Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, muweza wa mambo yote. Pili shukrani zije kwako Mheshimiwa Naibu Spika kwa umahiri wa kazi yako.
Nikianza kwa kuchangia Wizara hii, naanza na suala zima la kilimo. Kilimo kama usemi ulivyozoeleka kuwa ni uti wa mgongo, maana yake ni kwamba kilimo ndiyo kila kitu, ni shughuli inayotoa ajira kubwa nchini kuliko sekta nyingine yoyote, yaani kilimo kimeajiri zaidi ya asilimia sabini . Changamoto iliyo ndani ya sekta ya kilimo ni kutokana na kutegemea mvua za msimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, dunia haisimami, ni lazima na sisi twende na wakati, naishauri Serikali tuondokane na kilimo cha kutegemea mvua za msimu peke yake, umekuwa ni wimbo wa siku nyingi juu ya suala la kilimo cha umwagiliaji lakini sijui tunakwama wapi? Naishauri Serikali kufanya utafiti wa hali ya juu kuona kwamba tunakwamuka na suala la umwagiliaji linachukuliwa nafasi na kuondokana na utegemezi wa mvua za msimu pekee.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la umwagiliaji, naishauri Serikali tujikite zaidi kwenye uvunaji wa maji ya mvua. Tazama tunasifika kuwa wamwagiliaji wazuri wa bahari, maana yake maji yote ya mvua tunayaruhusu kutiririka na kuingia baharini bila faida yoyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kwa kutumia miundombinu mbalimbali kuweza kujenga mabwawa takribani nchi nzima ili kuweza kuhifadhi kiasi kikubwa cha maji ya mvua ili kufanikisha kilimo cha umwagiliaji kwa ufanisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mabwawa tukiweza kuyaimarisha yanaweza kutuimarishia ajira nyingi hasa kwenye kilimo cha mbogamboga kwa maeneo kama yenye uhaba wa mvua. Aidha, yatatupunguzia migogoro kwa kiasi kikubwa kati ya wafugaji na wakulima kwa upatikanaji wa maji, pia wafugaji watanufaika sana katika kukidhi mahitaji ya wanyama wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, faida yenyewe ya uwepo wa mabwawa, watu watapewa kujitengenezea ajira kwa ufugaji wa samaki ambao samaki hao ni hitaji kubwa kwa chakula cha binadamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, maji ya mvua ni neema kubwa kwetu kutoka kwa Mungu iwapo tutaweza kuyavuna kitaalam na kuyatumia vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mifugo inasemekana Tanzania ni nchi ya pili kwa mifugo mingi katika Afrika. Ukweli huu unatudhihirishia kwamba tusingekuwa na shida ya aina yoyote itokanayo na mahitaji ya mifugo kama vile maziwa, siagi, samli, viatu na mazao mengine yatokanayo na mifugo, lakini bidhaa zote hizi nyingi au asilimia kubwa tunaagiza kutoka nje na hata nchi jirani, mfano Kenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hii, naishauri Serikali itimize kwa ufanisi ile azma yake ya kutaka kuifanya Tanzania iwe nchi ya viwanda. Kusudio hili likitimia naishauri sana Serikali kuzingatia ujenzi wa viwanda vya biashara za mifugo ikiwezekana kila mkoa wenye mahitaji haya ili kupunguza mahitaji na malalamiko ya wafugaji na hasa ikizingatiwa sekta hii imeajiri watu wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uvuvi; Tanzania tumejaaliwa na neema kubwa ya bahari, maziwa na mito ambayo ni mashamba yaliyosheheni mazao na ambayo mashamba hayo yaani bahari na mito hayahitaji mbolea wala pembejeo yoyote, bali yanataka kuvunwa tu. Ushauri wangu kwa Serikali, suala la uvuvi limekuwa likiongelewa kwa siku nyingi, sasa wakati umefika wa Serikali kuliangalia suala hili kwa kina kuona kwamba rasilimali hii inafanyiwa kazi ili inufaishe jamii na Serikali kwa ujumla. Serikali imezungumza sana juu ya kuishughulikia Sekta ya Uvuvi, naomba azma hii itekelezwe na tija ionekane kwa manufaa na ustawi wa Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kuwasilisha.