Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuchangia hoja ya hotuba ya Wizara ya Madini. Namshukuru Mungu kwa kibali hiki. Nampongeza Mheshimiwa Waziri Angellah Jasmine Kairuki kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Madini na Naibu Mawaziri wake Mheshimiwa Biteko na Mheshimiwa Nyongo. Nawapongeza pia kwa hotuba nzuri iliyozingatia masuala yote muhimu pamoja na taarifa za ziada walizotupatia kwenye makabrasha maalum na maonesho yaliyoletwa kwenye viwanja vya Bunge ambayo yametuongezea uelewa wetu juu ya sekta hii muhimu sana kwa uchumi, lakini pia kutuwezesha kutambua changamoto zake na nini kinafanyika kukabiliana nazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa hatua madhubuti alizochukua kuhakikisha kunakuwa na usimamizi na udhibiti mzuri wa rasilimali za sekta hii kwa kuunda Kamati za kukagua makinikia yanayotokana na uchimbaji wa madini na vito na hatimaye kupitisha sheria za kimapinduzi zinazoliwezesha Taifa kuipitia upya mikataba yote ya madini na vito ambayo ilikuwa ina vipengele vyenye kutiliwa mashaka ili irekebishwe na Taifa lipate mapato stahiki kutokana na sekta hii ambayo kwa muda mrefu Taifa limekuwa likipoteza mapato mengi sana. Tunamwomba Rais zoezi hili lifanywe kwa rasilimali zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, niruhusu sasa nizungumzie suala la migodi ya makaa ya mawe ambayo yanapatikana maeneo ya Kiwira Wilaya ya Ileje, Ludewa, Ruvuma, Mbinga na Songea. Makaa ya Mawe ya Ngaka, Mbinga, Ruvuma yana ubora wa juu zaidi duniani. Mgodi huo una zaidi ya tani milioni 400 za makaa ya mawe na yanaweza kuchimbwa kwa miaka 100. Kwa hivyo, ni rasilimali ya uhakika na kutegemewa sana katika mkakati wa kuzalisha chuma kwa ajili ya viwanda nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini Serikali haitilii mkazo mradi huu ambao utafungua Taifa kiuchumi na kiviwanda? Hili ni eneo ambalo Serikali itakuwa na kila sababu ya kuingia ubia mkubwa na wawekezaji wa sekta binafsi na hata kuchukua mkopo ili kuendeleza migodi hii yenye kuleta faida kubwa na mapato makubwa kwa Taifa na kuongeza umeme kwa asilimia 40 kama takwimu za dunia zinavyoonesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, makaa ya mawe ni nishati kubwa kwa kutengeneza cement, kuzalisha karatasi na kwenye viwanda vya nguo na bidhaa nyingine nyingi za viwandani pamoja na uzalishaji wa umeme. Hii pia itaokoa fedha ya kigeni iliyokuwa ikitumika kuagiza makaa ya mawe toka Afrika Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, STAMICO ndiyo iliyokabidhiwa Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira na taarifa zilizowasilishwa kwenye hotuba ya Waziri ukurasa wa 45 imeainisha kwamba STAMICO imeanza rasmi kuuza makaa ya mawe yanayozalishwa katika Mgodi wa Kabulo uliopo Ileje – Songwe kwa matumizi ya watumiaji wa viwanda wa ndani ikiwemo viwanda vya saruji na nguo. Uzalishaji wa majaribio ulioanza kwenye Kijiji cha Kapeta, Ileje tangu Aprili 30, 2017 na mpaka sasa imezalisha tani 6,197. Kiasi gani cha makaa haya yameshanunuliwa na Ileje kama Wilaya ina gawio la asilimia ngapi kutokana na mauzo hayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje inahitaji daraja la kwenye Mto Mwalisi linalounganisha Ileje na Mgodi wa Kiwira ili ipunguze gharama za kusafirisha makaa kupitia Kyela na kuwezesha makaa hayo kuhifadhiwa Ileje na vilevile kupitishwa Ileje wakati wa kupeleka kwenye viwanda vya cement na hata vya nguo vitakapoanza. Tunaomba Wizara itenge bajeti ndogo kujenga daraja hili fupi la kilomita 7 kuokoa gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu zaidi napenda kuona Mgodi wa Kiwira na Kabulo ungeendelezwa sasa na kuajiri watu 7,000 wanaotegemewa huku ingeongeza mapato Ileje na Songwe kwa ujumla. Mheshimiwa Waziri atueleze mikataba gani ipo sasa kuendesha Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira na ile ya kati ya Halmashauri ya Ileje na STAMICO.

Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji wadogo ni sehemu muhimu katika tasnia hii ya madini na wanachangia kwa kiasi kikubwa kwenye soko la ajira na kuliletea mapato Taifa na kuondoa umaskini. Wachimbaji wadogo wathaminiwe na kuwezeshwa. Maeneo wanayochimba wapewe leseni kwenye maeneo yaliyokwishapimwa rasmi na GST ili wasifanye uchimbaji wa kuhamahama unaoharibu mazingira na usiokuwa na tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, wazo la kutumia Tanzania kuwa kitovu cha vito na madini yetu ni zuri na linalohitaji kufanyiwa kazi kwa haraka. Kila eneo lenye uzalishaji wa vito lijengwe eneo la kucharanga vito na kuuza vito na mikufu, pete na vitu vya thamani. Vijana wetu wapewe mafunzo nje na ndani ya nchi kwenye usonara, design na wasaidiwe kupata vifaa na mitaji ya kujiendeleza kiajira na kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la migogoro ya maeneo ya wachimbaji wa tanzanite wadogo na wawekezaji wakubwa lifanyiwe kazi ili lisije umiza wawekezaji wadogo. Iko haja ya Wizara kuwa na kanzi data ya kila aina za madini na vito na kiasi kilichopo na thamani yake ili ituwezeshe kujua utajiri tulionao kama nchi na jinsi ya kuhakikisha kuwa inasaidia maendeleo ya kiuchumi ya Watanzania kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada kubwa za Serikali kusaidia wachimbaji wadogo, bado liko tatizo kubwa la watoto wanaofanya kazi kwenye migodi na ambao wanatumia zebaki kuchambua dhahabu na hii ni sumu ambayo wanaishika na inapochomwa pia inaingia kwenye mazingira. Watoto hawa vilevile huingia kwenye mashimo ya migodi iliyochimbwa kienyeji bila kinga zozote na hutumia kamba tu kuingia ndani ya mgodi na hii ni hatari sana kwa maisha yao. Licha ya kuwa wanakosa elimu, vilevile watoto wako kwenye kuvunja kokoto na kwenye vito Mererani. Wizara ishirikiane na Wizara ya Ajira, Mazingira, Elimu, Ustawi wa Jamii kuwaondoa watoto migodini.