Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa namna anavyotekeleza miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Mheshimiwa Selemani Jafo, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na viongozi wengine wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utawala bora, Wizara imetoa mafunzo kwa watendaji na Wakuu wa Wilaya ili kuboresha utoaji huduma kwa jamii. Ili kuendelea kutoa huduma bora na kutatua kero za wananchi, naiomba Serikali yangu sikivu iwaelekeze watendaji na wakuu hao waliopata mafunzo, kutoa mafunzo kwa walio chini yao na pia katika ngazi za chini ili viongozi hao na wananchi waweze kujua haki na wajibu wao katika kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo tatizo katika Jimbo langu la Singida Kaskazini ambapo vipo Vijiji viwili vya Nduamughanya na Sagara vikishindwa kutoa huduma bora kutokana na jiografia ya maeneo ya vijiji hivi. Kijiji cha Nduamughanya kilichopo Kata ya Mughunge kina vitongoji vitatu ambavyo vipo umbali wa kilometa 23 kutoka Makao Makuu ya Kijiji vilitengwa na Msitu wa Hifadhi wa Mgori una kilometa 26 ukipita Handa katika Wilaya ya Chemba. Aidha, Kijiji cha Sagara pia kina vitongoji vitatu vilivyo kilometa nne kutoka Makao Makuu ya Kijiji na vimetengwa na mlima wa kuteremka bonde la ufa na hakuna miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivyo vitongoji vyake vinaweza kusajiliwa kuwa kamili kwa maana ya Kijiji cha Mukulu kwa vitongoji vitatu vya Kijiji cha Nduamughanya na Kijiji kipya cha Gairo kwa vitongoji vitatu vya Kijiji mama cha Sagara, vijiji tarajiwa vipya viwili tayari vimekwisha jenga shule za msingi ambazo zimekwishasajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta ya afya, tunashukuru Serikali kwa kututengea bajeti ya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hospitali mpya ya wilaya. Aidha, Halmashauri ya Singida ina vituo viwili tu vya afya (Ilongero na Mgovi) ambavyo havitoi huduma ya dharura ya upasuaji kutokana na kukosa miundombinu na wataalam.

Niiombe Serikali kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya haina hospitali ya wilaya na kwa sasa inategemea hospitali ya Mission ya Mtinko na ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ama Hydom Mkoani Manyara. Serikali itoe kipaumbele kwa vituo hivi viwili vya afya kupatiwa fedha za ukarabati na vifaa ili kunusuru maisha ya wananchi zaidi ya 280,000 wa jimbo hili.

Mheshimiwa, Mwenyekiti, zipo changamoto nyingi katika suala la elimu ya msingi na sekondari hasa katika miundombinu ya shule. Zipo shule katika jimbo langu mfano Shule ya Mikuyu iliyopo Kata ya Makuro ina madarasa mawili tu tangu watoto wa awali hadi darasa la sita na imesajiliwa na SG 02/2/040. Kwa sasa ina jumla ya wanafunzi 476, hakuna nyumba hata moja wa Walimu, ina choo cha muda, matundu manne kwa Walimu na wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ipo shule ya Msingi ya Ntundu, Kata ya Kinyeto yenye wanafunzi zaidi ya 1,600 na vyumba sita tu vinavyotumika, wanafunzi wanasomea nje kwenye eneo la wazi na Mwalimu anazunguka na kibao uwanjani kufundisha. Hili hii haiwezi kuleta maendeleo kwa watoto wetu na kuongeza ufaulu. Niombe Serikali iangalie shule hizi kwa jicho la pekee kusaidia juhudi za wananchi na halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali iangalie juhudi za wananchi katika ujenzi wa maabara nyingi ambazo hazijakamilika, zikamilishwe ili kuanza kutoa huduma kwa kuwa wananchi sasa wana kazi ya kuanzisha ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari kutokana na ongezeko la wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miundombinu ya barabara, Jimbo la Singida Kaskazini lenye jumla ya miundombinu ya barabara iliyohakikiwa ya kilometa 772.39 zimekuwa hazipitiki wakati wa mvua kutokana na zaidi ya kilometa 704.28 sawa na asilimia 91.18 kuwa za udongo. Naomba Serikali kwa kweli iweze kuongeza bajeti ili kuongeza urefu wa barabara za changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi wa Tatu, tarehe 11 tulimwomba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutusaidia kujenga barabara ya kilometa 42 kwa kiwango cha lami inayounganisha Kata za Kinyeto, Kinyagigi, Merya, Maghojoa, Msange na Itaja. Mheshimiwa Rais alikubali kupokea ombi letu na niombe Serikali sasa kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2018/2019 kuanza mchakato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.