Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu. Awali ya yote napenda kupongeza Wizara ya Fedha kwa kazi wanazofanya ikiwemo za upelekaji fedha katika Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika kitabu cha hotuba ukurasa wa 32 Wizara imetoa mafunzo kwa Maafisa Ugani na Ununuzi 75 kwa ajili ya mafunzo ya kutumia mfumo wa malipo wa Serikali EPICOR. Hata hivyo, mafunzo haya hayatakuwa na tija kama Serikali haitarekebisha upungufu uliomo katika mfumo wa EPICOR, kwa sababu mfumo huu unatumia cash basis. Kwa hiyo LPO sasa hivi zinaandaliwa kwa kutumia cash tu, asilimia kubwa ya LPO zinatumiwa nje ya mfumo, kwa hiyo dhana zima ya internal control au udhibiti wa ndani haipo.

Mheshimiwa Spika, upungufu mwingine pia upo ikiwemo asset management bado hazijawekwa humo, naishauri sasa Wizara ione namna inavyoweza kutekeleza kuweza kuingiza package ambazo zinazopungua katika mfumo mzima wa EPICOR.

Mheshimiwa Spika, nishauri pia Wizara ijitahidi kuweka mfumo ambao utaweza ku-link mifumo mbalimbali kama PLANREP ili sasa taarifa mbalimbali ziweze kutoka katika mfumo wa EPICOR badala ya taarifa nyingine kutengenezwa nje ya mfumo ama taarifa baadhi za ufungaji wa hesabu zikafanyikia nje ya mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia niipongeze Wizara kwa namna inavyopeleka fedha za elimu bila malipo, inapeleka vizuri, nimeangalia katika kitabu cha CAG hoja iliyopo ni ndogo tu shilingi bilioni moja haikupelekwa na upungufu huu ulitokana na Wizara yenyewe kule ya Elimu ambako kulikuwa kuna utofauti wa takwimu. Kwa hiyo, naipongeza kabisa kwa namna inavyopeleka fedha za elimu bila malipo. Niipongeze pia Wizara kwa kupeleka fedha za ujenzi wa vituo vya afya au kuboresha vituo vya afya. Vituo vyetu sasa hivi vilivyoboreshwa vina hadhi nzuri kiasi kwamba wananchi sasa hivi wana mvuto wa kwenda hospitali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, nipongeze pia kwa namna inavyopeleka halmashauri ruzuku za matumizi ya kawaida. Kumekuwa hakuna na matatizo ya upelekaji wa ruzuku za kawaida, lakini tukumbuke kwamba ruzuku hizi zilipunguzwa kutoka asilimia 100 mpaka 40. Ukiangalia pale pale mahitaji ya halmashauri yako pale pale, stahiki za watumishi ziko pale pale, mtumishi anatakiwa aende likizo, mtumishi anatakiwa agharamiwe masomo.

Mheshimiwa Spika, kwa kupunguza hiyo asilimia kutoka 100 mpaka 40 kumekuwa na changamoto kubwa sana inayozikumba halmashauri katika upungufu wa fedha. Pamoja na hayo halmashauri zilitegemea sasa wangetumia fedha za mapato ili kuweza ku-accommodate shughuli za idara zinazopata ruzuku.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ilizozikumba halmashauri ni mapato mengine kuchukuliwa na Serikali Kuu na mapato mengine kupunguzwa. Kwa mfano, Mkoa wa Simiyu ushuru wa pamba ulipunguzwa kutoka asilimia tano hadi tatu kwa ajili ya standardize bei ya pamba. Halmashauri za Mkoa wa Simiyu zaidi ya asilimia 60, bajeti yake inatumia ushuru wa pamba.

Mheshimiwa Spika, changamoto zimeendelea kuzikumba halmashauri kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli zake. Ukiangalia kazi ziko pale pale, Waheshimiwa Madiwani wako pale kwa mujibu wa Sheria, wanahitaji kulipwa, wanahitaji kufanya ziara, lakini saa hizi Madiwani hao wamekuwa wakikopwa fedha kwa muda mrefu zaidi hata ya miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hao hao Madiwani tunategemea wakasimamie miradi ya maendeleo. Ukiangalia sasa hivi Serikali imejikita kutumia force account hilo ni jambo jema. Hapo hapo ukiangalia force account hiyo Wahandisi wengi wemeenda TARURA. Kwa hiyo, Madiwani ambao ni Wenyeviti wa WDC wanapaswa kusimamia ile miradi. Changamoto ukiangalia wenyewe kwanza hawana fedha wamekopwa, halafu wanaenda kusimamia force account ambayo kwa kiasi kikubwa ina-involve cash, pale Serikali ifanye tathmini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba Wizara ya TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha wafanye review kwa sheria ambazo tumezipitisha. Kwa mfano wa kupunguza rukuzu ya matumizi ya kawaida kutoka asilimia 100 hadi asilimia 40, kuondoa vyanzo vya mapato, wafanye review waangalie ni athari gani zilizopo katika halmashauri. Ikiwezekana sasa halmashauri hizi ziweze kupewa fidia, kama ilivyofanyika 2013 baada ya kupunguza vyanzo vilivyokuwa kero kwa wananchi, halmashauri zilipatiwa fidia mpaka leo hiyo fidia inaletwa. (Makofi)

Mheshimia Spika, naomba pia niongelee kuhusu upelekaji wa fedha za miradi ya maendeleo, nikijikita katika ruzuku ya uendelezaji wa mitaji za Serikali za Mitaa LGCDG au inavyojulikana kwa CDG. Ni miaka mitatu sasa hivi fedha hiyo imekuwa haipelekwi, fedha hiyo ni ya Wafadhili lakini sio asilimia 100. Kuna sehemu ambayo ni fedha ya mapato ya ndani ambayo inajulikana, kama Local kuna foreign na Local. Hata hivyo, ukiangalia hata zile fedha za local hakuna fedha iliyopelekwa katika miradi ya CDG. Kama wafadhili hawaleti je, Serikali ambayo inakusanya kwa nini haipeleki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali sasa ione namna inavyoweza kuinusuru miradi hii iliyotekelezwa kwa fedha ya CDG kwa sababu kila mwaka tunaopanga wananchi lazima waibue miradi na kuianzisha kwa ule mfumo wa C-matching. Kwa hiyo, miaka mitatu tumekuwa tukilimbikiza magofu, magofu, magofu kiasi kwamba tunawapelekea wananchi wanakuwa hawana imani sasa na Serikali waanza kupoteza imani kwa Serikali. Wananchi sasa hivi wametokea kuiamini sana Serikali ya Awamu Tano, sasa tusiwakatishe tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya TAMISEMI ilifanya kikao iliwaita Waheshimiwa Wenyeviti na Wakurugenzi kwamba, waainishe miradi inayoweza kutekelezwa ambayo inaweza kumalizwa na fedha ya CDG ili sasa iletwe, lakini mpaka ninavyoongea sasa hivi fedha haijaletwa. Tukumbuke halmashauri zingine ziliitisha Mabaraza Maalum, wakatumia fedha ili kuweza kupitisha miradi ambayo sasa inaweza ikatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri tuone namna tunavyoweza kui-rescue hii miradi, mingine ina miaka 10, mingine ina miaka mitano na kama Mfadhili haleti fedha kwa nini tunaendelea kubajeti? Nashauri kama mfadhili hajaonesha nia ya kuleta basi kwenye hicho kifungu tuweke token figure ili mfadhili atakapoleta tufanye supplementary budget, kuliko kuendeleza kulimbikiza magofu, watoto wetu hawana madarasa, zahanati zetu hazijakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.