Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kupata nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mezani ya bajeti ya TAMISEMI pamoja na ya Utumishi na Utawala Bora. Nami niungane na wenzangu waliotangulia kuchangia kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wa TAMISEMI pamoja na Naibu Mawaziri wake, pia, Waziri wa Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala la uhaba wa watumishi katika sekta ya afya. Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, ina jumla ya zahanati 42, ina vituo vya afya viwili ambavyo vinahitaji watumishi wa kada mbalimbali wapatao 324. Waliopo hadi sasa hivi wanaohudumia katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ni 112 tu na kufanya upungufu wa watumishi 212. Kwa hiyo, niiombe Wizara iangalie ni namna gani ya kutupatia watumishi ili kuboresha utoaji wa huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Halmashauri yangu ya Wilaya ya Mbinga walikamilisha ujenzi wa vituo vinne kwa maana ya zahanati za kutolea huduma za afya na hivyo kufanya kuongeza uhaba wa watumishi katika Halmashauri yetu. Zoezi hili lilimlazimisha Mkurugenzi wa Halmashauri yetu ya Mbinga Vijijini kuwatoa watumishi ambao walikuwa wanahudumia kwenye vituo vya afya vinavyomilikiwa na Kanisa Katoliki ili waende kuhudumia hospitali hizi ambazo zimejengwa kwa nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili lilileta mvutano mkubwa sana na kuharibu mahusiano kati ya Jimbo letu la Mbinga, pamoja na uongozi wa Halmashauri. Tunaiomba Wizara ili kurudisha uhusiano huu angalau ituletee watumishi 22 ili zahanati hizi Nne ziweze kufunguliwa na kurudisha mahusiano ambayo yanaelekea kuharibika kati ya Jimbo letu Kuu la Mbinga pamoja na uongozi wa Halmashauri kutokana na mvutano wa hawa watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili lilishapelekwa ofisini kwa Katibu Mkuu wa Utumishi na nina imani atalifanyia kazi haraka iwezekanavyo ili zahanati hizi nne ziweze kufunguliwa na kutoa huduma zilizokusudiwa. Sambamba na upungufu huo wa watumishi wa Wizara ya Afya tunao upungufu wa watumishi wapatao 755 katika sekta ya elimu kwa ujumla wake. Kwa hiyo, tunaiomba pia, Wizara iangalie ni namna gani inaweza kutuletea watumishi katika sekta ya elimu kwa maana ya sekondari na msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu wamekuwa wakishukuru sana hapa kwamba, wamepatiwa fedha kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa vituo vya afya, lakini Mbinga Vijijini hatujaletewa chochote mpaka sasa hivi. Nina imani Waziri amepitiwa tu au amejisahau, naomba aangalie ni kwa jinsi gani ambavyo hata Mbinga Vijijini atatukumbuka ili na tuweze kuletewa fedha kwa ajili ya ujenzi, aidha upanuzi wa vituo vya afya katika Wilaya yetu ya Mbinga. Hususan tunaomba fedha kwa ajili ya upanuzi wa vituo vya afya vifuatavyo: Kituo cha Afya Matiri, Kituo cha Afya Mapera na Kituo cha Afya Kindimbachini, angalau nasi tuwe na vituo vitatu vya afya katika Halmashauri yenye Kata ishirini na tisa (29). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru pia Serikali kwa kuniletea fedha kwa ajili ya ukarabati wa sekondari kongwe ya Kigotera, ujenzi wa madarasa manne, ofisi mbili za walimu na vyoo 10 katika Shule ya Msingi Maguu. Niishukuru Serikali kwa kuniletea vyumba nane vya madarasa na vyoo 20 katika mtaa wangu ninaotoka wa Msingwa, Kata ya Msigani, Wilaya ya Ubungo ambako mimi ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa. Naishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo tunayo maombi maalum. Tunazo sekondari zetu tano ambazo ziko kwenye mpango wa kupandishwa hadhi kutoka kwenye sekondari za kawaida kwenda kwenye A – Level. Kwa hiyo, tunaomba Wizara ituangalie namna gani inaweza kutu- support katika kuzipandisha hadhi sekondari zifuatazo: Sekondari ya Hagati, Sekondari ya Mkumbi, Sekondari ya Mahilo, Sekondari ya Langiro na Sekondari ya Kiamili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitamalizia na suala la TARURA. Tunaipongeza Serikali kwa kuunda TARURA, ni imani yetu kubwa sana chombo hiki cha TARURA kinaenda kutatua matatizo yote ambayo tulikuwa tunakumbana nayo hasa Wabunge wa Majimbo ya Vijijini. Barabara zetu zilikuwa hazihudumiwi kwa kiwango ambacho ni cha kuridhisha kutokana na usimamizi ambao ulikuwa si mzuri kutoka kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyochangia Wabunge wenzangu, tumeona TARURA ina-cover kilometa laki moja na kidogo, bajeti yake bado ni finyu. Kwa hiyo,
naiomba Serikali ione uwezekano wa kutenga huu Mfuko wa Barabara, Road Fund asilimia 50 kwa 50 ili kuiwezesha TARURA iweze kufanya kazi zake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Meneja wa TARURA Mbinga. Nilipokuwa ziara mwezi wa 11 aliweza kunipa Mhandisi wake nikazunguka naye Jimbo zima ili kubainisha changamoto zilizoko kwenye upande wa usafiri. Pia, tulibaini kwamba, kuna barabara ambazo zinahitaji matengenezo ya haraka, nyingine zinahitaji kuwekezwa kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali kupitia Halmashauri yangu ya Wilaya ya Mbinga kwa maana ya TARURA, waangalie barabara itokayo Mapera kwenda Mikalanga, inaishia Ilela, barabara hii haijapitishwa grader tangu uhuru. Pia, waangalie njia ambayo inahudumia watu wengi na eneo ambalo linazalisha pia njia pacha kutoka Ngima hadi Ukiro pamoja na madaraja yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana niiombe Wizara kupitia TARURA Ubungo iiangalie Barabara inayotoka kwa Musuguri mpaka kwa Unju ambayo inaunganisha Ilala, pia barabara inayounganisha Maramba Mawili kuunganisha barabara inayotoka Mbezi kwenda Kinyerezi. Barabara hii inahudumia watu wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la ushauri. Barabara zetu zimepewa code number ambapo barabara hizi baada ya kupewa code number zinaingizwa kwenye mfumo wao wa dromas, nashauri kwamba TARURA waangalie uwezekano wa kuzi-grade hizi barabara kupewa namba kutokana na maeneo yetu ya utawala, kwa maana kwamba wafuate kama ni Kata, ifuate mtaa au kitongoji, ili wasimamiaji tuweze kufuatilia kwa rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukipewa network ya barabara kwa mfano ya Jimbo langu la Mbinga unaikuta barabara namba moja inatoka kwenye Kata nyingine, namba mbili inatoka kwenye Kata ambayo ni ya mbali sana.

Inatufanya ufuatiliaji wa hizi barabara kuwa mgumu. Kwa hiyo, nashauri TARURA wapange hizi codification kutokana na maeneo yetu ya utawala iwe rahisi kufuatilia kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo barabara moja kule Mbinga ambayo ilikuwa inajengwa kwa ufadhili wa EU, barabara hii ilikwama kutokana na changamoto walizopata za udongo. Barabara hii inatoka Longa inakwenda mpaka Litoho. Niliambiwa kwamba, barabara hii imechukuliwa na TARURA. Niiombe sasa Serikali itenge fedha za kutosha, ili barabara hii imalizike kipande cha kutoka Longa hadi Kipololo ambapo ndipo changamoto kubwa ilijitokeza, lakini pia, niiombe Serikali iunganishe kipande cha kutoka Mbinga Mjini hadi Longa.