Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia na mimi katika hotuba hizi mbili za Mawaziri hawa. Kwanza kabisa, namshukuru Mungu sana kwa ajili ya Tanzania, amani na utulivu uliopo. Namshukuru Mungu sana kwa Rais Dkt. Magufuli na Serikali yake nzima kwa ubunifu wanaoutumia katika kuhakikisha kuwa wanathubutu kuingia katika mikakati mikubwa ya kuiletea maendeleo Tanzania kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kumshukuru Rais Dkt. Magufuli kwanza kwa ahadi zake ambazo amekuwa akizitimiza kama sehemu ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Kipekee nataka kusema kuwa namshukuru Rais Dkt. Magufuli na Serikali yake kwa sababu kubwa sana kwa ajili ya Ileje. Nataka itambulike kuwa Ileje ni Wilaya Kongwe na imekuwa nyuma kwa miaka mingi sana. Sasa kwa miaka miwili na nusu Ileje inakua kwa kiasi ambacho watu hawawezi hata kuamini. Wale wanaoijua wilaya ile wanakubaliana nami. Mimi naomba kwa heshima na taadhima nipige magoti hapa. Magoti yangu ni mabovu, lakini naomba kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alikuja akatuahidi barabara ya lami ambayo imepiganiwa karibu miaka 40 na sasa inajengwa kwa kiwango cha lami. Nina kila sababu ya kushukuru kwa sababu miaka 42 unangojea barabara ya lami ya kwanza katika Wilaya, kwa nini nisishukuru? Hivi ninavyozungumza tumepata fedha ya kwenda kumalizia Hospitali ya Wilaya kubwa ya kisasa. Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja akaweka jiwe la msingi, alijionea mwenyewe jinsi ambavyo ile hospitali itakavyokuwa. Tulikuwa tunatibiwa Malawi, sasa watu watatibiwa Wilayani kwangu Ileje. Tumeenda kupata vituo vya afya viwili na magari yake ya wagonjwa. Hii ni Wilaya ambayo ilikuwa imesahauliwa, kwa nini nisiseme ahsante kwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi? Sasa hivi tunaenda kujengewa kituo cha forodha mpakani mwetu na Malawi na Zambia, hii vilevile ni juhudi ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ina mpaka mrefu sana karibu kilometa 108 na hizo hazina doria ya aina yoyote, hazina ulinzi wa aina yoyote. Wahamiaji haramu wengi wamekamatwa kule, wengine wamekufa kwenye mabonde yetu kule kwa sababu barabara zetu ni mbaya sana na wengine hawazijui wanapita usiku kutaka kuingia nchi za jirani wanakufa. Tunahitaji sasa gari ya doria, lakini ile barabara itakapojengwa Kituo cha Forodha nacho kikijengwa tuna uhakika Ileje itapanuka kiuchumi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuishukuru Serikali kwa miradi mikubwa ya maji inayojengwa Ileje. Ileje tunakunywa maji ya matope. Tuna vyanzo vingi vya maji, tuna mvua nyingi, lakini miradi ya maji ilikuwa hakuna. Sasa hivi tuna miradi mingi ya maji, mmoja mkubwa sana unajengwa pale Isongole, utakaokidhi haja ya shida ya maji yote ya maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru vilevile kuwa sasa hivi TARURA wameweza kwa kiasi kikubwa kumudu barabara zetu za milimani ambazo zilikuwa hazipitiki kipindi chote cha mvua. Kipindi hiki japo kidogo watu wanaweza kuwasiliana. Hizi zote ni pongezi na shukrani kwa watu wa Ileje kwa ajili ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi, imeweza kututazama na sisi kwa jicho special. (Makofi)

Vilevile nataka kuishukuru Serikali kwa sababu tunaenda sasa hivi kujengewa barabara zinazounganisha vijiji kwa vijiji, kata kwa kata kwa kutumia TARURA. Ilikuwa unatoka kijiji kimoja inabidi upite kata nyingine kurudi kwenye kijiji cha Kata yako. Huo ulikuwa ni usumbufu mkubwa na kwa jiografia ya kwetu, hiyo ilikuwa ni adha kubwa lakini Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaenda kutujengea. Ninachotaka kuomba sasa, tunaomba kwa haraka sana tupatiwe gari ya doria kutokana na kwamba sasa hivi uhalifu wa mpakani umeongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa vilevile tusaidiwe kuongezewa pesa TARURA; barabara zetu sisi na jiografia zetu ni ngumu mno; na kwa kuwa ni Wilaya ya pembezoni na ina changamoto nyingi, basi tuangaliwe kwa jicho la huruma zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru vilevile kwa REA. Ileje ilikuwa ni Wilaya iko gizani lakini REA sasa hivi imefunguka. Leo hii unasikia watu wa Ileje wanalalamika mbona leo umeme umekatika? Tulikuwa zamani hatuzungumzii mambo ya umeme, kwa sababu hatukuwa nao. Naishukuru sana Serikali kwa juhudi zao. Naomba hili zoezi la densification kwa ajili ya kuhakikisha miradi ya REA II inakamilika lifanyike haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna upungufu mkubwa wa watumishi; na yote hii inachangiwa vile vile na jiografia yetu. Wengi hawapendi kuwa kule, wengine wakija wanatoroka. Tuna upungufu wa watumishi kwenye sekta ya elimu na afya zaidi ya 580. Tunaomba sana zoezi la kuajiri litakapoanza basi na sisi watufikirie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna tatizo kubwa Kiwira. Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira uko Ileje na nasikitika kwa miaka yote uliokuwa ukifanya kazi Ileje haijafaidika kwa sababu, kwanza ulikuwa unahesabiwa kwamba ni wa Kyela. Mradi ule sasa hivi unatambulika kuwa ni wa kwetu na tunaambiwa kuwa, STAMICO wameuchukua na wameshaanza majaribio ya kuchimba makaa ya mawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kujua sasa mustakabali wake ni upi maana hatujasikia Mkandarasi aliyepatikana ni nani na atauendesha vipi. Tunaambiwa bado kuna mambo ya kupata ile hati ya kukabidhiwa, haijakabidhiwa na yule aliyekuwa mwekezaji wa huko nyuma. Tunaomba hili lifanyike haraka ili wananchi wetu wapate ajira na ule mgodi utuletee faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna daraja pale ambalo limeharibika la kilometa saba ambalo ndiyo linaunganisha Kiwira na Ileje. Sasa hivi inabidi unataka kwenda Kiwira uzungukie Kyela kutokea Kiwira mgodini, hiyo siyo hesabu nzuri kiuchumi. Tunaomba sana hili daraja la kilometa Saba tu lijengwe, ili sasa Ileje na mgodi wake wa Kiwira viunganishwe moja kwa moja kwa mawasiliano.