Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika mpango. Kwanza kabisa nianze kwa pongezi. Naipongeza Serikali kwa kutekeleza mpango ambao tuliupitisha hapa mwaka 2017, leo tunaona uanzishwaji wa ujenzi wa Standard Gauge unaendelea, napongeza sana, pamoja na kwamba kuna baadhi ya watu wanasema Standard Gauge tunaizungumzia kwenye muda wa kusafiri tu. Sisi watu wa Tabora na mikoa mingine tunarajia Standard Gauge itakuja kutusaidia katika usafirishaji wa haraka na bei nafuu wa mazao yetu, mfano tumbaku na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza pia ununuaji wa ndege unaofanyika. Tulikuwa tunasema ni tatizo kubwa sana, lakini sasa Shirika letu la Ndege linaelekea kuja kuchangia katika uchumi wa nchi yetu, lazima nipongeze hili. Tuna ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya nchi nzima. Limekuwa ni kelele sana na tumekuwa tunalizungumzia sana hili, lakini Serikali yetu sikivu imeanza kukarabati vituo vya afya takriban 200 sasa katika maeneo yetu. Vilevile kuna ujenzi wa Hositali za Wilaya, zimetoka takribani shilingi bilioni moja na nusu katika Wilaya zetu na ujenzi wa Hospitali za Wilaya unaendelea. Ni utekelezaji wa mipango mizuri ambayo tuliipanga mwaka uliopita na sasa inaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miundombimu tumeshuhudia ujenzi wa barabara kubwa nchi nzima. Pia flyover za Dar es Salaam, zinasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamo. Kuna ujenzi unafanyika Mkoa wa Tabora, tulikuwa tunasema sana barabara kubwa ya Chaya
- Nyahua ambayo inaunganisha karibu mikoa mitano ya Kanda yetu huku, ujenzi wake umefikia asilimia 30. Mipango yote hii ilikuwa mizuri na sasa inatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri, nilikuwa na machache ya kushauri. Nikianza na eneo la utangulizi la Mheshimiwa Waziri, nina maeneo matatu ya kuzungumzia. La kwanza ni vipaumbele ambavyo vimewekwa katika hii miaka mitatu ya mpango wetu. Moja la vipaumbele ni suala la viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda vyetu. Hapa nilitaka nizungumzie maeneo mawili tu kwa kifupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni SIDO. Unapozungumzia SIDO ni eneo ambalo linasaidia uchumi mdogo wa maeneo yetu ya vijijini. Katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Mipango, amezungumzia kilimo kilivyokua kwa 7% na kusaidia usalama wa chakula, kupunguza mfumuko wa bei, ku-stabilize uchumi na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kilimo kiende vizuri pamoja na upelekaji wa mbolea na upatikanaji wa masoko na kadhalika, lakini kilimo chenyewe kinahitaji zana za kilimo. SIDO wanatengeneza majembe ya ng’ombe ambayo tunayatumia sana vijijini, wanatengeneza mashine za bei rahisi za kusagia na kukamulia mafuta na kadhalika. Nina hakika SIDO ikiwezeshwa, wananchi wetu watanufaika sana na uchumi utazidi kukua katika maeneo yetu ya vijijini ambao unakuja kuchangia katika uchumi mkubwa wa nchi hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka Serikali iliangalie sana ni CAMARTEC. CAMARTEC ni Kituo cha Zana za Kilimo na Teknolojia Vijijini ambacho kipo Arusha. Watu wengi hawaifahamu CAMARTEC lakini wanatengeneza zana za kilimo na teknolojia za vijijini, ni sawasawa na SIDO. Hawa wanatengeneza mashine za kupandia mbegu za mazao mbalimbali ikiwemo tumbaku, korosho na kadhalika. Pia wanatengeneza kwa bei nafuu mashine za kusagia karanga na nafaka nyingine. Nasisitiza kwamba mpango huu uangalie sana haya maeneo mawili kwa maana ya SIDO na CAMARTEC ili kusaidia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo limepewa kipaumbele katika mpango ni kufungamanisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu. Hapa naomba nipongeze upatikanaji wa huduma bora za afya vijijini kwetu. Kama nilivyosema ili wananchi waone ukuaji wa uchumi wao, zile huduma mbalimbali lazima zionekane zinapatikana katika maeneo yetu. Siyo tu kupata fedha mfukoni, lakini unapozungumzia huduma za afya, leo upatikanaji wa dawa ni asilimia takribani 80 katika maeneo yetu. Tumeongeza bajeti ya dawa na dawa zinapatikana. Mheshimiwa Dkt. Mpango katika hili nakupongeza. Pia naipongeza Serikali kama nilivyosema katika suala la ujenzi wa vituo vya afya na hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza pia ujenzi wa barabara kuu zinazosaidia usafirishaji na ufanyaji wa biashara kwa gharama nafuu. Nimesema barabara zinatengenezwa, lakini hapa naomba nizungumzie suala la TARURA. TARURA inatengeneza barabara zetu ndogo kuja katika barabara kuu. Ili mkulima asafirishe mazao yake kwa gharama nafuu ni lazima barabara zetu za vijijini ziwe nzuri. Leo tusipoiwezesha TARURA hata hizi barabara kubwa tunazozijenga zitakuwa hazina manufaa makubwa sana kwa wananchi wetu. Naomba tuiwezeshe TARURA ili barabara zetu zipitike vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hilo hilo, kuna suala la upatikanaji wa maji safi na salama. Nimeona tunachimba visima katika maeneo mengi, lakini nashauri tuangalie uchimbaji wa mabwawa makubwa yatakayosaidia upatikanaji mkubwa wa maji tukiyawekea miundombinu. Yako maeneo yanayowezekana kuwekewa miundombinu hiyo, tuwekeze katika uchimbaji wa mabwawa makubwa na kuyawekea miundombinu ili kusaidia wananchi wetu katika maeneo mbalimbali. Mpango pia uangalie kwenda kukamilisha miradi ya maji ambayo imeanzishwa vijijini na imekwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nataka nishauri, kama kweli kilimo kinasaidia katika uchumi wetu, tuwekeze katika mpango wa kilimo cha umwagiliaji. Tukiwekeza katika kilimo cha umwagiliaji tuna uhakika wa kupata mazao mengi zaidi, maana tutapa fedha zaidi kwa wakulima wetu, kodi tutapata nyingi na vilevile usalama wa chakula utaongezeka na uchumi wa nchi yetu utaongezeka. Sijaona mpango uliozungumzia kilimo cha umwagiliaji, mwaka jana nilisema na mwaka huu narudia kusema, tunayo maeneo mazuri ambayo yakitengenezewa miradi ya umwagiliaji itatusaidia sana. Kwa hiyo, nashauri mpango uangalie eneo la umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, REA ni sehemu ambayo inahitajika sana kuwekeza. Naomba tuongeze fedha katika miradi ya REA, pamoja na juhudi zinazofanyika za kuongeza upatikanaji wa umeme kwa miradi, mfano Stiegler’s Gauge. Tukiwekeza katika REA maeneo yetu ya vijijini yakapata umeme wa uhakika, tutakuwa na teknolojia ya kisasa ya gharama nafuu ya kusaidia uzalishaji kwenye maeneo yetu. Kwa kweli miradi ya REA bado inasuasua kwa sababu ya kukosekana kwa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la tatu la uboreshaji wa mazingira wezeshi kwa uendeshaji wa biashara na uwekezaji. Kwanza naipongeza Serikali, tulishauri uboreshaji wa bandari zetu ikiwemo ya Dar es Salam. Sasa hivi Bandari ya Dar es Salaam inaboreshwa, inaongezwa kina, maana yake ufanyaji wa biashara katika eneo lile unaweza ukasaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo moja la blue print. Tumeandaa blue print ili kusaidia mazingira ya uwekezaji katika nchi yetu ya Tanzania...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)