulima ya matrekta na uwezeshaji kutoka kwenye taasisi za kibenki. Lakini mikopo yetu mingi mikopo rafiki kwa wakulima, mabenki mengi yamekuwa na riba ya juu sana, lakini ukienda kwenye mabenki wanasema sisi kama benki hatuna riba ya juu, riba hii imewekwa na Serikali. Sasa Serikali mnataka nini, mnataka wakulima waneemeke, mnataka kupata hela nyingi kutoka kwenye riba. Hili ni jambo ambalo mnatakiwa mliangalie kama mkulima hawezi kukukopa benki na kulipa mkopo huo, maana yake hayo matrekta hayawezi kununulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana wakulima wa mahindi wapate uangalizi maalum ufanywe utaratibu maalum wa masoko, ni kweli tunahitaji mahindi kwa chakula katika nchi, lakini vile vile tunahitaji wakulima hawa waneemeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la mnafahamu kabisa sisi kama nchi tunahitaji fedha ya kigeni. Katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini sasa hivi liko zao la parachichi. Zao hili limekosa watalaam, hebu niombe sana Serikali muangalie namna gani sasa mtazidisha wataalam kwenye hili zao kwa sababu hili zao ndio linaleta fedha za kigeni sasa. Matokeo yake sasa ni kwamba kila mteja anayekuja anakuja na standard zake, anakwenda kwa mkulima mwingine anasema ananunua parachichi kubwa, mwingine anasema ananuna parachichi ndogo, kwa hiyo kila mtu sasa amekuwa anaamua anachokitaka.

Lakini sio hiyo tu, hatuna nyumba maalum za kuhifadhia maparachichi kwa maana ya park house, lakini vilevile kuna tatizo la vifungashio vya mazao kama parachichi. Vifungashio vinakuwa imported lakini vina kodi kubwa na kadhalika. Kama kweli parachichi linaleta fedha ya kigeni basi naomba sana msaidie kama Serikali kuona kwamba zao hili sasa linapata mstakabali mzuri ili kusudi, wakulima wengi waneemeke, lakini vilevile hata nchi iweze kupata fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la miradi ya maji. Tunafahamu kwamba hatuwezi kufanya maendeleo kama hatuna maji. Lakini tunalo tatizo kubwa sana kwenye miradi ya maji, tuna fedha ambazo miaka yote tumesema ziko ring-fenced kwa ajili ya miradi ya maji. Lakini ukiangalia Waziri wa Maji au Wizara ya Maji hailipi wakandarasi on time, inachelewa sana kuwalipa wakandarasi. Hakuna mkandarasi tajiri Tanzania anafanya kazi ya maji, Makandarasi wanaofanya kazi ya maji ni makandarasi wenzetu tu malofa malofa tu, ananunua mabomba, analaza mabomba, akimaliza kulaza mabomba na yeye mwenyewe ameishiwa, aki-raise certificate Wizarani certificate ni miezi mtatu mpaka miezi minne, haiwezekani. Miradi hii haiwezi kukamilika hata kama tunasema tunataka kumtua mama ndoo haiwezekani, utamtuaje ndoo mkandarasi halipwi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba sana Serikali iangalie kwamba tunapopanga hii mipango tunaposema kwamba tunawapa wakandarasi kazi halafu wakandarasi wakishafanya kazi wa-raise certificate walipwe basi walipwe kwa wakati. Mkandarasi anatoa certificate miezi mitatu halipwi, tuliangalie sana hilo ili tuweze kusaidia.

Jambo lingine kwenye miradi, tunayo miradi ambayo ni miradi ya kuendeleza miji. Miradi hii ina mikopo kutoka World Bank, lakini miradi utekelezaji wake umekuwa ni wa mateso makubwa sana kwa Halmashauri zetu. Wanajenga stand, wanajenga masoko, wanajenga barabara, lakini wakandarasi kwenye mikataba wameandikiwa kwamba kutakuwa na msamaha wa kodi. Lakini unapopeleka msamaha wa kodi Wizarani, msamaha hautoki. TAMISEMI imefanya semina, imewaita watalaam wa Wizara ya Fedha, imeita wataalam sijui wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali wamewapa semina, wamewaelimisha wanaanza kutekeleza yale waliyowaelimisha ukifika Wizara ya Fedha hakuna msamaha wa kodi.

Naomba sana kama tunapanga mipango yetu, tunawapa watu semina tujue kabisa zile semina ni gharama ya Serikali, na ni fedha ile tunaipoteza. Kwa hiyo, tunapoanza utekelezaji miradi hii basi mara moja msamaha wa kodi uweze kutoka na miradi iweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije suala la biashara. Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, biashara nyingine ambayo wanafanya ni biashara ya mazao ya misitu. Lakini sisi kama Watanzania kama kweli tunataka maendeleo kwenye hizi biashara, hebu tuangalie style yetu ya kufanya biashara. Mazao ya misitu ya Nyanda za Juu Kusini ni mazao ambayo yanatokana na misitu ya kupandwa ambayo ni mbao, nguzo, magogo mbalimbali, fito na mijengo mbalimbali. Lakini iko sheria ya maliasili ambayo inakataza mazao ya misitu yasitembee usiku. Sasa unajiuliza sheria hiyo ni nzuri sawa, lakini mfanyabiashara anabeba mzigo kutoka Nyanda za Juu Kusini kwa maana ya Njombe, amebeba mbao, halafu akifika karibu anakaribia Dodoma kama mitaa ya huko Mpunguzi, saa 12 jioni ikifika lazima asimamishe gari alale pale. Lori la mzigo lililobeba mbao, lililobeba nguzo, lililobeba fito, linasimamishwa lilale hata kabla hata kuku hawajaingia kulala. Hivi kweli sisi tunataka kufanya maendeleo tunataka kufanya nini. Kama gari la mizigo limekaguliwa njia nzima toka alikotoka na mzigo amekaguliwa lakini anafika Mpunguzi ambako hazizalishwi mbao, haizalishwi nguzo, hakuna miti ya kupandwa lakini anapaswa kulala hapo mpaka asubuhi saa 12 jioni, aendelee na safari.

Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama unataka watu wawe na fedha na watu wafanye biashara, vikwazo vidogo vidogo kama hivi muwe mnavifuta mara moja ili kusudi watu wafanye biashara. Mimi sioni kama kuna sababu yoyote ya kuzuia watu wanaosafirisha mazao ya msitu hayakupandwa baada ya saa 12 jioni. Kwanza ameambiwa gari unayotumia kusafirishia liwe la wazi, amefanya gari limekuwa la wazi, usifunike na turubai, hajafunika na turubai, lakini bado anaambiwa saa 12 jioni mwisho. Ukikutwa na gari imebeba mbao saa 12:05 unapigwa faini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la elimu. Tunaiendea sana Tanzania ya viwanda, naomba sana Serikali iangalie uwezekano wa kuwa na vyuo vya uwalimu wa ufundi ili kusudi sasa waweze kutoka Walimu wengi waweze kufundisha katika shule zetu ili tuweze kupata mafundi wengi vinginevyo viwanda hivi tutawafanya vijana wetu wawe watwana, wawe watu wa kupakia maboksi, kufagia viwanja na kuchimba mashimo ya takataka. Lakini kama tunataka vijana hawa wafanye kazi za kitaalam viwandani ni kazi za ufundi. Kwa hiyo kazi ya kwanza ni tupate walimu wa kutosha wa Ufundi na waweze kutoa elimu kwa wanafunzi ili waweze kufanya hizo kazi za ufundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa walimu wa sayansi hali ni mbaya sana wewe shule ni ya sekondari miaka 10 lakini haina mwalimu hata mmoja wa physics naomba sana hilo liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.