Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi nichangie hoja hii iliyokuwa mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza na mimi niwapongeze sana Wizara ya Ardhi, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii. Pamoja na changamoto kubwa ya migogoro mingi iliyokuwepo kabla lakini kwa kasi wanayoenda nayo tunaimani siku moja itakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme mimi ni mmoja wa Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii, lakini ushirikiano tulioupata kutoka kwenye Wizara hii katika majukumu yetu ni mkubwa sana. Tulikuwa na ziara na Kamati ya Ardhi kukagua mipaka ya nchi, lakini huwezi kuamini tulipewa ushirikiano na Naibu Waziri, Katibu Mkuu siku zote tulivyokuwa kwenye safari wote tulikuwa nao mguu kwa mguu mpaka tumerudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulipokwenda Dar es Salaam siku tatu siku zote Waziri mwenyewe Lukuvi tukawa naye siku tatu, ni tofauti kabisa na wakati mwingine kwa watu wengine ambao wanasema wako busy. Tunashukuru sana waendelee na moyo huo ili kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nina machache leo na zaidi ni ushauri. La kwanza, dhuluma ya wamiliki ardhi hasa wanyonge hususani Manispaa ya Morogoro. Mheshimiwa Waziri ni mchapakazi na aliwahi kufika Morogoro kwa ajili ya kutatua migogoro hii ya ardhi. Hata hivyo, nataka nitoe mfano mmoja kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya tatizo la njaa mwaka 1974, Mwalimu Nyerere alitaka tuwe na kilimo cha kufa na kupona na akasema kila Mkuu wa Mkoa asimamie suala la uzalishaji wa chakula, anayezembea basi kazi hana. Basi ilitokea siku moja akaenda Mkoa mmoja akakuta kwa sababu mtu anataka asipoteze kazi wakatafuta wafungwa Magerezani, wakatafuta shamba likalimwa, wakachukua mahindi ya wakulima wakayapanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyapanda ili kuonesha kwamba chakula hali safi akapelekwa pale Mwalimu. Sasa kwa sababu Mwalimu uzuri alikuwa anatafuta taarifa mbalimbali, kufika pale akanyofoa tu mhindi mmoja akaona ni feki na yule Mkuu wa Mkoa akapunguzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi, Mheshimiwa Waziri aliwahi kuja Morogoro Manispaa kutatua tatizo la ardhi na kusikiliza changamoto za dhulma ya ardhi Mkoa wa Morogoro hususani Manispaa; lakini alichofanyiwa hakijui na sasa leo nataka nimwambie. Watu wa Morogoro hasa wamiliki wa ardhi wanyonge walichonganishwa na Serikali yao, lakini sasa wamepata ukweli wanamwomba sana arudi tena akawasikilize ili atatute changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ile Mheshimiwa Waziri alipokuja Morogoro watu wenye migogoro ya ardhi wakakusanywa Ukumbi mwingine, halafu akapelekwa kwenda kuongea na watumishi. Watu walikasirika sana na hili jambo halipendezi, wanaleta chuki kugombanisha Serikali ya Awamu ya Tano na wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Morogoro Manispaa kuna dhuluma kubwa sana ya ardhi, kazi yote wanayofanya Mawaziri inaharibiwa na watendaji wao kule chini. Kule chini wakigawa ardhi wanajigawia wao halafu wanauza kwa watu wengine. Pia hata ile ardhi wanayogawiwa wanyonge, wale Maafisa Ardhi wanaowaleta na Wataalam wa Ardhi hawako kwa ajili ya kusaidia matatizo ya watu, badala yake ni kila siku kupora ardhi ya wanyonge na kuwauzia wenye pesa na wakija viongozi wakitaka kusema matatizo yao wanaminywa, wanakanyagwa kwenye Mikutano na Mabango yote yanachanwachanwa ili wasijue matatizo yanayowakabili Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aje, kuna mchezo mchafu mpaka wanachoma mafaili ya wamiliki halali wa ardhi wanatengeneza hati mpya na mafaili mapya. Mheshimiwa Waziri anione nimpe ushahidi mimi mwenyewe mwathirika, marehemu baba yangu mwathirika, dada yangu mwathirika, majirani zangu waathirika, watu wa Morogoro waathirika. Nitampa hivyo viwanja vyote ambavyo na watu wengine wenye matatizo kama ya kwangu na jamii ya Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kuhusu fidia ndogo wanayolipwa watu kupisha miradi ya maendeleo hususani vijijini. Kwanza tunashukuru sana Serikali inavyotuletea miradi mingi kwa ajili ya maendeleo hususani huu mradi wa reli inayoenda kasi. Wananchi wetu hasa Mikese Station, Ngerengere na Kidugalo ni miongoni mwa waliotoa ardhi yao kwa ajili ya kupisha miradi hiyo. Hata hivyo, fidia waliyolipwa ni flat rate 500,000 kwa heka, kitu ambacho ni tofauti na bei ya soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajiuliza; Serikali hii hii taasisi zake kama NSSF au ukikuta National Housing wakitaka kujenga nyumba kwenda kununua ardhi wananunua kwa bei ya soko na hiyo bei ambayo haipo popote pale. Natoa mfano tu, mradi kule wa Dege Beach ilinunua heka moja zaidi ya milioni 800, kwa kusema land for equity hata National Housing hivyo hivyo, matokeo yake zile nyumba zinakuwa na gharama kubwa na wanakuja kuumizwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wananchi wanajiuliza mbona Serikali hii ikitaka kujenga mjini au sehemu yoyote wananunua bei ya soko, lakini wakija kuchukua ardhi yetu huku vijijini wanasema tunalipa bei ya Serikali. Huku wanatuumiza wanalipa mapato madogo kitu ambacho leo hii aliyelipwa 500,000 pale kupisha miradi hii hawezi kupata ardhi kama ile ile pale hata nusu ya pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, leo bei ya ardhi pale Mikese ni zaidi ya shilingi milioni nane kwa heka. Natoa mfano, Kampuni ya Mahashree ambayo imewekeza pale Kiwanda cha Mbaazi ilinunua mwaka jana heka moja milioni nane, lakini yenyewe imekuja kulipwa 500,000 kwa heka na Serikali ardhi ile ile, ndani ya mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sasa tuwe kama msumeno. Kama bei inayotumika ni 500,000 kote hata huku kwenye taasisi za umma kama NSSF na National Housing inapotaka kujenga miradi ya maendeleo bei iwe hiyo hiyo ili nyumba hizi ziwe bei nafuu wananchi hawa wapate uwezo wa kuzimiliki hizo nyumba tofauti na sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bei kubwa ya kodi za ardhi, hili ni janga lingine, kwa sababu Mheshimiwa Waziri yeye mwenyewe ni shahidi, tumekwenda wote Kilungule amepima ardhi bure, lakini watu kwenda kulipia mpaka leo wameshindwa. Hili kama halitaangaliwa vizuri, basi tunakwenda katika njia nyingine ya kumilikisha ardhi kutoka kwa wanyonge kwenda kwa matajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipotahadhari ardhi hii itamilikiwa na wachache Tanzania kwa kisingizio cha Watanzania wengine kushindwa kulipa ardhi kwa sababu kama wanavyosema mtu akishindwa kulipa kodi watampeleka Mahakamani, watamnyang’anya ardhi na kweli watawanyang’anya wengi, lakini ndilo lengo la Serikali? Maana yake ni nini, ni kwamba ardhi hii tunaipokonya sasa kwa wanyonge walio wengi tunapeleka kwa matajiri wachache wenye uwezo wa kulipia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri na bora Mheshimiwa Waziri akaweka bei inayoweza kulipwa na wengi ili watu wote walipe kuliko wakiweka bei kubwa watalipa wachache wengine hawataweza kumilikishwa ardhi, kitu ambacho itakuwa ni hatari sana huko mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Umiliki wa Ardhi Vijijini. Nnafahamu kwenye nyaraka zinaonekena ardhi kubwa inamilikiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.