Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na watendaji wenzake kwa kazi kubwa wanayofanya katika Wizara hii. Hata hivyo, napenda kushauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ugatuaji wa madaraka D by D halitekelezwi inavyopaswa kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara hii, ningependa kufahamu ni wapi wanapokutana kuweka masuala ya elimu sawa? Hizo hati idhini walizonazo zinawakutanisha kwenye masuala gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano suala la Walimu wa Shule za Sekondari kuhamishiwa katika Shule za Msingi ni mambo gani wamejadiliana na Wizara ya Elimu, hususan, suala la mafunzo (Induction Course) kwa Walimu hawa? Nani atatoa mafunzo ya Child Centered Psychology ambayo ni kipaumbele kwa Walimu hawa kwa kuwa, tunafahamu kwamba, Wizara ya Elimu ndio mtoaji wa mafunzo? Je, Wizara imeshawaandalia fedha zao za uhamisho au posho ya usumbufu? Mheshimiwa Waziri anapohitimisha atuambie ni nini watakachokitekeleza kwa Walimu hawa hasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upungufu wa Walimu shule za msingi na Walimu wa sayansi kwa shule za sekondari. Tatizo hili ni kubwa, katika Mkoa wa Iringa hadi 2017 kulikuwa na upungufu wa Walimu shule za msingi 785, kwa Walimu wa sekondari sayansi mahitaji yalikuwa 1,290, waliopo 619, upungufu Walimu 671. Tatizo hili ni kubwa, hivyo nashauri Wizara iajiri Walimu wa kutosha na wapelekwe hasa shule zilizopo vijijini na wapewe motisha ya mazingira magumu ya ufundishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya; kuna tatizo ama upungufu wa watumishi katika sekta hii, hasa kwa Mkoa wa Iringa katika zahanati na vituo vya afya, Wilaya ya Kilolo na Iringa Vijijini hasa. Naiomba Serikali iajiri watumishi hawa na kupelekwa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Barabara, TARURA. Hiki ni chombo muhimu sana, lakini kina changamoto ya uhaba wa fedha. 30% wanayopata ya fedha ni kidogo sana kukamilisha miradi. Naungana na maoni ya Kamati kuongeza hadi angalau 50% ya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba barabara inayounganisha Wilaya toka Iringa Manispaa kupitia Jimbo la Kalenga, Kata ya Luhota na Magulilwa kwenda Wilaya ya Kilolo ambazo ni kilometa chache tu zitengewe bajeti na kujengwa kwa kiwango cha lami kwani kuna wafanyabisahara na wakulima wa mazao mbalimbali kama vile matunda, mahindi, njegere. Miti ambayo inazalisha mbao hupata tabu kupita katika barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na maoni ya Kamati kuhusu suala la kuwasilisha Bungeni Muswada wa kusudio la kutunga sheria itakayosaidia kusimamiwa utengaji, utoaji na urejeshaji wa fedha zinazotokana na 10% ya mapato ili kuwezesha wanawake na vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile suala la kuondoa kodi au kupunguza kodi kwa taulo za kike ili kuwezesha watoto wa kike hasa kutoka katika familia maskini kumudu gharama hizo na kuweza kuhudhuria masomo kikamilifu na ikiwezekana wapewe bure kama ilivyo katika nchi za Kenya, Shelisheli na nyinginezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utawala bora. Kumekuwa na kawaida katika Awamu hii kutoongeza mishahara kwa wafanyakazi wakati maisha kila siku yanapanda kwa gharama za bidhaa. Wafanyakazi wengi hawana raha kwa kutokuweza kukidhi mahitaji na kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi. Serikali iweze kupandisha au kuongeza mishahara kwa wafanyakazi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ukiukwaji wa sheria na taratibu. Mfano Mkurugenzi kutotii mamlaka ya Waziri mwenye dhamana mfano Mkurugenzi wa Tunduma Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Wilaya na wengineo wateule wa Rais kutofuata taratibu. Hii ni kinyume kabisa na utawala bora tunaotarajia, Serikali ilifanyie kazi suala hili ili wananchi wapate haki yao ya kupata maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.