Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza kazi nzuri sana inayofanywa na viongozi wa Wizara hii na Rais wetu. Mheshimiwa Rais amekuwa mzalendo na mtu ambaye yuko tayari kufa kwa ajili ya kutekeleza kazi za kizalendo kwa nchi yake. Tumeona hatua mbalimbali alizozichukua kwa kunusuru uchumi wa nchi hata zile ambazo zinahitajika uamuzi mgumu, ni Rais mwenye maamuzi na anasimama kidete kulinda msimamo wake ambapo mara zote ni wa kizalendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Selemani Jafo ni kijana shupavu mwenye kufanya kazi kwa weledi mkubwa, mara zote anakonga nyoyo za Watanzania. Mheshimiwa Jafo hakika amejaa kwenye nafasi yake hongera sana Mheshimiwa jafo. Nawapongeza pia Manaibu Mawaziri wawili Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Kakunda, wote kwa hakika wanakonga nyoyo za Watanzania kwa uchapakazi wao. Mheshimiwa Rais ni kweli ana macho mengi kubaini wateuzi wake kuwa watendaji wanaoakisi barabara mwelekeo na kasi ya Mheshimiwa Rais mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze kwa dhati ya moyo wangu Katibu Mkuu wa Wizara, Mheshimiwa Mussa Iyombe, kiongozi mzoefu wa siku nyingi kwa kazi nzuri sana anayofanya kuongoza Wizara, lakini pia kupata nafasi ya kusikiliza Wabunge katika changamoto mbalimbali, Mungu akuzidishie maisha aendelee kutoa uongozi kwa Watanzania. Mwisho, niwapongeze Manaibu Waziri na Katibu Mkuu kwa kazi nzuri sana; ndugu Zainabu Chaula na Tixon Nzunda, Wizara iko vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, elimu, Wilaya ya Nkasi tumejenga vyumba vya madarasa vitatu, kila shule ya msingi kuna madarasa yapatayo 348 yote yamefikia mtambaa panya yaani yamekamilka katika ujenzi wa ukuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walihamasishwa na sisi viongozi tukiongozwa na kamanda wetu DC Said Mtonda, watusaidie wananchi watashindwa kutuelewa. Tunaomba watupatie fedha ili juhudi hizi ziwe na manufaa yaliyokusudiwa na nadhani Nkasi inaweza kuwa ni Wilaya ya kwanza nchini, naiomba Wizara ilipe fedha ili pia iwe na maana ya kutupongeza na kuhamasisha maendeleo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tumekosa watumishi wa kutosha katika sekta ya elimu hasa shule za msingi bado Walimu hawatoshi hasa maeneo ya mwambao mwa ziwa, Kata za Kala, Wampembe, Kizumbi na Ninde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, nyumba za Walimu hazitoshi kwenye shule za msingi na sekondari pia tunaomba fedha ili watumishi hawa muhimu wapate mahali pa kuishi ili watulie kazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, wananchi wa Jimbo la Nkasi Kusini wamejitahidi kujenga maabara katika sekondari zote na sasa yamebaki magofu, watusaidie kutoa fedha ili kukamilisha ujenzi wa maabara ili pia majengo yatumike kupata wataalam wa sayansi kama Walimu wa Waganga na wataalam wa maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, fedha za miradi kwenye halmashauri yetu hazijakuja hasa kwa miradi iliyopitishwa mwaka jana. Fedha iletwe haraka kukamilisha miradi iliyopendekezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, kilimo, kwa Mikoa wa Nyanda za Juu Kusini msimu wa kilimo huanza Oktoba kumbe pembejeo zifike Agosti kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, saba, Mawakala wa mbolea wapewe masharti ya kufikisha pembejeo kwenye mikoa ya uzalishaji siyo kurundika Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nane, Serikali itenge fedha kwa ajili ya top up kuwezesha bei za pembejeo zisibadilike badilike katikati ya msimu kutokana na mabadiliko kwenye bei ya dunia ili kutoleta usumbufu kwa wananchi. Hii ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tisa, wananchi wa Vijiji vya Kaso, Milundikwa, Kisura na Malongwe wameathirika sana na ujio wa jeshi ambapo ardhi yao waliyopewa kihalali na nyaraka zipo wamenyang’anywa. Naishauri Serikali kuliangalia jambo hili vizuri na Mheshimiwa Waziri naomba amwagize Mkuu wa Mkoa akafanye tathmini ili kuona hali iliyojitokeza zaidi ya watu 5,000, hawana pa kulima kabisa na ni wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumi, naomba gari ya kusaidia kazi ofisi ya kilimo ambao hawana fedha kabisa za kufanya matengenezo ya mara kwa mara gari yao mbovu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya hali ya huduma za afya kwenye zahanati zetu siyo nzuri kwa tatizo la ukosefu wa watumishi hatuna Waganga, Manesi na watumishi wengine. Tunaomba watusaidie kupata watumishi, zahanati nyingi zinaendeshwa na Wauguzi. Wananchi kujenga zahanati katika Vijiji vya Kautawa, Kipande, Kalundi, Mkomanchimbo, Mlambo, Tundu, Kisambara, Ifundwa, Nchenje, Ntuchi na zinginevyo, watusaidie kumaliza zahanati hizi. Wananchi pia wanajenga Vituo vya Afya vya Kasu Kala, Kate na Ninde. Tunaomba kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakushukuru sana kuona Serikali imeweka kwenye bajeti yake, ujenzi wa hospitali ya wilaya, nampongeza kwa hatua hiyo, lakini nashauri kutekeleza ujenzi kwa mtindo wa force account, impact itaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gari ya wagonjwa Wilaya ya Nkasi ina majimbo mawili, gari mbili zimetolewa kwa jimbo moja, mimi sijapata jambo hili halina afya kwa siasa za jimbo. Naomba gari moja Kala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maji, jimboni ina kasi ndogo, mwanzo kazi zilikuwa zinaenda vizuri, lakini kwa sasa kazi yake imepungua sana Serikali itoe usimamizi zaidi kwa miradi yote ya maji ikiwepo ya Kisura, Kawa, Mpasa na Isake ili kasi iongezeke na rasilimali zitumike kwa manufaa ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA hawana gari ya supervision, hawana fedha ya kutosha kwa matengenezo ya dharura, hali siyo nzuri barabara zifuatazo zimefungwa na zingine kupitika kwa tabu kabisa, barabara hizo ni:-

Barabara ya Kitosi- Wampembe kupitika kwa shida na daraja la Kizumbi limekatika na hakuna fedha. Barabara ya Ninde- Kala inapitika kwa shida sana makalvati yamekatika hakuna matengenezo na fedha hakuna. Barabara ya Namanyere- Ninde ijengwe ili kunusuru fedha iliyotumika kujenga madaraja na makalvati, lakini pia kufungua Kata ya Ninde iliyoko kandokando ya mwambao mwa Ziwa Tanganyika.