Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunipa fursa kutumika katika Serikali yake, Serikali ambayo imefufua matumaini ya Watanzania walio wengi. Vile vile nitumie fursa hii kumshukuru sana Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa ushirikiano mkubwa anaonipa katika majukumu yangu ya kila siku. (Makofi)
Nimejifunza mengi sana kutoka kwake, ni mtu ambaye anatoa ushirikiano.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Kwa hiyo, namshukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nitumie fursa hii kuwashukuru Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa ushirikiano wanaonipa katika majukumu yangu ya kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutumia fursa hii kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge na lazima niseme kwamba nimefarijika sana kwa namna Waheshimiwa Wabunge mlivyoonesha hamasa kubwa katika kuchangia Wizara ambayo ndiyo inabeba maslahi ya Watanzania walio wengi. Wote mmetoa michango ambayo itatusaidia katika kutekeleza majukumu yetu ya kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda haitawezekana kujibu hoja zote, mengine yatajibiwa na Mheshimiwa Waziri, lakini mengine tutayaleta baadaye kwa maandishi kabla ya Bunge hili kwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein kwamba Serikali haina vision ya kilimo. Naomba tu nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kati ya eneo ambalo nafikiri tuko mbele sana ni kuhusu visioning, sera, mipango na mikakati. Wizara yetu katika sekta zake zote zina sera ambazo zinaainisha kwa kirefu sana kuhusu dira katika maeneo tofauti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Sera ya Mifugo ya mwaka 2006, Sera ya Maendeleo ya Ushirika ya mwaka 2002, Sera ya Uvuvi ya Taifa ya mwaka 1997. Zote hizi zinachangia katika kufikia malengo na sera na dira ambayo imeainishwa katika Sera ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2025, katika maana ya kwamba development mission 2025. Zote hizi kwa pamoja zinaeleza kwamba dira yetu katika kilimo ni kuwa na kilimo cha kisasa, cha kibiashara na chenye tija na faida ambacho kinatumia rasilimali kwa ufanisi na endelevu na kuwa kiungo muhimu na sekta nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze tu kwa ufupi kwamba kuhusu vision na sera, hili ni eneo ambalo tuko mbali sana. Kuna changamoto katika utekelezaji, lakini siyo kwenye eneo la sera.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa vilevile niangalie eneo ambalo limechangiwa kwa hamasa kubwa na kwa msisimko mkubwa na Waheshimiwa Wabunge walio wengi. Hili ni eneo la migogoro kati ya watumiaji mbalimbali wa ardhi hususan kati ya wafugaji na wakulima. Hili ni eneo ambalo kama Wizara tunatoa kipaumbele kwa sababu ya namna inavyoleta changamoto katika kuendeleza kilimo; ni eneo ambalo linatishia amani ya nchi yetu. Kwa hiyo, Wizara imeweka kipaumbele katika shughuli zake za kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na wakulima ina vyanzo vingi, lakini chanzo kikubwa ni ukosefu wa ardhi, lakini vile vile inasababishwa na kukosekana kwa huduma kwenye maeneo ya wafugaji, inasababishwa vilevile na wafugaji mara nyingine kukimbia magonjwa kwenye maeneo yao na kwenda maeneo ambayo magonjwa siyo mengi. Vile vile inatokana na kukosekana kwa baadhi ya huduma kama maji na kama mlivyosema Waheshimiwa Wabunge wanalazimika kufuata maji maeneo ambayo yana maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ni lazima tukubali kwamba kwenye baadhi ya maeneo wafugaji wanahama kwa sababu ya ongezeko la watu, lakini vile vile kwenye baadhi ya maeneo wanahama kwa sababu ya mabadiliko ya tabia ya nchi. Kimsingi tunasema kwamba kuna tatizo, tunakiri kwamba ni tatizo ambalo ni lazima tulishughulikie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni namna gani Serikali kupitia Wizara yetu imejipanga kutatua tatizo sugu la migogoro ya ardhi? Mkakati wa kwanza ni namna ya kupata ardhi. Tunapanga kutafuta ardhi ambayo itatosheleza mahitaji ya wafugaji kwa kufanya masuala yafuatayo:-
Moja, kulinda ardhi ya wafugaji kwa kuitangaza kwenye Gazeti la Serikali. Vile vile kufanya mkakati wa zoning katika maana ya kwamba kutafuta na kutenga ardhi katika baadhi ya mikoa ambayo ina ardhi kubwa na kuyasajili ili itumike kwa ajili ya wafugaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vile vile kwa muda mfupi uliobakia kuchangia kuhusu uvuvi haramu na hili nasema kwa ujumla wake kwa sababu mmechangia sana. Waheshimiwa Wabunge, tunaomba mtuunge mkono katika jitihada zetu za kupambana na uvuvi haramu. Ukiruhusu uvuvi haramu uendelee, hautakuwa unampenda mvuvi wako kwa sababu rasilimali za uvuvi zitakwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari kuna matatizo makubwa kwenye baadhi ya maeneo, samaki wanakwisha. Kama mnavyofahamu Ziwa Victoria, tayari kuna crisis na Ziwa Rukwa; yote ni kwa sababu ya uvuvi haramu. Kwenye baadhi ya maeneo ya maji ya chumvi, baadhi ya species za samaki, mfano kamba mti (prawns) zimekwisha kwa sababu ya uvuvi haramu. Naomba mtuunge mkono! Hatuwezi kumpenda mvuvi kwa kuendelea kumruhusu aendelee na uvuvi haramu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tufahamu wazi kwamba uvuvi haramu kwa kutumia njia ambazo haziruhusiwi na sheria ni mbaya na huwezi kuruhusu kwa sababu tu unataka kumlinda mvuvi. Kwa hiyo, tunawaombeni Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono katika hili, Serikali ina nia ya dhati ya kuendelea kutoa elimu. Wavuvi wengi kabla ya kupewa Leseni ya Uvuvi, wanapewa elimu kuhusu uvuvi ambao unaruhusiwa na sheria. Kwa hiyo, mara nyingine inakuwa ni suala la kawaida tu la kutokufuata sheria na wala siyo suala la kutofahamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo kuhusiana na suala ambalo limeibuliwa sana na Mheshimiwa Dau kuhusiana na uvuvi kwa kutumia mitungi ya gesi. Uvuvi wa kutumia mitungi ya gesi unaruhusiwa kwenye aina fulani fulani za uvuvi hususan uvuvi wa samaki wa mapambo. Mara nyingine mitungi ile hutumika kufanya uvuvi wa majongoo; atakuwa anafahamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, uvuvi ule unaharibu matumbatu; kwa hiyo, unaharibu mazalia ya samaki. Kwa hiyo, tunaendelea kusisitiza kwamba leseni zitolewe, badala ya kusema kwamba turuhusu tu kila mtu atumie uvuvi wa aina ya gesi ambao unaharibu mazingira. Serikali nia yake ni ya dhati katika hili, kwa hiyo, tunaomba mtuunge mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi wametoa hoja ya msingi sana kuhusu kodi au leseni zinazotolewa kwa wavuvi katika Ziwa Victoria ambao wanalazimika kupata leseni kwenye Halmashauri mbalimbali ambapo wanakwenda kuvua, suala tunaloliita migratory licences au migratory taxes.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge kwamba nia ya Serikali katika hili ni jema. Tukiruhusu kwamba mvuvi akipata leseni katika Halmashauri moja, basi anaruhusiwa kwenda kote; moja, tutanyima Halmashauri zetu mapato, lakini vile vile ni vigumu kuzuia uvuvi haramu pamoja na uhalifu ambao wengi wenu mmeulalamikia sana. Kwa hiyo, tunatumia utaratibu ule wa leseni kutolewa katika kila Halmashauri kama namna ya sisi kuratibu uvuvi unaofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge kwamba, siyo kwamba maji hayana mipaka. Maji ya Ziwa Victoria; kila Halmashauri inafahamu maji yake yanaishia wapi, kuna alama. Kwa hiyo, nawaombeni mfahamu kwamba ni kwa nia njema na hata hivyo leseni ya uvuvi ni shilingi 15,000/=. Kwa ambao hawafahamu...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba umalize.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Kwa ambao hawafahamu, ndiyo bei ya samaki mmoja. Kwa hiyo, naomba mtuunge mkono kwa sababu tunafanya kwa nia njema.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.