Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mungu kwa kutujalia uzima na afya ya kuweza kuhudhuria Bunge letu. Namshukuru Mungu kwa kutupa Rais mwadilifu mwenye mapenzi mema na wananchi wake na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu na Baraza la Mawaziri wachapa kazi. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo na Manaibu wake, Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege. Binafsi natoa shukrani za pekee na za unyenyekevu kwa Rais na Baraza zima la Mawaziri kwa jinsi walivyotekeleza miradi ya maendeleo mikubwa Ileje ambayo ilisahauliwa miaka mingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMISEMI. Shukrani kwa Mungu. Pongezi kwa Serikali ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Baraza lote la Mawaziri kwa mipango ya maendeleo mikubwa inayotekelezwa kwa ufanisi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pongezi kwa ajili ya Ileje. Kwa heshima ya kipekee na kwa niaba ya Wanaileje napenda kuishukuru Serikali kwa mambo makubwa iliyofanya kuleta maendeleo Ileje. Napenda kupiga magoti kutoa shukrani za dhati kwa kuiwezesha Ileje kuinuka, kujulikana na kutambulika. Ileje sasa hivi inaonekana, barabara iliyopigiwa kelele kwa zaidi ya miaka 40 imepata mkandarasi yuko site na barabara itajengwa kwa kiwango cha lami kilometa 58, inategemewa kumalizika 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata fedha ya kujenga vituo vya afya viwili, Kituo cha Lubanda ambacho Mheshimiwa Waziri wa Afya mwezi uliopita alitembelea na Kituo cha Ibaba. Hii itatusaidia sana kupunguza athari zilizokuwa zinawapata wananchi kwa sababu ya jiografia na miundombinu na Ileje hizi ni kata ambazo hazifikiki kwa urahisi na ziko mbali sana na hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata fedha ya kujenga hospitali ya wilaya na inajengwa kwa kiwango cha asilimia 75, imesimama kwa miaka mitatu, lakini nashukuru kuwa nina taarifa kuwa, tumetengewa fedha ya kumaliza ujenzi wa hospitali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ilipokea fedha kwa ajili ya kukarabati shule kongwe na miradi mikubwa ya maji na masuala ya upimaji viwanja Ngulilo, Ilulu, Izuba. Kupitia Ofisi ya Mbunge nilitafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa VETA kutoka Balozi wa Japan. Chuo kimejengwa na nashukuru kuwa, Serikali imekubali kukichukua chuo hicho na kukimalizia na kukiendesha.

Tunaishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo kwa mwaka mmoja uliopita hadi sasa tumetembelewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyeweka jiwe la msingi na Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Waziri kwa nyakati mbalimbali. Naamini huu ni ugeni mkubwa sana uliowahi kutokea katika historia ya Ileje. Hii, ilitutia moyo sana, lakini iliwawezesha Waheshimiwa viongozi hawa kujionea wenyewe changamoto na fursa za Ileje na kwa hivyo, kujua jinsi gani Ileje isaidiwe. Tunawaomba Mawaziri wengine wote watembelee maeneo yote ya pembezoni ili kujionea changamoto zao na kuzitatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi zote hizo nyingi na shukurani za unyenyekevu kwa miradi mikubwa ya maendeleo, yapo mambo machache ninayotaka kuiomba Serikali yangu sikivu ya Chama cha Mapinduzi. Tutashukuru kama fedha iliyotengwa kwa hospitali ya wilaya itatolewa mara moja ili huduma hii muhimu ya afya wilayani iimarike na tuache kupeleka wagonjwa Malawi maana Mbeya ni mbali sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ni Wilaya ya mpakani mwa Tanzania na Malawi na kwa sehemu ndogo Mashariki Kusini na Zambia. Mpaka wenye umbali wa kilometa 108. Kwa hiyo, ni mpaka mrefu na wilaya yetu haina kituo cha mpakani madhubuti na mpaka wetu ni Mto Songwe. Kwa hiyo, tunaomba uhitaji mkubwa na wa haraka wa gari la doria kwa ajili ya kudhibiti mpaka wetu. Wahamiaji haramu wengi wanapitia Ileje kuingia Malawi kuelekea Afrika Kusini na imefikia hadi upande wa Malawi kuanzisha Kituo cha Wakimbizi kwa ajili hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2015, TRA walionesha haja ya kujenga kituo cha mpakani na tayari wameshapata eneo la kutosha Isongole, karibu kabisa na mpaka. Umuhimu wa mpaka huu ni mkubwa na hasa ikizingatiwa suala la usalama, lakini pia, kiuchumi na biashara za mipakani. Kwa kuwa, Barabara ya Mpemba – Isongole inajengwa itaunganisha Tanzania na nchi jirani ya Malawi na kituo hiki kitapunguza msongamano wa Kituo cha Tunduma na kuwezesha magari ya mizigo na abiria mengine kupitia upande wa Ileje hasa kwa yale yanayotokea Malawi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zilizopo ni kuwa barabara ya Chilipa kutokea Ileje ni tambarare zaidi kulinganisha na ya Kasumulo kwa hiyo, madereva wa mizigo wangeweza kuitumia kwa urahisi zaidi. Vilevile Malawi na Tanzania tuna biashara kubwa na kituo cha forodha kitawezesha kukinga mapato mengi na kusimamia ubora wa bidhaa zinazopita hasa za mazao na mifugo kuzuia magonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaipongeza Wizara kwa ubunifu wa kuhamisha Walimu wa masomo ya sanaa kutoka shule za sekondari kwenda kujaza nafasi shule za msingi, zoezi hili kama ilivyo kwenye wilaya nyingine chache, kwa Ileje limezua malalamiko kwa Walimu 83 walioguswa nalo na kuleta mgongano kwa kuwa, kuna imani kubwa kuwa zoezi limetumika kukomoa Walimu wanaoonekana kuwa wakorofi na kuhamisha wale ambao wana degree hadi masters na kuwaacha wenye stashahada kama agizo la Serikali lilivyokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi baada ya kuahidiwa malipo, hii inabadilika, kufuatia Walimu walioitwa mbele ya Kamati ya Ulinzi na Usalama na kuhojiwa kwa vitisho. Zoezi la kawaida limegeuka kuwa vita kwa sababu, ya jinsi lilivyotekelezwa na Mkurugenzi wa Ileje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira umesimama kwa miaka zaidi ya nane na pamoja na STAMICO kuruhusu hakuna kinachoendelea kwa uhakika. Mwaka huu tulielezwa kuwa, uzalishaji wa majaribio umefanywa, lakini hatujajua kama unaendelea na kwa
utaratibu upi kwa sababu, mpaka sasa hatufahamu mwekezaji ni nani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hatupewi taarifa juu ya taratibu za uhamishaji mgodi toka mwekezaji aliyeshindwa na STAMICO kama umekamilika ama vipi na suala la ubora wa makaa na matumizi kusudiwa. Wananchi wa Ileje wangependa kufahamu maana mgodi huu ni tegemeo lao kwa ajira na mapato kwa Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile daraja la mgodini Kiwira kutoka barabara ya Mto Mwalisi linahitajika kujengwa ili kuepuka usumbufu wa kupitia Wilaya ya Kyela kuja Ileje, umbali wa kilometa 36 wakati daraja linalohitajika ni kilometa saba tu kuufikia mgodi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingi za ndani ya Ileje zinazounganisha kata zinashindwa kujengwa kwa sababu ya ukomo wa bajeti. Changamoto ipo katika barabara zinazounganisha vijiji na vijiji, mfano, madaraja matatu kutoka Kijiji cha Bwenda kuja Makao Makuu Kata ya Lubanda mpaka uzungukie Kata nyingine ya Luswisi. Daraja toka Kata ya Ibaba kuunganisha Kata ya Ngalilo kupitia daraja la Shilinga lingesaidia kuwaunganisha wananchi na wilaya na mkoa wao lakini hawa wametengwa kwa kukosa daraja hili. Daraja la Kajeshi kuunganisha Sekondari ya Bupogo, daraja la Bupigu kwenda Chongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umaliziaji wa zahanati pamoja na Mfuko wa Jimbo haujakamilika. Upungufu wa watumishi ni mkubwa sana Idara ya Afya na ukamilishaji wa vituo vya afya, zahanati na hospitali ya wilaya kutahitaji watumishi wengi zaidi. Vyoo mashuleni pamoja na Mfuko wa Jimbo bado kumalizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Elimu Sekondari na Msingi; kuna upungufu wa Walimu 50 na 482; Uchakavu wa miundombinu ya madarasa na nyumba za Walimu ambayo mengi yalijengwa kwa udongo muda mrefu; Ukosefu wa gari la Idara ya Elimu Msingi; na Upungufu wa matundu ya choo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kilimo kuna kuchelewa kwa pembejeo na Ukosefu wa masoko ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji. Upungufu watumishi idara ya maji na vitendea kazi kwa usimamizi na ufuatiliaji wa miradi ya maji. Kukosekana kwa chujio la maji kwa Mradi wa Maji Humba – Isongole kunafanya tuendelee kupata maji yenye matope na kwa hivyo, siyo salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutotolewa fedha yote ya miradi ya maendeleo na kwa wakati kunaathiri sana miradi ya maendeleo na kuchelewesha maendeleo ya wilaya ambayo tayari imekuwa nyuma kimaendeleo muda mrefu kwa sababu, miradi mingi inawekwa kwenye bajeti kila mwaka bila utekelezwaji. Serikali itoe kipaumbele kwa wilaya za pembezoni na hasa zenye mvua nyingi ili zipatiwe fedha ya kutosha kwa ukarabati wa barabara za vijijini katika wilaya hizi ili ziweze kutumika kwa mwaka mzima kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya wilaya hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inasifika sana kwa utawala bora na tunaishukuru sana Serikali kwa kusimamia utawala bora na amani na utulivu mkubwa. Ziko nchi zinazotuzunguka ambazo hata kwenda kukutana na Waziri utoe rushwa? Pia mishahara inalipwa kwa kubahatisha, nchi zina rutuba lakini uzalishaji hakuna na wanaishia kutegemea nchi jirani. Amani haipo na mifumo yote imevurugwa. Sisi Tanzania tuna kila kitu, tunaomba sana watendaji wachache wanaotuvurugia utawala bora hasa Wakurugenzi na wale wasiozingatia maadili basi wachukuliwe hatua kali za kinidhamu ili iwe mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje tuna Mkurugenzi ambaye amevuruga sana Madiwani, Walimu, Watendaji chini yake na hata wananchi tumeshatoa malalamiko kwa Waziri Mkuu na kwa Waziri wa TAMISEMI. Tunaomba wamwelekeze aache au kwa kuwa, uwezo wake ni mdogo basi atafutiwe atakapoweza kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.