Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara ya Ardhi. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na nguvu mpaka kuweza kuchangia katika Hotuba hii ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Lukuvi na timu yake kwa ujumla, pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa mama Angelina Mabula kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Waziri na timu yake wanafanya kazi kubwa sana, na-declare interest kwamba mimi nipo kwenye Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Tulitembelea juzi miradi ya NHC pale Dar es Salaam, tuliona mambo makubwa sana. Wakati huku ndani watu walikuwa wanasema kwamba Mradi wa NHC, Mradi wa nyumba unakufa, lakini mradi upo vizuri. Nikupongeze Waziri endelea na kasi hiyo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona mfumo wa upimaji ardhi mpya ambao unaitwa ILMIS, mfumo ule ni mzuri, naamini kabisa utaondoa ile zana ya kudhulumiwa hati au wale wajanja wajanja sasa wanaotaka kuuza viwanja vya watu itakuwa sasa haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niendelee kuchangia sasa katika suala la upimaji ardhi. Lushoto ni eneo ambao lina wakazi wengi sana, wanahitaji kupimiwa ardhi na wanahitaji hati. Hata hivyo upatikanaji wa hati katika Halmashauri ya Lushoto, tuseme Wilaya kwa ujumla ni mgumu sana. Nimwombe Waziri sasa, pamoja na kwamba ana mpango mzuri wa kupeleka vifaa vya kisasa kupima maeneo ya Lushoto, basi nimwombe aharakishe ili wananchi wa Lushoto waweze kupata hati zile. Maana kupata hati Lushoto ni sawasawa na kuokota dhahabu chini ya mchanga, ni ngumu sana, lakini kwa mfumo huu Waziri anaokuja nao naamini kabisa sasa mambo yatakuwa ni mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nimwombe sasa Waziri katika mfumo huu wa ILMIS usiishie Dar es Salaam tu, hebu uende kwa Kanda, wagawe Kanda ndani ya Tanzania hii ili uweze kwenda kwa kasi kwani mfumo huu ni mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala la hati. Nilienda Dar es Salaam kwenye mtaa mmoja wanaita Kilungule A na B. Tulikuta wananchi wa Kilungule A walioomba hati ni 600, lakini ambao wameenda kuchukua hati ni 176, kumuuliza Waziri akasema hati zote 600 zipo. Baada ya kuwauliza wananchi wale wakasema kwamba hawana pesa za kulipia gharama ya hati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri hizi gharama za kulipia hati hebu ziangaliwe upya maana ni gharama kubwa, wananchi wale wanasema kwamba kupimiwa ni Sh.300,000 wakajumuisha pamoja na hati kwamba gharama yote ni Sh.300,000, matokeo yake kufika kule katika kuchukua hati wanaambiwa kuwa, kuna gharama za hati na kuna gharama za upimaji. Kwa hiyo hili niiombe sasa Serikali iangalie upya ili ipunguze wananchi wale waweze kupata hati kwa bei rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye Mabaraza ya Ardhi. Kule Lushoto namshukuru Waziri Lukuvi alituwekea Baraza la Ardhi, lakini Baraza la Ardhi lile mpaka sasa hivi halina Mwenyekiti, Mwenyekiti anatoka Korogwe. Kwa hiyo nimwombe sasa Mheshimiwa Waziri apeleke Mwenyekiti katika Baraza lile la Ardhi kwani kuna msongamano mkubwa sana katika Baraza la Ardhi la Lushoto na wananchi wengi wanatoka maeneo mbalimbali na maeneo ambayo kwa kweli wanafika pale huenda kwa siku moja au siku mbili. Kwa hiyo nimwombe sasa Waziri anisaidie kupeleka Mwenyekiti katika Baraza lile la Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mipaka. Sisi na Kamati yetu tulienda maeneo ya Mtukula kule mpakani mwa Uganda na Tanzania; tuliona vile vigingi vya mkoloni ni vizuri kuliko vigingi vinavyowekwa na Serikali. Kwa hiyo ningeomba Serikali yangu sasa itumie modal ile ya vigingi vile vya mkoloni. Kwanza vigingi vile viimarishwe then viwekwe vya kutosha katika maeneo yote ya mpakani katika mipaka yetu yote ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna mipaka kwenye maziwa; mipaka yetu kwenye maziwa haijulikani, kwa hiyo niiombe Serikali yangu iweke maboya yale sasa kwenye maziwa ili wananchi wetu wanapoenda kuvua katika maziwa yale wasiingie katika maeneo ya watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.