Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Bajeti ya Ofisi ya Rais katika Wizara hizi mbili kama zilivyotajwa. Nataka niende moja kwa moja kwenye masuala makubwa yanayohusu eneo langu la utawala, nalo si lingine, ni Halmashauri ya Chalinze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha bajeti iliyopita, Serikali ikishirikiana na halmashauri imeweza kufanya mambo mengi makubwa, ikiwemo kusaidia kuimarisha maeneo ya afya, maeneo ya elimu na maendeleo ya vijiji vyetu kwa ujumla wake. Pamoja na jitihada hizo bado yapo mapengo ambayo leo hii ninaposimama hapa nataka nimkumbushe hasa Mheshimiwa Waziri Jafo; kwa sababu kwenye eneo huko la Ofisi ya Rais upande mwingine sina mengi; lakini eneo la TAMISEMI ndiko nina mengi mengi kidogo; nataka nimkumbushe juu ya mapengo machache ambayo naamini tukishirikiana kwa kasi ambayo ameendelea kufanya kazi, tutaweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na eneo la afya. Kwanza nianze kushukuru maana tunaelekezwa kwamba usiposhukuru kwa kidogo huwezi kushukuru kwa kikubwa. Katika kipindi cha bajeti iliyopita ndani ya Halmashauri yangu ya Chalinze nimeweza kuletewa zaidi ya shilingi milioni mia saba kwa ajili ya maendeleo ya afya. Katika shughuli hizo tumeweza kufanya mambo makubwa sana kwa mfano kwenye zahanati yetu kule Kibindu, mambo yanakwenda vizuri, naishukuru sana Serikali yangu. Vile vile pale Lugoba nako pia mambo ni mazuri sana na naendelea kuishukuru Serikali yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo, upande wa watumishi imekuwa sasa ni kizungumkuti kikubwa sana. Tumeweza kufanikiwa na kama tunavyoendelea kufanikiwa kujenga miundombinu mizuri lakini kuna upungufu wa Wauguzi na Wakunga imekuwa ni shida kubwa sana. Vifo vya akinamama na watoto vimeendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba kwa sasa hivi tumevipunguza sana, lakini kwa kweli kukosekana kwa watu hawa ambao ni viungo vizuri sana katika kutimiza eneo zima au lengo zima la Serikali kwa upande wa afya mambo yameendelea kuwa si mazuri sana. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama aseme neno kidogo ili watu wa Chalinze waweze kufurahi juu ya mikakati mizuri ambayo Serikali imepanga katika kuhakikisha kwamba anatupatia wauguzi na waganga ili mambo ya afya yaweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia mahitaji makubwa ya sasa ni mahitaji ya gari za kupakia wagonjwa. Kama anavyojua Mheshimiwa Waziri alipokuja kwa mara ya mwisho tulimwonesha tulikuwa na magari mengi lakini Mungu naye ana yake. Magari yetu mawili ambayo tulikuwa tunayategema yamepata ajali na sasa hivi imekuwa ni tabu kweli kweli, hasa inapofika wakati wa kuwasafirisha wagonjwa kutoka katika vituo vya afya kwenda katika hospitali kubwa za rufaa; kama ambavyo anazifahamu, kule Tumbi, Bagamoyo na nyingine ambazo zinakwenda Msoga pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika eneo la elimu kilio kinafanana kidogo na kilio cha afya. Jitihada kubwa tumeendelea kuzifanya katika kuhakikisha kwamba madarasa, tunaendelea kujenga nyumba za Walimu. Hata hivyo, ukweli ni kwamba upungufu wa Walimu pia umeendelea kutusumbua. Kwa mfano, kama anakumbuka vizuri katika ile zoezi letu la kukagua vyeti feki tumepata shida sana kwa sababu baadhi ya Walimu walionekana kupungukiwa na sifa na kuondolewa, lakini sasa hivi kwa jinsi ambavyo tunakwenda nina imani kabisa kwamba kama katika bajeti yake mzee atatuangalia vizuri, basi mambo kule nako yataendelea kuwa mazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ya bajeti sikumbuki ukurasa wa ngapi lakini upo ukurasa anaozungumzia mradi wa uendelezaji wa miji kimkakati. Katika eneo hili sihitaji kusema mengi sana. Geographical position ya Chalinze inajieleza, wala sihitaji kueleza kwamba kuna maji, kuna kitu gani. Sielewi wanapozungumzia mikakati ya uendelezaji wa miji kimkakati, maana hapa ni strategical development ambayo tunaizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji kama wa Chalinze ambao sasa hivi umeendelea kupanuka na idadi ya watu imeendelea kuwa kubwa, viwanda vimeendelea kushamiri na maendeleo ya mmoja mmoja yameendelea kuwa makubwa; mipango miji, mahitaji ya kijamii kuanzia kwenye upande wa mahitaji ya masoko, afya, elimu na miundombinu yameendelea kuwa ni mahitaji ya muhimu sana kwa mji ule. Hata hivyo, katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri niliposoma ametaja maeneo mengine lakini Chalinze sijaiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba tu kujua ni mkakati gani alionao Mheshimiwa Waziri katika miji kama hii ambayo kwangu mimi naona kama ndiyo sehemu ya kupumulia kwa Mji mkubwa kama wa Dar es Salaam kwa sasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo, lipo jambo ambalo pia limekuwa kizungumkuti na nafikiri kwa namna moja ama nyingine tumelizungumza sana katika vikao vya maendeleo ya Mkoa, hili jambo la TARURA. Ni kweli TARURA imeanza kufanya kazi na matunda katika baadhi ya maeneo tumeyaona. Hata hivyo, sisi ndani ya halmashauri ambako ndiko tunakoibua miradi ile mara nyingi tunapokuja kutekelezewa miradi ile na TARURA hatuoni ile tija ya yale ambayo tumeyakusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja; iko barabara inayotoka kwa Ruombo mpaka Kijiji kinachoitwa Kwa Mduma. Barabara hii umbali wake unakaribia kufika kilometa 12, lakini ilipopelekwa katika TARURA, ilipokamilika zilizokuwa zimetengenezwa ni kilometa nane tu. Sasa tunaomba tujue, hii mipango ya TARURA inakaakaa vipi? Wanajipangaje na je, ni lini tunaweza tukafikia malengo tajwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia tunatambua uchache wa fedha katika eneo hili. Kwa hiyo nafikiri siku nyingine tukikaa na TARURA wetu hawa, tukaenda kwa pamoja, tujadiliane nao juu ya vipaumbele ambavyo wananchi wanavitaka halafu wao watuambie. Sisi tunaposema barabara ya kutoka kwa Ruombo kwenda kwa Mduma maana yake tunaelewa umuhimu wa barabara ile. Sasa mtu akija akitengeneza barabara ile ya kilometa nane halafu yale malengo ambayo tunayakusudia sisi kama Halmashauri hayafikiwi nina uhakika kabisa hata malengo hayo ya Serikali Kuu pia hayatafikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo pia, niendelee kuipongeza Serikali kwa juhudi kubwa inayoendelea kufanya katika kuhakikisha kwamba tunahakikisha halmashauri zetu zinapata mapato ya kutosha. Mheshimiwa Waziri katika hatua hizi ningeomba sana tuendelee kuangalia vyanzo vipya tena, tuendelee kuhamasisha halmashauri zetu ziendelee kupata maendeleo katika kutatua au kuamsha vyanzo vilivyo vipya. Wameeleza waliotangulia hapa kwamba katika fedha ambazo zimepelekwa ndani ya Halmashauri zetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nakushukuru sana.