Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kumshukuru Mwenyezi Mungu kunipa nafasi ya kuchangia katika Bunge lako Tukufu, lakini nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Jafo pamoja na wasaidizi wake. Mheshimiwa Jafo anafanya kazi kubwa mno na sijui kama familia yake anakaa nayo saa ngapi kwa sababu kila wakati tunamwona kwenye vyombo vya habari akiwa kwenye shughuli za Kitaifa. Nawaomba Wabunge wenzangu tuwaombee Mungu hawa Mawaziri kwa sababu wanatumia vyombo vilivyotengenezwa kwa mikono ya wanadamu. Wakati wowote wanaweza wakapata hatari za barabarani na tulishuhudia juzi juzi tu Mheshimiwa Kakunda alipata ajali mbaya, tunamshukuru Mungu kwamba hakuumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuuliza swali moja ambalo limenisumbua, nimesikia baadhi ya Wabunge wa upande wa Upinzani wakisema kwamba hawaruhusiwi kufanya mikutano. Mimi ninavyojua ni kwamba kila Mbunge anaruhusiwa kufanya mkutano katika jimbo lake. Sasa sijui pengine tuje tupate ufafanuzi kwamba ni mikutano ipi wanayoilalamikia kwa sababu hata sisi tunaruhusiwa kufanya mikutano katika maeneo yetu. Kama wewe siyo Mbunge wa Dodoma Mjini unataka uje ufanye mkutano katika Jimbo la Dodoma Mjini unataka nini Dodoma Mjini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachokijua ni kwamba Mbunge anaruhusiwa kufanya mikutano kwenye eneo lake. Kama lipo jambo lingine Mheshimiwa Waziri naomba Serikali ije itoe ufafanuzi, lakini ndivyo ninavyojua. Pengine lisiwe kwa ajili ya kuwapotosha wananchi kwamba wamekatazwa kufanya mikutano iwe dhahiri kwamba Mbunge yeyote anaruhusiwa kufanya mkutano katika eneo lake la kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, neno la Mungu linasema aombaye hupewa, atafutaje huona na abishaye hufunguliwa. Sisi watu wa Dodoma tumeomba sana, tuliomba sana Serikali ihamie Dodoma na namshukuru Mheshimiwa Rais na Serikali yake ya Awamu ya Tano ametimiza lengo lile, yale maombi yetu tuliyoomba siku nyingi ameyatimiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi mvua za masika zikinyesha watu wanaotoka Kilosa kwa njia ya reli kuja Dodoma wanaweza wakalala wiki nzima njiani hawajafika Dodoma kwa sababu ya mafuriko. Sasa hivi reli inatengenezwa Standard Gauge kitu ambacho sisi Watanzania hatukutegemea kwamba tungepata kwa muda mfupi hivi. Naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi wa kujenga standard gauge tena kwa fedha zetu za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani ukitaka kuja Dodoma lazima ukodi ndege yako au ndege za kukodi, sasa hivi Air Tanzania inakuja Dodoma mara tatu kwa wiki, hatukulitegemea kwa haraka hivyo. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa mafanikio tunayoyapata Mkoa wa Dodoma. Sasa hivi mikutano mikubwa inafanyika Dodoma na hivi sasa tuna Bunge la Afrika Mashariki hapa hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata Maafisa Mipango Miji wazuri na naamini Mji wa Dodoma utakuwa mji mzuri katika Afrika nzuri kama tutafuata utaratibu na ujenzi ambao tunaelekezwa na maafisa wetu ambao tumepata kutoka kwa Mheshimiwa Lukuvi. Kitu ambacho nakiomba ni kwamba kama kuna changamoto zozote kwa mfano ulipaji wa fidia kwa wananchi uende kwa wakati ili wananchi wapishe na makao makuu yaendelezwe kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kitu kimoja pia kwa Serikali yetu sikivu, Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali imeamua Makao Makuu yaje Dodoma, lakini bila sheria itakayoweka msingi kwamba Makao Makuu ya nchi hii ni Dodoma itaweza kuwa shida baadaye. Sijui mbele ya safari baada ya Mheshimiwa Magufuli kumaliza muda wake, atakayekuja simjui, lakini anaweza kuja mtu ambaye hapapendi Dodoma, kama hakuna sheria inayotamka kwamba Dodoma ni Makao Makuu kunaweza kukatokea mtafaruku mbele ya safari. Kwa hiyo, niiombe Serikali kwamba walete basi Muswada wa Sheria hapa Bungeni na tuufanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ujio wa watu au ujio wa Makao Makuu nimeanza kuona changamoto kama upungufu wa maji, hasa maeneo ya UDOM kule, maji hayatoshi na kule kuna wanafunzi wengi wanaosoma kule. Niombe DUWASA wapate fedha za kutosha kwa ajili ya maji ili wageni wanaokuja basi wasiwazie tena Dar-es-Salaam wajue kwamba wamekuja mkoa wa asali na maziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkoa wetu kabla ya ugeni huu haujaja tulikuwa na mahitaji ya Walimu wa sayansi 373, waliopo ni 258. Niiombe Serikali watuletee Walimu wa sayansi. Tuna maboma 116, tuna mahitaji ya maabara 116, yaliyopo ni 11 tu. Niiombe Serikali kukamilisha maboma ya maabara yaliyopo ili wanafunzi wapate elimu kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali kwa kukarabati na kujenga Kituo cha Afya Makole. Kituo kile kinahudumia zaidi ya wagonjwa 300, wauguzi hawatoshi, waganga hawatoshi, naomba tufikiriwe katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile jengo la Halmashauri ya Chamwino lina zaidi ya miaka 10 halijakamilika. Sasa hivi tunajitahidi kukamilisha ground floor lakini haitawatosha wafanyakazi wa Halmashauri ya Chamwino. Naomba fedha zitolewe kwa ajili ya kukamilisha jengo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Chemba wanaomba magari mawili tu ili yawasaidie kutoa huduma ya afya na elimu kwa sababu magari waliyonayo ni machakavu. Mkitusaidia katika hilo tutashukuru sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.