Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala zima la makinikia. Mheshimiwa Biteko alikuwa Mwenyekiti na taarifa yake ilikuwa very hot na baada ya taarifa ile matumaini ya Watanzania kupata mafanikio makubwa na pesa nyingi yalikuwa makubwa, lakini mpaka sasa tunavyozungumza hatujui yale matumaini na zile taratibu zimepotelea wapi. Tulitumainishwa kwamba tungepata nyingine lakini mpaka sasa naona mambo yako kimya. Mtakapokuja kuhitimisha Mheshimiwa Waziri tunaomba muwafafanulie Watanzania habari za makinikia na hatima yake imefikia wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la elimu ya madini kwa Waheshimiwa Wabunge. Elimu hii ya madini kwa Waheshimiwa Wabunge haitoshi na siyo Wabunge wote tunatoka katika kanda za madini, wale ambao wanatoka katika Kanda za Madini wana uelewa zaidi kuliko ambao hatutoki katika kanda za madini. Wakati mwingine scope yetu ya kutoa michango inabanwa kutokana na hilo. Kwa hiyo, niombe Waziri basi atutengenezee mazingira tupate semina tuwe na uelewa zaidi katika madini ili basi tuwe tunaweza kuchangia vizuri katika sekta hii ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye vitabu vya Wizara tumeelekezwa aina za madini zinazopatikana katika maeneo tofauti tofauti. Naomba nishauri utafiti ufanyike zaidi kwa sababu naamini Tanzania ni tajiri kwa madini na madini yanaweza yakapatikana sehemu yoyote. Kwa hiyo, kama utafiti utafanyika zaidi basi upo uwezekano wa kuweza kugundua madini katika sehemu tofauti tofauti hata kule kwangu Kilwa.

Mheshmiwa Naibu Spika, Kilwa kwetu tukizungumza madini tunazungumzia gypsum, chumvi na gesi, niseme kuhusiana na gypsum. Gypsum inachimbwa Kilwa kwa ajili ya material ya viwanda vya cement lakini kuna changamoto kubwa ambayo ni gharama ya uzalishaji na bei ya soko ya gypsum. Gharama ya uchimbaji wa tani moja ya gypsum ni Sh.27,000, bei ya gypsum kwa viwanda vya cement vya Dar es Salaam ni kati ya Sh.80,000 au Sh.90,000 ukichanganya na gharama nyingine za usafirishaji na ushuru wa Serikali na kodi maana yake hawa wafanyabiashara wa gypsum wanafanya shughuli zao katika mazingira magumu. Tunaomba sana Serikali ije na bei elekezi ya gypsum ili basi wajasiriamali wetu waweze kufanya kazi ambayo inaweza ikawaletea tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitaja madini basi akili zetu moja kwa moja zinatuelekeza kwenye jambo ambalo lina pesa nyingi lakini mchango wa madini katika bajeti ya Serikali ni finyu sana. Nitoe ushauri kwa Serikali bado ipo haja ya kuwekeza ili basi tuweze kuyatumia midini yetu ipasavyo na yatoe mchango mkubwa kwa bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la madini ya gesi. Madini haya gesi ambayo kwa sisi watu wa Kilwa kwa mara ya kwanza gesi ilipatikana katika Kisiwa cha Songosongo mpaka sasa kuna changamoto kubwa katika madini ya gesi, watu wa Kilwa hatujafaidika nayo moja kwa moja, imefikia hatua hata wale ambao walitakiwa walipwe fidia kutokana na kupisha mradi ule wa bomba la gesi mpaka sasa hawajapata fidia zao. Nichukue nafasi hii kuishauri Serikali iwaangalie wadau wengine ambao walitakiwa wapate tija kutokana na madini haya ya gesi ili basi nao waweze kufaidi matunda hayo ya gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Serikali iwe wazi kuhusiana na madini ya gesi, ni aina gani ya gesi tuliyoipata. Gesi tuliyoipata ndiyo hii tunayotumia kupikia majumbani maana wananchi wakiona gesi hizi zinazouzwa wanafikiri ndiyo gesi ambayo tumeipata kutoka kule Songosongo. Tuwe wazi ni gesi hii au ni gesi tofauti, wananchi wafahamishwe maana kuna sitomfahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaambiwa uwezekano wa kupata mafuta upo, je, katika machimbo hayo ya gesi yaliyofanyika kuna dalili ya kupata mafuta? Serikali itueleze ni wapi tunaweza tukapata mafuta maana tumetumia gharama kubwa kuchimba gesi kama tulikuwa na tumaini la kupata mafuta Serikali iko kimya haijatueleza chochote kama tutakuja kupata mafuta au lah, maana tunaelezwa gesi na mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la madini ya chumvi. Sisi tunazalisha chumvi lakini gharama za uzalishaji wa chumvi na tozo zilizowekwa katika uzalishaji wa chumvi ni nyingi sana wajasiriamali wetu ambao wanajishughulisha na shughuli ile hawapati faida. Kwa hiyo, niombe Serikali ipunguze hizo tozo ili basi hawa wajasiriamali wetu waweze kupata faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.