Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kuishauri Wizara kuzingatia ushauri wote uliotolewa na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini kwani pamoja na kuwa nchi yetu kuwa ya nne (4) Barani Afrika kwa kuwa na aina nyingi za madini, lakini sekta hii haijapewa msukumo wa kutosha ili kuleta tija inayokusudiwa. Bado mchango wa sekta ya madini kwenye Pato la Taifa haulingani na uhalisia. Hivyo basi, Serikali ikafanye uwekezaji wa kutosha katika sekta ya madini ikishirikisha wawekezaji wenye mitaji ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, machimbo ya Kitowelo kwenye Kata ya Lilombe ni ya muda mrefu sana lakini hadi leo Halmashauri haijanufaika na chochote. Hii ni kwa sababu soko la madini hayo liko Tunduru Mkoani Ruvuma, hivyo wachimbaji huenda Tunduru bila kupitia kwenye kata au kijiji, hivyo kijiji kukosa mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo kuna kampuni ya utafutaji wa madini, kampuni ya GWENA, kampuni hii mkataba wake haujulikani wala haina ushirikiano na vijiji uchimbaji huo unakofanyika kwani elimu ni ndogo sana kwa jamii hivyo kushindwa kusimamia vyema utafutaji huu wa madini. Hivyo Wizara sasa ione umuhimu wa kuwa na Afisa Madini kila halmashauri kwani hapa nchini hakuna halmashauri ambayo haifanyi biashara ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa madini aina ya green garnet katika Wilaya ya Ruangwa na Liwale. Serikali haijafanya utangazaji wa kutosha ili kupata wawekezaji katika uchimbaji wa green garnet, hivyo kukosa tija iliyokusudia. Hata hivyo, naishauri Serikali kuangalia upya leseni za utafutaji wa madini kwani wapo wenye hizi leseni wanazitumia kufanya uchimbaji wa madini na si utafutaji au utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado Serikali haijawekeza vya kutosha kwa wachimbaji wadogo wadogo. Sekta hii imeshindwa kuongeza ajira nchini kwa kuwa wachimbaji wadogo wadogo hawajapewa mitaji ili kupata vifaa na kuboresha mazingira ya kazi zao. Sheria vilevile ikaangaliwe ili kuwe na uwanja sawa kati ya wachimbaji wakubwa na wadogo kwani sasa wachimbaji wananyanyasika sana katika tasnia hii ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Sheria ya Madini ikaangaliwe ili kufanya madini yanayotumika katika ujenzi wa barabara ikiwezekana tozo hizi na ushuru mbalimbali zikafutwa ili kupunguza gharama za ujenzi wa barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba kupatiwa majina ya wachimbaji na watafutaji wa madini walioko katika Wilaya ya Liwale. Kwani hadi sasa shughuli hiyo hufanywa holela, hata Mkurugenzi wa Halmashauri hana hiyo takwimu, hivyo hata yeye hajui chochote. Jambo hili haliwezi kuwa sawa kwa kuwa kazi hizi zimekuwa zikifanywa kwenye eneo lake la utawala. Bila kusahau status ya Kampuni ya GWENA na machimbo ya Kitowelo.