Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri inayotarajiwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha wa 2018/2019. Serikali ya Awamu ya Tano imefanya mambo mengi muhimu ndani ya kipindi kifupi cha miaka miwili na nusu cha uhai wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto tuliyonayo wananchi wa Wilaya ya Mbogwe ni uhaba wa miundombinu ya majengo ya halmashauri pamoja na makazi na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Tunaiomba Serikali itusaidie kuhakikisha hospitali yetu ya Wilaya ya Mbogwe inaanza kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wanambogwe tunaiomba Serikali itusaidie kutupatia huduma ya maji ya uhakika kutoka Ziwa Victoria maji ambayo tayari yako katika Wilaya jirani ya Kahama ambayo ni wilaya mama ya Wilaya za Bukombe na Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya mpya ya Mbogwe tunaipongeza Serikali kwa kutupatia jumla ya Sh.800,000,000 kwa ajili ya Vituo vya Afya vya Iboya na Masumbwe. Kila kituo kimepewa Sh.400,000,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa elimu, wilaya yetu ya Mbogwe tayari inaendelea na ujenzi wa shule ya sekondari ya kidato cha tano katika Shule ya Sekondari Mbogwe, hata hivyo shule hii imeshindwa kufunguliwa kutokana na uhaba wa upatikanaji wa maji. Tunayo matumaini makubwa kuwa Serikali itasaidia juhudi za uongozi wa wilaya katika kuhakikisha kuwa shule hii ya pekee ya kidato cha tano Wilayani Mbogwe inafunguliwa mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali kuongeza juhudi za kutupatia watumishi katika sekta za afya na elimu kwani tunao upungufu mkubwa wa watumishi wa sekta hizi muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ambao ni Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini unafanya kazi zake vizuri, kinachotakiwa ni kuongeza ushirikiano baina ya idara hii na uongozi mzima wa wilaya ikiwemo Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi na Baraza la Madiwani ili kujenga umoja na mshikamano katika kutatua kero na matatizo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Wakala wa Maji Vijijini na Mijini ni wazo jema hasa ikizingatiwa kuwa wakala mbalimbali za Serikali zimeonesha mafanikio makubwa na kuwa na ufanisi wa kuwahudumia wananchi katika sekta hii muhimu ya maji hasa ikizingatiwa msemo usemao maji ni uhai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi ya mazingira ni jambo mtambuka kwani mabadiliko ya tabia ya nchi yamekuwa na athari mbaya kwa maisha ya mwanadamu na kusababisha ukame, uharibifu wa vyanzo vya maji, ukosefu wa mvua. Ni wajibu kwetu kama Taifa kuhakikisha tunatunza mazingira yetu kwa kuanza jitihada za kupanda miti na kuihifadhi na kujiepusha na tabia ya ukataji miti ovyo. Aidha, naishauri Serikali kufanya jitihada za makusudi kuongeza matumizi ya nishati mbadala ya kuni na mkaa kwa kuwekeza zaidi katika matumizi ya umeme, umeme jua na gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uti wa mgongo wa Taifa letu limekuwa likitilia mkazo yaani kilimo, naishauri Serikali kuweka mkazo zaidi katika uwekezaji wa viwanda vya mbolea nchini hasa ikizingatiwa kuwa nchi yetu imejaliwa kuwa na hazina kubwa ya gesi asilia ambacho ni chanzo muhimu cha malighafi ya utengenezaji wa mbolea. Mbolea ikipatikana kwa bei nzuri itasaidia kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo ambacho ni chanzo muhimu cha malighafi katika sekta ya viwanda ambayo imekuwa ni kauli mbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri.