Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Kwanza nianze kwa pongezi za dhati kabisa, napenda kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kazi kubwa aliyoifanya hasa kwenye jimbo langu. Ameleta mageuzi makubwa sana kwenye sekta karibu zote, kwenye miundombinu, maji na pia sasa hivi hata kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kumpongeza Mheshimiwa Jafo, Waziri wa TAMISEMI na Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege Naibu Mawaziri, wamefanya kazi kubwa sana na kweli kazi imeonekana. Wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini wamenituma nizilete pongezi zenu hizo pamoja na wataalam wenu katika Wizara zenu ikiwemo na Wizara ya Utumishi wamefanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazitoa hizo pongezi kwa sababu moja tu. Jimbo la Mbeya Vijijini tunategemea sana kilimo lakini tulikuwa hatuna barabara kabisa huko vijijini, mazao tulikuwa tunashindwa kuleta mjini. Leo hii tuna kilomita za mtandao kama 1,007, tulikuwa hatuna barabara kabisa za kuaminika. Tulikuwa na kilomita moja tu ya barabara ya lami ukiachilia mbali zile barabara za TANROAD kwa barabara yetu ya TANZAM ya kutoka Dar es Salaam kwenda Zambia. Hivi navyozungumza kutokana na jitihada alizofanya Mheshimiwa Jafo na timu yake pamoja na matunda mazuri ya ziara yake, leo hii kuna maandalizi ya kilomita 37 ambazo zitajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizo kilomita 37 lakini leo hii kuna design ya kilomita 126 ambazo nazo tunategemea zitajengwa kwa kiwango cha juu. Kwa vile pesa zipo wakimaliza design tu hizi barabara zitatangazwa na wananchi wameshaliona hilo kwa sababu wameshaziona survey zinazofanyika, kwa kweli kazi ni nzuri na timu ya TARURA tuliyonayo ya Country Manager wa Mbeya Vijijini ni kijana mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba Mheshimiwa Jafo huyu kijana anachohitaji pale ni motisha, hana gari. Utatembelea vipi mtandao wa kilomita zaidi ya 1,000 wakati huna usafiri? Vilevile ukiangalia hii kazi iliyoko mbele yake kilomita 163 ata-supervise namna gani akiwa hana usafiri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na barabara hizo, tunaomba vilevile wenzetu wa TANROAD kuna barabara ya mchepuko ambayo inaingiliana na hizi barabara waweze kuimalizia. Kwa hiyo, itategemea ni kiasi gani watafanya haraka kuijenga ile barabara ya kuanzia Mlima Nyoka kuja mpaka Songwe ili ziende pamoja kwa vile kiuchumi hizi barabara ni muhimu sana na ndiyo zitatuongezea mileage sana kwa ajili ya ushindani na nchi jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizi barabara naomba waangalie ni namna gani wataipandisha hadhi barabara ya kuanzia Mbalizi kwenda Shigamba mpaka Isongole. Hii barabara Mheshimiwa Mbena asubuhi alipiga magoti, ni barabara muhimu sana kiuchumi kwa vile hizi barabara ndiyo zinakuja kutuunganisha sisi Tanzania na majirani zetu wa Zambia. Kwa hiyo, tumeomba hizi kilomita 96 za hii barabara, wenzetu wa TANROAD wafanye mchakato wazipe bajeti za upendeleo kabisa ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizi barabara, Mbeya sisi pale tuko kimkakati, biashara ya bandari inategemea zaidi nchi za Zambia, Congo, Malawi na kwa kiasi fulani Zimbabwe. Bila kuboresha TAZARA na bila kuwa na bandari kavu pale Mbeya biashara yetu ya bandari hasa kwa nchi za nje kwa kweli itapata mtikisiko sana. Nilizungumzia juzi ni namna gani wenzetu Msumbiji wamejiandaa kuchukua soko hilo, wameshaanza ujenzi tayari wa reli na wanaboresha bandari yao ya Nakao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya haraka na wenzetu wa Wizara ya Miundombinu wasipochukua uamuzi wa haraka kwa sababu eneo limeshatolewa, wananchi wameshatangaziwa bila kujenga bandari kavu pale soko lote kwa ajili ya hizo nchi litachukuliwa na wenzetu wa Msumbiji. Pamoja na hilo, naiomba Serikali iangalie namna gani itajenga reli ya kuanzia Mbeya mpaka Ziwa Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri ni suala zima la maji. Nililalamika sana hapa kuhusu miradi ya maji lakini leo hii kwa ajili ya ubunifu wake tulikuwa tunadanganywa kuwa hela hazitoki lakini amekuja kutuambia Waziri wa Maji kuwa pesa zipo na leo natoa ushuhuda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)