Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi lakini pia nianze kwa kuwapongeza Mawaziri wote wawili kwa hotuba nzuri ambayo wamewasilisha nikianza na kaka yangu Mheshimiwa Mkuchika vilevile na Mheshimiwa Jafo na timu yake wakiwepo na Naibu Waziri Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege, hongereni sana kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwapongeze Watendaji Wakuu, kuna Dkt. Ndumbaro wa Utumishi lakini pia Kaka yetu Injinia Iyombe wa TAMISEMI; Dkt. Chaula pia na kaka yangu Nzunda, Naibu Makatibu Wakuu wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI, hongereni sana kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kwa pongezi kwa sababu asiyeshukuru kwa moja hata akipewa tano hatashukuru. Niishukuru TAMISEMI kwa uratibu mzuri wa ujenzi wa vituo vya afya na hospitali za wilaya. Wote mtakuwa mashahidi katika hotuba zilizopita tulikuwa tunauliza Ilani ya Chama cha Mapinduzi inasema kila kijiji kutakuwa na zahanati, kila kata kutakuwa na kituo cha afya, lakini mtekelezaji ni nani? Wizara ya Afya hawakuwa na mpango na TAMISEMI hawakuwa na mpango. Leo ukienda ukurasa wa 25 utaona mpango wa ujenzi wa vituo vya afya, hongereni sana TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vituo 208 ambavyo vinajengwa na vinakarabatiwa na mwezi Aprili vitajengwa vingine 25. Haya ni mapinduzi makubwa na wasikate tamaa kwa wale ambao wanawabeza kwamba watachukua sijui miaka mia tano kukamilisha nchi nzima, hiyo siyo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mipango ya maendeleo tunapanga kulingana na rasilimali zilizopo, mwaka huu wameweka fedha ya vituo 208, mwakani unaweza kuweka fedha ya vituo 1,000. Kwa hiyo, siyo sahihi kwamba kwa idadi ya vituo vya afya vilivyopo nchini tutakarabati kwa muda mrefu inategemea na upatikanaji wa rasilimali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya hivi hata elimu ya msingi, PEDP tukajenga madarasa, SEDP tukajenga madarasa na tukajenga maabara. Kwa hiyo, wasikate tamaa waendeleze kuweka mipango mizuri, watafute fedha kwa wafadhili ili tuongeze kasi. Tunatarajia bajeti ya mwakani tutaona ukarabati na ujenzi wa vituo zaidi ya 1,000 ili wale wanaowabeza wakose cha kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru kaka yangu Mheshimiwa Jafo, Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Kakunda wote mmefika Jimbo la Nanyamba na waliona hali halisi. Walipofika kulikuwa hakuna kituo hata kimoja cha afya na tukawaambia mikakati yetu kwamba hatusubiri fedha za Serikali, tunaanza kwa fedha zetu za korosho. Wakati tumeanza ujenzi wa OPD pale Dinyecha, namshukuru sana Mheshimiwa kaka yangu Jafo kwa sababu ametupa fedha shilingi bilioni moja na milioni mia nne kwa ajili ya ukarabati wa vituo vitatu vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwa sababu tuliona kwamba hakuna kituo cha kukarabati tukaanza na ujenzi, tumesimamia vizuri na yale majengo ambayo walisema tujenge tumeongeza mengine. Mheshimiwa Kakunda atakuwa shahidi pale Dinyecha walituambia tujenge wodi ya akinamama sisi tumejenga wodi mbili, tumejenga wodi ya akinamama na wodi ya jumla lakini tumejenga na OPD kwa fedha za korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na fedha za TAMISEMI lakini na sisi kwenye mipango yetu tumeongeza fedha. Pale Majengo wametupa shilingi milioni mia nne na sisi tumeongeza shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa OPD. Nimshukuru vilevile ametupa ambulance, Mheshimiwa Jafo amefanya kitu kikubwa sana kwa mara ya kwanza ambulance imeingia Halmashauri ya Mji wa Nanyamba, tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu Mheshimiwa Waziri amesoma Halmashauri ya Mji wa Nanyamba ni miongoni mwa halmashauri zitakazopata fedha za ujenzi wa hospitali ya wilaya. Kwa hiyo, namshukuru na nampongeza kwa sababu ameangalia mahitaji halisi ya halmashauri yetu na jinsi sisi wenyewe tunavyotumia rasilimali chache tulizonazo kuwekeza katika afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye suala la Madiwani. Ukisoma Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Toleo la mwaka 1977, Ibara ya 145 na 146 inazungumzia kuanzishwa kwa majukumu ya Serikali za Mitaa. Madhumuni ya kuanzisha Serikali hizi ni kupeleka madaraka kwa wananchi na kuna Diwani ambaye ni mwakilishi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie sasa package ya Madiwani hawa. Madiwani hawa wana majukumu mengi, wana kazi nyingi lakini bado package yao hairidhishi. Madiwani wana malalamiko, wana matumaini makubwa sana na Mheshimiwa Jafo, awasikilize Madiwani hawa. Aunde Tume afanye tathmini ya majukumu ya Madiwani aangalie ukubwa wao wa kazi na si vibaya sasa kupitia posho zao na maslahi yao kwa sababu posho yao ambayo wanayo sasa hivi ina zaidi ya miaka sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tusiwajibu majibu mepesi mepesi kwamba uwe na kazi nyingine au uwe na shughuli nyingine ndiyo uombe udiwani, Diwani ana majukumu mengi, kumlipa shilingi laki tatu kwa mwezi na Diwani huyu unategemea asimamie miradi ya maendeleo, asimamie fedha za halmashauri lakini kwa mujibu wa sheria zetu Baraza la Madiwani ndiyo mamlaka ya nidhamu kwa watumishi wa halmashauri, kwa posho ya shilingi laki tatu uhukumu kesi ya Mkuu wa Idara ambaye ana mshahara wake ni shilingi milioni mbili ni rahisi kuwa corrupted.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutengeneze vizuri package ya Madiwani ili wafanye kazi kwa uaminifu, kwa uadilifu ili kusukuma maendeleo ya halmashauri zetu. Kama ninavyosema Mheshimiwa Jafo wana matarajio makubwa sana na yeye, awasikilize, atengeneze timu ikawasikilize, afanye tathmini tuje na kitu kipya kwa Madiwani wetu kama anavyofanya reform katika maeneo mengine pale TAMISEMI na mimi nina matarajio na Mheshimiwa Waziri na najua hatawaangusha Madiwani wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la tatu, kuna fedha zinaitwa payment for result ambazo zinakwenda kwenye mamlaka zetu za Serikali za Mitaa na zinakwenda kwenye sekta zote za elimu, afya nafikiri na maji. Fedha hizi TAMISEMI sijaona kwenye kitabu chao, nikawa najiuliza fedha hizi wanatoa TAMISEMI au Wizara ya Elimu. Kama zipo Wizara ya Elimu naomba nishauri fedha hizi ziende TAMISEMI ili Wizara ya Elimu ibaki na mambo ya sera tu. Hawa ambao wanakwenda field na TAMISEMI sasa hivi wana kitengo kizuri cha ufuatiliaji wa fedha kwenye Serikali za Mitaa na Mkoani, hizi fedha ziende kwao lakini vilevile zionekane kwenye vitabu. Wenzao wa Wizara ya Maji mwaka jana walionesha kabisa fedha za OC na fedha za P for R.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wao pia Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Elimu waige wanavyofanya Wizara ya Maji, inaonekana kabisa na zile key performance indicators zionekane kwamba halmashauri inapata fedha nyingi kwa sababu ipi. Wizara ya Maji walitengeneza vizuri kabisa na hata sasa hivi wameshatoa matokeo ya halmashauri na TAMISEMI waige kitu kama hicho ili tusije tukawa tuna hisia tu kwamba zimepelekwa nyingi Nanyamba kwa sababu Mheshimiwa Kandege na Chikota ni marafiki, hapana. Tupeleke kwa vigezo vilivyowekwa na vya wazi na halmashauri ziwe zimeshindanishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la TARURA. Nami niungane na wenzangu kuwapongeza TAMISEMI kwa kuanzisha TARURA na TARURA inafanya vizuri. Ningeomba Waheshimiwa Wabunge tuipe muda TARURA tusianze kuwalaumu, huwezi kumlaumu mtoto wa mwaka mmoja ukasema hawezi kutembea. TARURA imeanzishwa na imeanza kufanya kazi vizuri, tuipe muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA wana changamoto ya rasilimali fedha, watumishi na usafiri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Jafo natarajia kwa kipindi hiki atapunguza haya matatizo ambayo TARURA wanakabiliana nayo. Suala kubwa ambalo tunamwachia Mheshimiwa Jafo na hili ningependa kusikia kauli yake wakati wa kuhitimisha ni kile kilio chetu cha Wabunge kwamba mgao ubadilishwe, wa fedha za Road Fund ambazo zinakwenda TANROAD na hizi za TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna majukumu mengi TARURA wanayo na network ya barabara za vijijini ambazo mwananchi wa kawaida, mpiga kura akiamka anakutana na barabara za TARURA halafu ndiyo anakwenda za TANROAD. Kwa hiyo mgao ubadilishwe…

(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa wakiongea bila mpangilio)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.