Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kazi kubwa na nzuri ya kulinda na kudumisha amani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba na Waandamizi wake kwa hotuba nzuri ya kiwango na kwa kazi nzuri wanayoifanya. Baada ya pongezi, naomba sasa nichangie hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kuhoji yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hati za dharura za safari, naomba Mheshimiwa Waziri anifafanulie kwa nini hati za dharura za safari kwa sasa zinatolewa kwa single journey badala ya multiple trips kwa muda wa mwaka mmoja kama zamani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wengi wa wasafiri wanaokwenda nchi za jirani hususani Kenya kwa upande wa mpaka wa Namanga Wilayani Longido ni Watanzania maskini na wajasiliamali. Je, Serikali haioni inawakandamiza na kuwasababishia usumbufu usio wa lazima wananchi ambao watahitaji kufanya safari kadhaa kwenda na kurudi nchi ya jirani ndani ya muda mfupi au mara kwa mara, kwa mfano wanaokwenda kwenye masoko ya County ya Kajiado na Nairobi kila wiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali ilivyo sasa hivi kwa wananchi wenye haja ya kwenda Kenya angalau mara moja kila wiki na ambao ni maskini tu wasio na pesa kubwa wanalazimika kuomba mpya kila wiki na wanalazimika kuwasilisha upya viambatisho lukuki (Vyeti vya kuzaliwa vya Mwombaji na wazazi, vitambulisho na kadhalika) ambavyo mara nyingi hawana na hasa kwa jamii yetu ya Kimasai ambao wengi hawana vyeti vya kuzaliwa. Utaratibu wa sasa unaleta adha kubwa kwa wasafiri maskini na hivyo naomba Serikali irejeshe Multiple Trips Travel Documents.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa kutoa hati za dharura za safari mpakani. Naomba kuishauri Serikali iboreshe mazingira ya wananchi wanaohitaji kusafiri nchi za jirani kwa kutumia hati za dharura waweze kupewa pale mipakani tofauti na sasa ambapo wanalazimika kusafiri kwenda Makao Makuu ya Wilaya kupata Hati hizo ambazo uhai wake ni kwa safari moja hata kama atahitajika kurudi mara kadhaa ndani ya wiki moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kurahisisha upatikanaji wa Pasi za Afrika Mashariki; kwa kuwa hati za dharura za safari ina adha kubwa na gharama kwa wasafiri wanaohitaji kusafiri na kurudi ndani ya muda mfupi, watengenezewe mazingira ya kuweza kupata pasi za Afrika Mashariki zenye uhai wa muda mrefu palepale mpakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ilivyo kwa sasa upatikanaji wa pasi Afrika Mashariki ni mgumu kwani ni mpaka upeleke maombi Makao Makuu ya nchi na inachukua muda mrefu kabla ya kutoka. Kwa kuwa, Wilaya ya Longido ni ya mpakani na kuna haja ya kuiwekea ulinzi wa kutosha, naomba Serikali itujengee angalau kituo kimoja cha Polisi katika kila Tarafa hasa zile zinazopatikana Kenya ikiwemo Tarafa ya Katumbeine na Engarenaibor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Wilaya ya Longido ina vituo vitatu vya Polisi kimoja mpakani Namanga, kimoja Mjini Longido na Kata ya Kamwanga. Kwa uhaba uliopo wa vituo vya usalama wa raia, katika Tarafa ya Ketumbeine, karibu kila mwaka majambazi huteka watu na kuwapora mali. Hivyo, kuna haja kubwa ya kujenga kituo cha Polisi katika Tarafa hiyo hasa Kata ya Mairugoi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.