Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya usalama nchini. Pamoja na Mheshimiwa Waziri kutoa tamko kwamba watu wawe mbele ya matokeo kabla hayajatokea kwamba yaweza kudhibitiwa, kauli hii ilikuwa ni wimbo tu kwa sababu Mhariri Mchambuzi wa Gazeti la Mwananchi alitoa taarifa kwamba, maisha yake yako hatarini anatafutwa na watu wasiojulikana. Leo Msemaji Mkuu wa Serikali anasema ni usanii na upuuzi mtupu, matokeo yake Mtanzania huyu amekimbilia nchi ya Finland kuomba hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Waziri anasema, miili ya watu inayookotwa inaelea majini ni ya wahamiaji haramu, leo mwili wa tajiri wa mabasi anayemiliki Kampuni ya Mabasi ya Super Sami umeokotwa kwenye kiroba na wavuvi unaelea kwenye Mto Ndabaka, Wilayani. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuwa kauli yake haina mashiko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya chaguzi nchini; wakati Mheshimiwa Waziri anasema Serikali haiwezi kuvumilia kuona wananchi wake wanaumizana kutokana na matokeo ya uchaguzi kisha Serikali ikae kimya bila kuchukua maamuzi yoyote, leo wanachama kadhaa wa upinzani wamepigwa, wameumizwa na wengine kuuawa. Je, mbona Serikali imeshindwa kuchukua hatua yoyote juu ya wahalifu waliohusika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Waziri anaposema kuwa ni aibu kwa nchi yenye vyama vingi vya siasa wananchi wake kufanyiana fujo, lakini kwa upande mwingine Serikali ya CCM, vyombo vya dola na taasisi za Serikali bila aibu zinashiriki kikamilifu katika kukivuruga Chama cha CUF. Je, kwa nini Jeshi la Polisi haliheshimu sheria na taratibu za vyama vya siasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alitoa tamko la kuwa, watu waache tabia ya kuunganisha matukio na imani ya dini, siasa au chama. Matokeo yanayotokea Zanzibar kabla, wakati na baada ya chaguzi mbalimbali huwa Serikali na vyombo vya dola vinayahusisha matokeo hayo kuwa, yametekelezwa na wafuasi wa Chama cha CUF, bila kufanyiwa uchunguzi, jambo ambalo husababisha wafuasi wa CUF kupigwa na kuumizwa bila hatia yoyote. Mheshimiwa Waziri tunaomba tabia hii ikomeshwe mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.