Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, na mimi naomba nianze kwa kuipongeza Serikali yangu kwa jinsi ambavyo inaendelea kufanya kazi ya kutatua matatizo ya maji katika maeneo mengi. Pamoja na hilo pia nimewasikiliza wachangiaji wengi na wengi wao nimewasikiliza vizuri sana, naomba tu nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba kinacholalamikiwa kikubwa zaidi kama umewasikiliza wachangiaji wengi ni kitu ambacho kwa lugha ya kingereza tunaweza kusema ni poor project management ambayo mnayo katika Wizara yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani miradi ya maji kwa mfano nikizungumzia mradi wa maji wa Chalinze ambao sasa una miaka zaidi ya 15 kila siku tumekuwa tunazungumzia mradi huo wa maji, Mheshimiwa Waziri nina imani kwamba sasa baada ya kumaliza kupitisha bajeti hii unaweza ukaenda ukaliangalia vizuri hili. Nina imani pia kwamba kuna vijana wazuri wa Kitanzania ambao wamesomea project management ambao tukiwapa kazi ya kusimamia project hizi wanaweza wakatufanyia kazi iliyo nzuri zaidi, lakini utaratibu ule wa kwenda kuwapa hela moja kwa moja Wakandarasi kama ambavyo umefanya pale Chalinze, ndiyo ambao umetufikisha hapa.

Mimi nakuomba sana Mheshimiwa Waziri ambaye ninaamini kabisa kwa experience yako kama Engineer, msomi mzuri na ambaye uko tayari kuhakikisha kwamba maisha ya watu yanatoka katika taabu wanayoipata naomba jambo hili uliangalie vizuri sana. Nasema hivi Mheshimiwa Waziri ni kwa sababu siyo mara ya kwanza kutoa ushauri mzuri wa namna hii.

Mheshimiwa Spika,nimewahi kutoa ushauri wa namna hii miaka mitatu iliyopita, juu ya kujengwa kwa tekeo pale katika chanzo chetu Wami, lakini miaka yote Mheshimiwa Waziri imekuwa ni uamuzi ambao au ushauri ambao hamkuwahi kuufanyia kazi. Faraja yangu leo hii kwenye kitabu hiki katika moja ya jambo kubwa ambalo mnakwenda kulifanya pale Chalinze ni kwenda kutengeneza lile wazo ambalo niliwashauri na kipindi kile nilishangaa kwa nini halikufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo pia nimesoma vizuri kitabu chako cha hotuba ya bajeti Mheshimiwa Waziri. Uharibifu mkubwa unaofanyika katika vyanzo vyetu ni kweli lakini katika jambo ambalo sikuliona humu ndani ni nafasi ya mifugo yetu tunayokwenda kunywesha katika vyanzo vyetu na ambayo inapelekea kuharibu vyanzo hivyo. Jambo hilo hamjalizungumza humu ndani, lakini nikupe mfano mmoja wa Chalinze hasa kwa ndugu yangu kule Mheshimiwa Murrad hayupo humu ndani leo, kwamba katika eneo kubwa ambalo linasababisha matatizo ni mifugo ya wafugaji inayopelekwa katika chanzo cha Mto Wami ambayo inapelekea kuingiza matope mengi na udongo mwingi katika maji ambayo ikipeleka kule kwenye tekeo letu lililopo linapelekea panajaa matope na hata pia wakati mwingine maji yale tunashindwa kuzalisha kwa wingi kwa sababu ya uchafu huu ambao unaletwa na mifugo hiyo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hiyo pia Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana kwa hatua kubwa ambazo mmekwishazifanya, Serikali mkishirikiana na Wizara ya Mazingira kwa jinsi ambavyo mnaendelea ku-preserve vyanzo vyetu vya maji na kuvifanya vyanzo vyetu viendelee kuwa salama. Ninaamini kama hamtoliangalia hili jambo la mifugo yetu inayofugwa na kunyweshwa kiholela katika vyanzo vyetu, hata yale mazingira mazuri ambayo mnatengeneza itakuwa nayo ni taabu tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo lingine Mheshimiwa Waziri ambalo umelizungumzia kwa ufundi mkubwa zaidi ni usimamizi wa mamlaka za maji. Mheshimiwa Waziri ni ukweli kazi kubwa mnaifanya na maji hayawezi kutoka vizuri kama usimamizi utakuwa poor, lakini nikizungumza kwa mfano wa Mradi wa Maji wa Chalinze bado tumeendelea kuwa na taabu kubwa sana katika usimamizi wa maji yale. Imefika kipindi kwamba hata unapotaka kuuliza maswali yanayohusu maendeleo ya mradi ule kumekuwa na sintofahamu kwamba huyu anaweza kukwambia hili, huyu akakwambia hili, lakini haya yote ni kwa sababu nazungumzia tu lile kwamba kutokuwa na utaratibu mzuri juu ya upashanaji wa habari, lakini pia juu ya usimamizi mzuri wa maji yetu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo pia Mheshimiwa Waziri liko eneo kubwa ambalo nimekuwa na interest nalo sana ni katika miradi ya matokeo ya haraka.

Mheshimiwa Waziri unakumbuka ulipokuja mara ya mwisho wakati nazungumzia juu ya kusuluhisha tatizo la maji Chalinze, tulizungumza juu ya mradi wa maji yatakayotoka Ruvu kwenda Chalinze mpaka maeneo ya Mboga kwenye kiwanda kikubwa kinachozalisha products za matunda. Mheshimiwa Waziri mradi ule kwangu ni moja ya miradi ambayo naiona ni miradi ambayo inatupelekea kupata matokeo mazuri katika muda mfupi. Kitu cha ajabu zaidi katika kitabu chako hiki hakuna sehemu ambayo mradi ule umetajwa, labda sijasoma vizuri lakini kwa kuangalia kwangu katika pages zinazozungumzia miradi ya namna hiyo ya matokeo ya haraka, mradi ule haupo. Mheshimiwa Waziri naomba utakaposimama utujibu kwamba mradi ule umekufa, mmekataa kuuanzisha au ni nini kinachoendelea ili wananchi wa Chalinze wajue kama tunaendelea kunywa maji pamoja na mifugo katika malambo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja hilo, ninakupongeza sana kwa hatua kubwa unazoendelea kuzifanya hasa ile taarifa ya ukamilishaji wa uchambuzi au upembuzi yakinifu katika Mradi wa Maji wa Kidunda. Mheshimiwa Waziri mradi ule ulipofikia sasa hivi wanachohitaji ni pesa na katika kitabu chako hiki ukurasa wa 57 mmeeleza juu ya matarajio yenu ya kutafuta pesa ili mradi uweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri katika jambo hili naomba tu nikutie moyo na kukupa nguvu zaidi ya kwamba ukamilifu wa mradi ule ndiyo ukombozi wa watu ambao tunategemea sana mradi huu. Bwawa la Kidunda litakapokamilika faida zake kama ulivyozieleza kwenye kitabu, lakini niwaongezee kwa faida ya Watanzania wengine kwamba maji mengi tunayopoteza yanayokwenda baharini tutayapunguza. Leo hii ukienda pale kwa mfano kama ukitoka Msata unakwenda Bagamoyo, unaona katika lile Bonde la Mto Ruvu lilivyojaa maji mengi sana, maji yale mengi Mheshimiwa Waziri tunayapoteza ambapo kama tungeweza kutengeneza mabwawa makubwa kama la Kidunda, tungeweza kuwa na faida kubwa sana ya kupata maji ambayo wakulima wetu wa Bagamoyo pale wanaotegemea bonde lile wangeweza kufaidika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu, pia tunategemea kupata nguvu ya umeme ambayo pia najua watu wa Chalinze na maeneo mengine ikiwemo watu wa Morogoro Vijijini tutaweza kufaidika nalo sana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikupe moyo na kuendelea kukupa nguvu kwamba jambo hili lisimamie kwa sababu hapa ndiyo unakwenda kuwakomboa Waswahili au Watanzania wanaoishi katika maeneo ya Pwani hususan eneo la Chalinze, Bagamoyo na Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa sana maana leo ni siku ya kushauri tu ni eneo la Jangwani. Wengine tunaishi Dar es Salaam pia, eneo la Jangwani hasa katika Bonde la Jangwani pale ambapo kuna Mradi mkubwa wa Mabasi ya Mwendokasi, matope au mchanga umejaa mpaka umekaribia sasa kufikia level ya chini ya daraja. Ninavyofahamu kwa udogo wake, kwamba mchanga au matope yakijaa maana yake maji yatapita juu ya matope yale na ndiyo jambo ambalo limepelekea leo hii bonde lile panaponyesha mvua hata ya mililita mia moja yanapita juu ya daraja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmeandika vizuri katika kitabu chenu kwamba sasa mnataka kutafauta kujenga mabomba makubwa ambayo yatasafirisha maji taka. Bonde la Jangwani sidhani kama linahitaji mabomba makubwa ya kusafirisha maji taka. Bonde la Jangwani linachohitaji ni master plan nzuri ambayo inaweza ikasaidia kutatua tatizo lile moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii ukija na hadithi ya kutengeneza mabomba unachozungumzia ni kutafuta maji yapite wapi, tatizo la Jangwani siyo maji yapite wapi, tatizo la Jangwani kwamba watu wamejenga, wameziba njia, wameharibu miundombinu na wameharibu mazingira. Kinachotakiwa ni kutengeneza master plan mpya ambayo itahakikisha kwamba maji pale yanapita vizuri kufika katika Bahari yetu ya Hindi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miaka minne kama siyo mitano iliyopita alikuja mama yangu Mheshimiwa Profesa Anna Tibaijuka akatupa mpango mkakati juu ya jinsi gani wanataka kutengeneza Bonde la Jangwani ili liweze kuwa sehemu nzuri ya kivutio, lakini pia liweze kutumika kwa ajili ya kupitisha maji, mpango ule sijui ulifikia wapi. Taarifa nilizonazo ni kwamba ulikataliwa lakini pamoja na kukataliwa huko kuna kitu cha muhimu cha kufanya ambacho Mheshimiwa Waziri nina uhakika kabisa unajua na wewe nina hakika umetembea.

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa London wametengeneza mto wao pale ambao unaitwa River Thames ambao unapita katikati ya Jiji la London, umekuwa ni sehemu ya kivutio na sehemu nzuri, leo hii London hawana wasiwasi wa kupata mafuriko, tunashindwa nini kutengeneza

Bonde la Jangwani lile kutoka katika maeneo ya Tabata mpaka kwenye Daraja la Salender ili maji yaende baharini na maji yanayotoka baharini, na maji yanayotoka baharini hata ikiwezekana baadae huko kama nchi itakuwa imepata mambo mazuri zaidi ikiwezekana tutengeneze boats nazo ziweze kupita pale zipeleke watu mpaka huko Tabata na iwe sehemu ya kivutio pia katika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la mabwawa, Mheshimiwa Waziri naomba nikukumbushe wakati Mheshimiwa Maghembe, Mbunge kwa sasa akiwa Waziri wa Wizara yako, Serikali ilibuni mradi wa kutengeneza bwawa kubwa la maji katika Kijiji chetu cha Mjenge kule Kibindu, Chalinze. Bwawa lile lilikuwa ni substitute ya mradi wa maji wa Wami – Chalinze, mradi ambao kwa mujibu wa mchoro wake ulikuwa haufiki katika eneo la Kata ya Kibindu. Mheshimiwa Waziri nimejaribu kutazama kitabu chako hiki, katika hotuba ya mwaka jana bwawa hilo limetajwa, lakini mwaka huu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja naomba bwawa hili nalo lifanyiwe kazi, ahsante sana.