Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu. Namshukuru Mwenyezi Mungu pia kwa kuniwezesha kusimama hapa jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba kuipokea hoja hii ya bajeti ya Wizara ya Maji na naiunga mkono na natoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa namna wanavyojituma katika shughuli za maji. Nitoe shukrani zangu za dhati kwa jinsi walivyounusuru Mradi wa Maji wa Bwawa la Mwanjoro kutoka Wilayani Meatu kwa sababu bwawa hili lilikuwa limetelekezwa toka mwaka 2012.

Mheshimiwa Spika, nikijielekeza upande wa hotuba, naomba kuongea kuhusu huduma ya maji vijijini. Katika kitabu cha hotuba ukurasa wa saba, Wizara imesema kwamba imejenga vituo vya kuchotea maji 123,000 na vituo 85,000 ndiyo vinavyofanya kazi tu. Kwa hiyo, ukiangalia pale ni vituo 38,000 ambavyo havifanyi kazi ambapo ni sawa na asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukienda zaidi Wizara imeona changamoto inayosababisha vituo visitoe maji ni usimamizi pamoja na uendeshaji wa miradi hii unaosababishwa na uendeshaji kwa kutumia dizeli. Naiomba Wizara iende zaidi kuangalia changamoto inayosababisha vituo visifanye kazi ikiwa ni pamoja na usanifu mbovu, usimamizi mbovu na utafiti mbaya. Kama Wizara itazichukua hizo sababu nyingine tatu kama changamoto, itaweza kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji kwa sababu tumeona usanifu umekuwa ukifanyika chini ya viwango, utafiti mwingi wa maji unafanyika wakati water table iko juu na kusababisha maji kupatikana wakati wa masika tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichangie kuhusu mradi wa maji wa kutoka Ziwa Victoria na kuyaleta katika Makao Makuu ya Wilaya ya Busega ambayo ni Nyashimo, Bariadi pamoja na Itilima. Utekelezaji wa mradi huu imekuwa ni muda mrefu sasa. Toka Septemba, 2016 Waziri wa Mazingira alitujulisha kwamba fedha tayari zimeshaletwa lakini mpaka leo usanifu unafanyika. Naomba usanifu uishe haraka ili mradi utekelezwe kwa sababu maji yanahitajika kwa ajili ya hiyo miji mipya ya kiutawala iweze kujengeka. Nyashimo ni Makao Makuu ya Wilaya ya Busega, Bariadi ni Makao Makuu ya Mkoa wa Simiyu na Itilima na Makao Makuu ya Wilaya ya Itilima yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maji haya pia ni muhimu kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na fedha hizi zililetwa kwa ajili ya kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi. Kwa namna unavyochelewa kutekelezwa maana ya makusudio ya kuletwa hii fedha itakuwa haipo.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee Mradi wa Maji wa Kitaifa wa Wilaya ya Maswa. Katika kitabu cha bajeti wamesema kwamba utekelezaji wa ujenzi wa mtambo na kuchujia na kutibu maji unaendelea kukamilika na kwamba mradi utakamilika Mei, 2018 ambao ni mwezi huu. Ukiangalia muda wa mkandarasi wa kufanya kazi umekwisha lakini kazi haijakamilika. Mtambo huu utatumika kuchuja, kusafisha na kutibu maji lakini ukiangalia bwawa lile halina maji, limejaa tope. Kwa hiyo, hapa mimi naishauri Serikali itenge fedha kwa ajili ya kutoa tope hilo ili kuweza kuongeza kina cha maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee mradi wa skimu ya umwagiliaji iliyopo Wilaya Meatu ambapo mimi ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani pia ni mjumbe wa Kamati ya Elimu, Afya na Maji. Ipo skimu ya umwagiliaji Kijiji cha Magwila na ilianza kutekelezwa 2012/2013 na ungekamilika 2013/2014 lakini mpaka leo mradi huu haujakamilika. Fedha iliyotumika ni shilingi 1,165,000,000 na kazi iliyofanyika ni kujenga chujio, kujenga mfereji wa kati wa mita 1,000 kati ya mita 7,000 pamoja na sehemu 12 za kusambazia maji. Shilingi bilioni 1 ikawa imetumika na imekwisha lakini mradi huo mpaka leo haujakamilika kwa ajili ya kunufaisha wananchi kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, mimi nataka Mheshimiwa Waziri aieleze jamii ya Meatu kwa nini mradi huu haujakamilika? Kwa sababu fedha ilikuwa ya Mfuko wa Maendeleo ya Benki ya Afrika na usimamizi ulikuwa unafanywa na DASIP Kanda ya Mwanza. Halmashauri ya Wilaya haikuhusika na chochote katika usimamizi wa kiufundi. Mshauri wa mradi ilikuwa ni kampuni kutoka Jijini Nairobi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kujua ni lini mradi huu utatekelezwa? Naishauri Serikali ikamilishe sehemu iliyobaki ya mita 6,000 ya mfereji wa kati pamoja na kujenga mfereji mkuu ili sasa ule mradi uweze kufanya kazi. Pia naomba mradi huu ufuatiliwe ili kuona kama thamani ya fedha ipo. Maana mradi huu ungekamilika ungeweza kusaidia kaya 123 za kijiji hicho kati ya kaya 650 na ungeweza kusaidia upatikanaji wa mbogamboga na mazao mengine kwa Wilaya nzima ya Meatu.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja.