Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Engineer Masauni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni ngumu na nzito kama ilivyo Wizara ya Ulinzi. Unapozungumzia Polisi na unapozungumzia Jeshi unazungumzia coercive instruments of the State. Hiyo fact, ni lazima tuifahamu, we are dealing with coercive instruments of the State and which are indispensable.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ukiisoma Biblia hasa Agano la Kale na hasa Zaburi, Wanajeshi na Walinzi wamependelewa sana na Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuwauliza wataalamu wa maandiko, kwa nini inazungumziwa Mungu wa Majeshi, Majeshi, Majeshi? Wakasema hata huko kulikuwa na vurugu na ndiyo maana ulinzi uliwekwa ndani na nje na ibilisi alipoasi akatupwa huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, daima watu ambao kazi yao ni ulinzi wa milki iwe ni ulinzi wa ndani wa milki au ulinzi wa nje wa milki, lazima watumie nguvu wakati mwingine inapolazimika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ni lazima wafanye hayo ndani ya mujibu wa sheria. Pia ni lazima wote tufahamu these are coercive instruments of the State. Wengi hapa mmesoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na vyuo vingine, mmesoma Development Studies (DS 100), hayo ndiyo mliyofundishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vyombo ambavyo ni coercive instruments of the State ni lazima uviendee kwa namna inayostahili. Ukienda kinyume, vitachukua hatua kwa sababu ya kulinda Katiba. Zaidi hivyo ndiyo vyombo pekee vinavyoapa hata kufa ili kulinda nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumeapa kuiheshimu Katiba, lakini wao pamoja na kuapa kuiheshimu Katiba, wamekwenda mbali zaidi, ndiyo peke yao wanaoapa katika viapo vyao, kuna kufa kwa niaba ya nchi. Ila hiyo haina maana wafanye mambo kiholela, lakini daima tujue, nasi tumepata bahati, tumepita katika kipindi kigumu mwaka jana. Watanzania tunasahau haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingine za Ulaya nami nimekuwa na bahati, nimekaa miaka michache Ulaya, miaka 10 michache sana, lakini katika vipindi vigumu. Walifika zile nchi zilitangaza hata state of emergency. Mamlaka hayo Rais anayo ya kutangaza hali ya hatari chini ya Ibara ya 32 kwa eneo lenye matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kuchukua hatua ya kudhibiti hali ya Kibiti na Rufiji, hatukufika mahali Rais wa Jamhuri ya Muungano kutangaza hali ya hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Italia, Ujerumani na Uingereza, walipopitia katika hali hii na sitaki kuitaja nchi, Askari wao walipewa haki ya ku-shoot on site, sisi hatukufika hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tuvipongeze vyombo hivi kwa ku-contain hali ngumu lakini bila kulifikisha Taifa ama Rais kutumia mamlaka yake ya Ibara ya 32 ya kutangaza hali ya hatari kwa eneo la Rufiji, Ikwiriri au kufika kutoa amri ambayo ingekuwa na madhara. Tuwapongeze, tuwape nguvu. Kwa kufanya hivyo, wamekufa. Polisi wamekufa; cold blood on behalf of the United Republic of Tanzania. Mimi na ninyi hatukuapa kufa.

Wao wameapa kufa. Watu walioapa kufa kwa niaba yenu muwastahi, lakini zaidi muwaombee Mwenyezi Mungu kwa sababu ndio peke yao wamechukua dhamana hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio watu wa kuwabagaza, kuwazoza, kuwakejeli, kuwadharau na kuwadhihaki. Mtakatifu Agustino wa Hippo aliwaonya watu wa Carthage walipoanza kuwa na majivuno, akasema siku wanaosafisha mitaro watakapoacha kusafisha mitaro ndipo watu mtakapojua umuhimu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimesimama ili kutoa maelezo ya mambo mawili ambayo yameelekezwa kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo nadhani yanaangukia katika Sekta ya Sheria. Haya ni yale yanayohusu kesi ya Mashehe wa Uamusho wa Zanzibar na suala la Akwilini. Mambo haya yote mawili hayaihusu Wizara ya Mambo ya Ndani. Mambo yote haya mawili yanamhusu Mkurugenzi wa Mashtaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda Watanzania wote tuelewe, Mkurugenzi wa Mashtaka ameanzishwa kwa mujibu wa Katiba, Ibara ya 59B ambayo inaeleza wazi kabisa kwamba:

“kutakuwa na Mkurugenzi wa Mashtaka ambaye atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizoainishwa katika Ibara ndogo ya (2) na Ibara ya 59 na amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka 10. Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa na uwezo wa kufungua, kuendesha na kusimamia mashtaka yote nchini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwasomee Ibara ya (4):-

“Katika kutekeleza mamlaka yake Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa huru, hataingiliwa na mtu yeyote au mamlaka yoyote na atazingatia mambo yafuatayo:-

(a) Nia ya kutenda haki;
(b) Kuzuia matumizi mabaya ya taratibu za utoaji haki;
na
(c) maslahi ya Umma.”

Ibara hiyo hiyo unaikuta katika Katiba ya Zanzibar, Ibara ya 56A ambayo inaeleza wazi kabisa, hakuna anayeruhusiwa kumwingilia DPP hata Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata Zanzibar Ibara ya 56A inatamka wazi na niende kifungu cha nane (8) na chenyewe kiko very clear, “Hakuna mtu anayeruhusiwa kumwingilia Mkurugenzi wa Mashtaka.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Bunge hili hili lilipitisha Sheria Na. 27 ya mwaka 2008, The National Prosecution Services Act.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Ibara ya 19 ya kifungu hicho iko wazi kabisa. Mkurugenzi wa Mashtaka ana- enjoy security of tenure kama anavyo-enjoy Jaji wa High Court na ndiyo maana Rais hawezi kumwondoa DPP akishamteua. Ili amwondoe DPP na akidhani amefanya makosa au amekwenda kinyume, ni lazima amuundie Tribunal; na tribunal hiyo ni lazima iwe na Majaji watatu na mmoja awe wa Court of Appeal.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, aliondolewa na kupandishwa cheo kile kile cha Security of Tenure, huwezi kumshusha chini. Sifa yake ni kama ya High Court Judge, ndiyo maana huwezi kumtoa DPP kumpeleka chini. Ndiyo, hawezi na pale hakuondolewa, amepandishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkurugenzi wa Mashtaka ana uhuru kamili wa kufungua mashtaka na kuyafuta, ndiyo maana katika haya mambo mawili ambayo nataka kuyazungumza na kwa sababu Mkurugenzi wa Mashtaka hawezi kuingia Bungeni nimemwomba leo anipe maelezo ili nilieleze Bunge hatua anazozichukua kuhusu suala la Mashehe wa Uamsho na suala la Akwilini, yeye hawezi kuja hapa. Alikuwa Singida nimemwomba aje leo Dodoma ili atoe maelezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mashehe wa Uamsho wa Zanzibar ni suala nyeti sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. Kwa hiyo, jambo hili nataka niwaambie Watanzania kwamba Serikali inatambua uwepo wa kesi hii na kuwa imechukua muda mrefu Mahakamani. Kwa hiyo, ni nia ya dhati ya Serikali kuona kuwa kesi hii inafikia mwisho. Hata hivyo ucheleweshwaji wake unasababishwa na mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme ni bahati mbaya sana watu tunaowajadili sasa wana heshima na hadhi ya Mashehe, lakini hawakuingizwa kwa sababu ya heshima ya hadhi ya Ushehe, ni kwa sababu kuna tuhuma za ugaidi. Tuhuma hizi ni lazima zipelelezwe. Kesho na keshokutwa akitokea mwanasiasa au nani ameshutumiwa, lazima yafanyiwe uchunguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu adhabu yake ni kubwa na ndiyo maana Mashtaka ya Mauaji na mashtaka ya aina hii upelelezi wake unachukua muda mrefu ili mjiridhishe kabisa, mnapowapeleka Mahakamani kweli uko ushahidi unaotosha. Kwa sababu baada ya hapo wakitiwa hatiani adhabu yake ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kesi hii upelelezi pia umefanyika nje ya nchi ambapo tumeomba baadhi ya taarifa na vielelezo ili viletwe visaidie katika kesi hiyo. Ndiyo maana Mwendesha Mashtaka kupitia ofisi yangu ambayo ndiyo ina mamlaka ya kusaini hizo documents za kuomba nchi nyingine zitusaidie kuleta ushahidi, kazi hiyo imekuwa inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka inachukua hatua za kuharakisha upelelezi huo ili ukamilike mapema iwezekanavyo. Ndiyo maana nimesema hivi leo DPP alikuwa Singida nimemwita ili nipate maelezo haya ya kuliarifu Bunge lako. Naamini mambo haya yakikamilika, basi hatua za kisheria zitachukuliwa.