Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Selemani Said Bungara

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii leo. Pili, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi na uhai ili nichangie katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba yetu, inapambana au inakataza dhuluma na uonevu, lakini katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani inaonesha badala ya kulinda wananchi imekuwa wao ndio kipaumbele cha kuwatesa wananchi. Mtu yeyote mwenye dhuluma silaha zake ni mbili; silaha ya kwanza kutamanisha, maana yake kutoa rushwa, silaha ya pili ni kutisha na kuua. Tumefanikiwa Tanzania kwa kutumia silaha hizo za rushwa kuwanunua Wapinzani na kuwatesa watu, mmefanikiwa Serikali ya CCM kutufikisha watu wa Tanzania kuwa waoga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuoni ajabu kwa watu wa Serikali na watu wa CCM kuitetea Serikali ya CCM ambayo inawatesa Watanzania, hatuoni ajabu. Na hata enzi hizo wakati wa Firauni pamoja na ubaya wake Firauni lakini kulikuwa na wapambe wake waliokuwa wanamtetea; hii ina maana kwamba kila mtawala atatetewa na watu wanaomfuata nyuma yake hata kama akiwa mbaya, kwa hiyo, hatuoni ajabu kwa yote yanayofanyika katika nchi hii kuna watu wanatetea kwamba mambo mazuri tu. Hatuoni ajabu kwa jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.Kwa hiyo tunachoangalia hapa ni amani na utulivu na huu ni wakati wa Wizara ya Mambo ya Ndani. Najielekeza katika mada yangu, lakini ninachosema mikono yenu imeingia damu na sisi tunaweza tusiwape mikono kuanzia leo.

Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, katika hotuba ya Waziri Mkuu nilimwambia kuna vijana wangu wawili ambao wamewachukua mpaka leo hawajawarudisha na alisema atakuja kunijibu katika Wizara yake leo; naomba leo jibu langu nilipate, wako wapi na lazima wapatikane. Vijana hao ni Ali Mohamed Shari na Yusuf Kipuka.


Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna viongozi wamekamatwa kule Rufiji, leo nitakutajia viongozi 12, wamewakamata hatujui walipo. Wa kwanza Ziada Nongwa, huyu ni Diwani wa Viti Maalum kwa Tiketi ya CUF na ana mtoto mchanga, wamemkamata wamemchukua hajulikani wapi alipo, ni mama huyu. Nitaona ajabu sana akinamama wa CCM, mama mwenzenu tena Diwani kakamatwa hajulikani alipo, mseme hiyo ndiyo kazi tu, hapana; kwa hiyo, Ziada Nongwa Viti Maalum. (Makofi)



Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine ni Moshi Mchela, Mwenyekiti wa Kitongoji na ni mwanamke vilevile; Braziluli Lyango na mkewe; Jumanne Kilumeke, Mwenyekiti wa Ikwiriri; Kisangi Athumani, Mwenyekiti wa Kijiji na Katibu wa Vijana wa CUF; Kazi Mtokela, Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikwiriri; Mtuko Astella, Katibu wa CUF, Kata ya Ikwiriri; Khamisi Nyumba Mkali, ni Katibu wa CUF, Wilaya ya Rufiji; Baratu Kisongo, Ikwiriri; Kanjoma Mlanzi, mfanyabiashara Ikwiriri; Abdallah Mkiu na Salim Mkiu, Mwenyekiti Mstaafu wa Umwe, wote hao wamewakamata, wako wapi? Waleteni mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba anapofika hapa atuambie wako wapi na lini watawafikisha mahakamani, wazee wao wanalia watoto wao hawawaoni. Namwomba sana Mheshimiwa Nchemba, tuwajue hawa watu wako wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niongelee kuhusu Mashekhe, sisi ni Waislam na Muislam ni ndugu kwa Muislam mwenzake, ukimuua Muislam mmoja umetuua wote, sisi ni ndugu, hatuwaelewi Serikali ya CCM, hatuwaelewi, kwa nini wanawatesa Mashekhe; kwa nini wanawafunga Mashekhe? Wanawachukua Mashehe wanawaweka ndani hawawapeleki Mahakamani, kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waislamu wote tushikamane kama Mwenyezi Mungu alivyosema katika Quran yetu, tupambane na Serikali ya CCM. Mtume amesema mdhalimu yeyote anapofanya udhalimu wake tuseme na tukishindwa kusema tuuondoe udhalimu huo kwa mkono wetu; kasema Mtume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaambia Waislamu wa Tanzania tuutoe uongozi wa Serikali ya CCM kwa mkono wetu kwa kutumia kura, tutumie kura tuitoe Serikali ya CCM, inatuonea Waislamu kwa nini? Tumekosa nini? Mashekhe wetu Zanzibar wako ndani, Arusha wako ndani, Lindi wako



ndani, kwa nini? Kila Ijumaa tuombe dua Serikali ya CCM itoke madarakani, inatuonea Waislam kwa nini, tuna kosa gani sisi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamandharaba nafsi laa yabuk, ajipigae mwenyewe halii, tuiondoe Serikali ya CCM madarakani, Waislam tuungane, tushikamane na Muislamu yeyote atakayesema kwamba Waislam wakae mahabusu huyu sio Muislam, kafir.

Tunaomba sana Waislam tushikamane, wametugawanya kwa makusudi, wametugawanya. BAKWATA inaisherehekea Serikali ya CCM, wengine sisi tukisema hatuonekani. Tunaomba sana Waislamu kama kuna Waislamu kweli tushikamane, Waislam tunateketea.