Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. KATANI A. KATANI. Mheshimiwa Spika, nikushukuru na niombe tu kwa namna unavyoendesha mjadala kwa siku ya leo ingewezekana ungekalia kiti siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo la maji linalozungumzwa ni tatizo la kitaifa, na kaka yangu Mheshimiwa Chikota wakati anachangia amejaribu kuzungumzia Mradi wa Maji wa Makonde, mradi ambao uliasisiwa mwaka 1953 katika Wilaya ya Newala, mwaka 1953 ilikuwa bado haijawa Wilaya maana Wilaya ya Newala imepatikana mwaka 1954 Mzee unajua. Mradi huu wakati unasisiwa ulikuwa unahudumia wakazi 82,000 tu; leo tunapozungumza Newala kuna watu zaidi ya 205,000, Tandahimba kuna watu zaidi ya 227,000. Nanyamaba ambako mradi unatakiwa uende kunazaidi ya watu zaidi ya 60,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ukiangalia mradi huu kwa sasa, unahudumia watu zaidi ya laki saba. Hata hivyo mradi huu ukiuangalia kwenye bajeti, kuanzia mwaka 2016/17, 2017/2018 na mbaya zaidi tarehe 10 Septemba, 2016, mimi nilikuwa na Makamu wa Rais Tandahimba pale, amewaambia watu wa Mtwara kwa maana ya Newala, Tandahimba na Nanyamba kwamba Serikali imetenga shilingi bilioni 170 kwa ajili ya Mradi wa Maji wa Makonde.

Mheshimwa Spika, mpaka leo hii tunapozungumza ukiangalia kwenye makabrasha fedha iliyotengwa mwaka huu 2018/2019 ni shilingi bilioni moja. Sasa kuna majibu gani kwa wapiga kura wale wa maeneo ya Mtwara? Kuna maelezo gani ambayo yatawafanya watu wale waiamini Serikali ya CCM? Na tatizo la maji ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili, nimewahi kumwandikia barua, message zaidi ya tatu au nne Mheshimiwa Waziri, lakini mara ya mwisho hata Naibu Waziri nimewahi kumwambia, kwangu Tandhimba kuna Mradi wa Maji ya Mkwiti ambo unatekelezwa kwenye lot nne; lot ya kwanza mwaka 2016/2017 mkandarasi ameshasaini mkataba na tayari ameshapeleka bomba zenye thamani zaidi ya shilingi bilioni 1.4, advance payment hajapata, ameandika certificate ya pili ya kuomba shilingi bilioni 1.1 hajapata, Mheshimiwa Spika, tunaingia kwenye bajeti nyengine wakati mkandarasi ameshapeleka vifaa tayari lakini yeye hajalipwa hata advance payment na ukiusoma mkataba baina ya Mkandarasi na Halmashauri, advance payment inapaswa ndani ya siku 28, leo tunaozungumza toka mwezi Februari fedha hii haijatoka.

Mheshimiwa Spika, sasa sijui Waziri wa Fedha, maana niliuliza watu wa Wizara ya Maji wanasema taratibu zote zishakwenda Wizara ya Fedha, sasa sijui Wizara ya Fedha inauwezo ya kupata fedha ya kujenga viwanja vya ndege bila ya kutoka kwenye bajeti, ya kununua ndege bila ya kuwepo kwenye bajeti lakini hawana uwezo wa kulipwa fedha ya maji ambayo ipo kwenye bajeti, sijui. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hii sijui watu tunawaonea aibu Wizara ya Fedha, lakini kuna mambo mengi wanakwamisha ambayo hayana msingi kabisa. Wana uwezo wa kutafuta fedha za maneuver kwa kutengeneza vitu ambavyo haviko kwenye bajeti vya kwenye bajeti hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona mwaka jana Wizara ya Maji asilimia 22 tu ya fedha za maendeleo ndizo zimeenda; lakini ipo miradi zilitengwa pesa shilingi bilioni 35 zilmelipwa pesa zaidi ya shilingi bilioni 42. Kumbe mijitu hii ina pesa za kutosha kwa nini kwenye miradi ya maendeleo kama ya maji ambayo ndio uhai wa Mtanzania zisiende fedha hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana, dada yangu Ashatu Mheshimiwa Waziri sijui ametukimbia hapa, alitakiwa hapa alitakiwa awepo mwenyewe, kwa sababu yeye ndio mshauri wa mambo ya fedha kwa Rais na kwa Baraza la Mawaziri. Atuambie kama mna fedha za kufanya mambo mengine, lakini hamna fedha za kutatua tatizo la maji ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mtu alikuwa anachangia kwa kujipendekeza, mimi sijui kama Wabunge tuko Serious na Taifa letu, mtu anazungumza suala la bomba la maji mita 400? Mheshimiwa Waziri umefika Tandahimba, ukitoka Mkwiti kwenda Tandahimba kilometa 61 niambie wapi uliliona bomba? Halafu uniambie mita 400?

Mheshimiwa Spika, kilometa 61 mpaka unafika Wilayani hakuna bomba, anakuja mtu wa CCM anasema maji mita 400; mita 1000 hakuna bomba utazungumza mita 400? Tuwaonee huruma akina mama hawa, tuwaonee huruma Watanzania hawa kila anayesimama anazungumza wazi kabisa kwamba bila ya maji hakuna kinachoweza kuendelea, hivyo viwanda tunayoyasema kama bila ya maji hakuna viwanda, hili Bunge tunalolisema kama hatukuoga maji hatuwezi kuingia Bungeni, mbuzi tunaofunga, ng’ombe tunaofuga kama hawakunywa maji watakufa tu.

Mheshimiwa Spika, niombe sana nyie watu wa fedha mnakwamisha mambo mengi sana. Huyu mkandrasi wa kwangu sasa tunataingia mwaka 2018/2019 fedha ya mwaka 2017/2018 hajapata mpaka leo. Sasa hatimaye tutamlalamikia nani? kama fedha hajapewa na amepeleka bomba za shilingi bilioni 1.4 ziko site. Maana si wakandarasi wababaishaji yeye bomba ameshapeleka site, advance payment hajapata, hizo fedha za certificate ya shilingi bilioni 1.1 hajapewa. Kwa hiyo tatizo liko kwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Spika, Sasa kwa sababu jambo la maji umeliona ni jambo la msingi sana, moja mimi siwezi kuunga mkono hoja ya bajeti ya Wizara hii na ninaamini Wabunge wote kwenye shughuri pevu itatokea kwenye Wizara ya Maji, mimi ninaamini hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo miradi ambayo nataka Mheshimiwa Waziri ikiwezekana mtusaidie, ipo miradi mnapeleka fedha mnakwenda kuzindua, mfano Mahuta pale, tulienda na Mheshimiwa Selemani Jafo akiwa Naibu Waziri, akaenda kuzindua Mradi wa Maji wa Mkupete ambao fedha zake zimeshalipwa. Ule mradi umezinduliwa mwaka 2016 mpaka leo tone la maji hakuna na mradi umezinduliwa, hizi fedha mnazopeleka mnapeleka kwa ajili gani? Kama mradi umekamilika na umezinduliwa na maji hakuna huu mradi unakwenda kwa nini?

Mheshimiwa Spika, hebu mtuambie miradi inaenda kwa nini? Mnasema imekalimika lakini maji watu hawapati huduma nini maana ya kukamilika? Tuambieni maana ya kukamilka kwa mradi, umeleta mradi unasema mradi umekamilika. Mradi huo hauna tofauti ukienda Mahea kuna mradi mwengine, kuna miradi wa Mahuta mmepeleka zaidi ya shilingi milioni 86, lakini miradi hii yote imekamilika lakini watu hawapati maji.

Sasa mtuambie mnaposema mradi umekamilika maana yake ni kukamilika tu kuona aidha mmejenga mabomba mmeweka mabwawa au kukamilika Watanzania wapate amaji? Tunaomba sana mtupe ufafanuzi wa jambo hili kwa uzuri sana.

Mheshimiwa Spika, lakini bahati mbaya ukilisoma book lenu hili Mtwara tuna bahati mbaya sana. Katika mikoa ambayo bajeti ya maji ni ndogo, ni mkoa wa Mtwara. Tatizo la Mtwara ni nini? Miradi mnayotupa hewa, tunaozungumza wamakonde fedha hakuna, Kaka yangu Chikota amezungumzia mradi wa Ruvuma fedha mpaka sasa hakuna. Tuna tatizo gani watu wa Mtwara?

Mheshimiwa Spika, mimi nilidhani Mheshimiwa Rais alivyokuwa amezungumza watu wa Kusini, alijua kwamba Kusini tumeachwa nyuma kwa muda mrefu na tutapewa priority sasa kwa kuona kwamba vitu vya msingi vinavyokuja basi Kusini lazima tuwapelekee na wao waone wananufaika na matunda ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mnajua wakati anatoa taarifa Mheshimiwa wa Liwale amezungumza, zipo fedha za wakulima haohao wa korosho zaidi ya shilingi bilioni 250 na kitu zimekwenda kwenye matumizi yasiyoeleweka, lakini watu wake hawana maji. Watu wa Mtwara wanachangia pato
kubwa kwenye Taifa hili. Kwa miaka hii miwili/mitatu mfululizo ukiangalia trends ya Mtwara kutoka kwenye zao la Korosho hawakuwa watu wa kulilia maji leo, hata siku moja.

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana, tumekuwa na ngonjera, mimi tangu nakua nimemkuta Mbunge wa kwanza ninayemjua, Mzee Nandonde, kila niliposikiliza hotuba yake alizungumzia suala ya maji, akaja Mzee Lutavi alizungumzia suala la maji, amekuja ndugu yangu Njwayo akazungumzia suala la maji, napita mimi nazungumzia suala la maji. (Makofi)

Mheshemiwa Spika, ebu nyie ndugu zetu wa CCM, mnisaidie jambo kubwa sana; kwenye mazingira yetu ya taifa letu kitu gani tutaweka kipaumbele kama si maji? Katika vitu vyote tulivyokuwa navyo maji nadhani ni jambo la msingi kuliko kitu kingine chochote. Kwa hiyo tuweke priority kwenye maji kwanza halafu tufanye mambo mengine; na tunauwezo kuamua tukasema kwamba mwaka huu baadhi ya bajeti fulani zisinde tuitekeleze bajeti ya maji…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)