Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza niipongeze Serikali kwa kazi kubwa inayofanya. Pia nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote Serikalini kwa kazi kubwa wanayofanya. La kwanza nizungumzie kwamba katika Wizara ambazo zina changamoto lukuki katika nchi hii ni Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Wabunge wenzangu wote wamezungumza suala la miundombinu ya majengo kwenye makazi ya askari, maofisi na hata magereza na vituo vya polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mwaka wa tatu sasa, changamoto ya Wizara hii haiwezi kutatuliwa kwa jinsi tunavyokwenda, hali ni ngumu sana, fedha ni kidogo. Tulifanya ziara Mtwara na Lindi tukakuta viporo vya miradi ambayo hata kwenye kitabu cha bajeti baadhi yake haikuwekwa. Sasa Waziri tungependa atuambie ile miradi tuliyotembelea japo yeye hakuja ni kwa namna gani Serikali sasa inatatua changamoto ya hizi Wizara kwenye miundombinu ya majengo yale kwa sababu tumeshawekeza na sasa hakuna utekelezaji wa ukamilishaji wa hiyo miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais kwa hela aliyotoa kwa ajili ya Makao Makuu Dodoma lakini fedha zile hazitasaidia kwenye miradi ambayo tumekagua. Wizara hii Jeshi la Zimamoto, Polisi na Magereza magari yake ni mabovu sana na hasa kwangu kule Mbulu, hayana matairi, hayana muda wa matumizi, muda wa matumizi wa hayo magari umeshakwisha. Kwa hiyo, Waziri aje atuambie ni kwa namna gani angalau tunakombolewa kwenye tatizo kama hili la ubovu wa magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba matumizi ya magari ya Serikali ni miaka mitano. Kwa hiyo, inapokuwa zaidi ya miaka mitano yale magari yanakuwa hayana tena hadhi ya matumizi katika utendaji wa Serikali na hasa askari. Magari ya askari ni magari yanayotakiwa yawe mapya, watakapoitwa mwendo wao ni wa kasi, wanakimbia, kuna roho za watu juu ya yale magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa yanapokaa muda mrefu na yamechakaa, kule kwangu Wilaya Mbulu, magari yote matatu, majimbo yote mawili yamechakaa. Nimeomba miaka mitatu sasa na leo tunapitisha bajeti hakuna gari, lakini kwenye makazi, ni mahali gani tutakwenda, kule Mbulu tukienda Magereza haifai, imejengwa toka ukoloni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Polisi Wilaya hakifai, kimechakaa, majengo mengine yale ya makazi ya askari hayafai, wangeenda waandishi wa habari tungejificha. Nafikiri hata hayo yanayojengwa anzeni na Makao Makuu ya Maafisa wa majeshi yetu yaliyo chini ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waende kwenye ngazi ya mikoa kujenga nyumba za Makamishna wa Mikoa, waende kwenye ngazi za Wilaya tupeleke tuanze kwenye ngazi za Wilaya tupeleke tuanze kwenye ngazi za maafisa ili hata wale askari wa kawaida wakipangisha, basi na yale majengo yafanane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Askari ni utii, askari ni uhodari, askari ni uaminifu wanatupigia saluti, wanampigia Waziri saluti, mtu yoyote saluti mwenye mamlaka kwake, siku moja na sisi huko tunakokwenda kwa Mwenyezi Mungu wao watapewa ufalme huo, tutawapigia wao saluti. Nadhani mambo haya sio mambo ya mchezo wakati fulani tunapoyaongea, yanahitaji sana kuangaliwa na kwa namna gani tunatatua basi hata kwa awamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia kuna askari wachache wanaochafua majeshi yetu ziara ya viongozi Waziri, Inspekta Generali, RPC akutane na baadhi ya viongozi na baadhi ya wanajamii na viongozi wa madhehebu ili masikio yake pia yapate kusikia eneo hili kuna matatizo gani, kukagua tu askari na kupita hakusaidii kuona sikio lako, kisogo chako kina kitu gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, kuna Wabunge wameongea mambo hapa, kama hayana ukweli wafute zile kauli. Mfano, Mheshimiwa Zitto anazungumza watu 68 wameuawa, watu mia tatu na kitu hawaonekani, aisaidie Serikali upelelezi kwa sababu sisi tunazungumza kwa niaba ya Watanzania, mambo haya yanapotosha umma . (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumza ni kwamba, wakati huu ambapo tunaelekea kwenye kupitisha bajeti, mambo ni mengi, lakini tuyaweke kwenye vipaumbele, kuna baadhi ya mambo tumetembea sisi na Mheshimiwa Waziri, tumetembelea Wizara hii, tumeona mambo mengi sana, tumeona miradi viporo, tumeona hakuna namna ya utatuzi, basi tutafute njia mbadala ili tuweze kukamilisha hiyo miradi ambayo tulitarajia kwa namna ya pekee sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee nalipongeza Jeshi la Polisi kwa sababu kazi hii wanayofanya sio rahisi. Kama tunavyozungumza sisi ni kazi ngumu sana, unapolala yeye anakulinda na mali yako, unapoamka yeye anaendelea kukulinda, lakini mazingira yao hayafanani na kazi wanayofanya. Kwa hiyo, nadhani hatujawatendea haki askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umenipa dakika tano, ni ya kuishukuru Serikali, mimi nilitaka dakika 20 za kuizungumzia Wizara hii na kwa namna ya pekee nimwambie hatuwatendei haki askari. Mheshimiwa Mwigulu, yeye kama Waziri, ajitazame, atafakari maneno tunayoyazungumza hapa. Mengine yeye ni mtu mzima, aende kuyachambua kuna mambo ambayo yana ukweli kabisa na yafanyiwe kazi na yeye kama kiranja wa Wizara hii kwa nafasi yake anapaswa kuangalia Watanzania wanasema nini. Mengine yanasababishwa na askari kutokana na mazingira ya kazi yao. Kazi inapokuwa ngumu, mazingira yanapokuwa si rafiki, lazima mtu anashawishika kwenda kufanya mambo mengine ambayo hayana maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi, naomba watuangalie kwenye ngazi za wilaya, mikoa, na ngazi za Taifa ili tuweze kufanya kazi hii kwa weledi na askari wawe na amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.