Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye hoja zilizoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye kwa rehema zake ametuwezesha tumeendelea kuwa wazima na kuwa na afya njema ya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuchangia kwenye eneo moja ambalo nisipolichangia nitakuwa sijajitendea haki. Hali yetu ya lishe nchini siyo nzuri. Katika bajeti ya mwaka jana, kwenye fedha tulizotenga ziende kwenye halmashauri zetu ilikuwa ni shilingi bilioni 11 lakini tulipeleka asilimia 8 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu nataka kama Taifa tulione jambo hili ni tatizo. Takwimu zinatuambia nini juu ya hali yetu? Takwimu zinatuambia kwamba asilimia 34 ya watoto wetu walioko chini ya miaka mitano wamedumaa. Takwimu zinatuambia asilimia 58 ya akina mama waliko kwenye kipindi cha kuweza kuzaa wana upungufu mkubwa wa damu. Hii ndiyo hali ya Taifa letu kwamba tuna changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine wakati tuna lishe duni lakini tuna tatizo lingine la lishe iliyopitiliza, viriba tumbo. Ttizo hili linatuletea sasa magonjwa yasiyoambukiza mfano BP, kisukari na kadhalika. Kwa hiyo, tuna matatizo ya aina mbili kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Rais wa Benki ya Afrika anatuambiaje? Anasema stunted children today means stunted economy tomorrow. Tukiwa na watoto ambao hali yao ni mbaya leo basi tusitegemee kuwa na uchumi mzuri siku zijazo. Ukiangalia hali ya uchumi takwimu zile zinaonyesha kwamba uchumi wetu unakua lakini kwa taarifa hizi maana yake tunakoelekea ni kubaya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mpango mwaka huu hakikisha fedha hizi tulizotenga kwa ajili ya kupambana na tatizo la utapiamlo tunazipeleka zikafanye kazi. Maana wataalam wa economics wanatuambia stunted children today means stunted economy tomorrow. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye eneo lingine, naipongeza Serikali nimeanza kuona jitihada za kuzigeuza halmashauri zetu kuwa ni center za investment, ni jambo nzuri. Nasema ni jambo nzuri kwa sababu tumeanza kuona trend ya kuzinyang’anya vyanzo vyake vya mapato lakini sasa tunapoziwezesha kuwa na vyanzo vingine mbadala vya kupata mapato hili ni jambo nzuri. Maana tumeanza kushuhudia kupitia TAMISEMI tunashawishi halmashauri zianzishe miradi, vituo vya maegesho, standi za magari na mabasi, masoko na kadhalika. Yawezekana ni jambo nzuri lakini uwekezaji huu usipogusa maisha ya mtu wa chini, mtu wa kawaida yatakuwa hayana faida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ndipo napokuja kwenye lile jambo mahsusi la sisi watu wa Pwani. Tafiti zinaonyesha kwamba we have unattempted potential kwenye bahari na maziwa yetu. Mheshimiwa Dkt. Mpango Tanzania tuna Ukanda wa Pwani kilometa 1,424, tuna EEZ kilomita 220,000 lakini kwenye eneo la maziwa na mito tuna takribani kilomita 64,500 lakini tunatumiaje rasilimali hii. Uzalishaji wetu wa samaki ukoje? Takwimu zinaonyesha kwenye mpango kwamba kwa takribani miaka mingapi hii, tumekuwa tukivua kati ya tani 325,000 na 380,000. Katika hizo, asilimia 85 uvuvi huu umefanyika kwenye maziwa, asilimia 14 tu ndiyo umefanyika kwenye eneo la bahari. Mbaya zaidi, ufugaji wa samaki kwenye nchi hii, katika hizo tani 380,000 its only one percent, hii haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ambayo ina potential kubwa namna hii, inachangia ajira asilimia 0.7, haikubaliki. Ukisikiliza taarifa ya Kamati wanasema kwamba tuna tatizo kwenye ajira, tuna tatizo kwenye kuagiza zaidi bidhaa kutoka nje kuliko tunavyoweza kuuza nje, lazima tuwekeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwaige wenzetu South Africa, wao kwenye kutatua jambo hili la ufugaji wa samaki, walichofanya wameanzisha Aquaculture Investment Zone. Wanachofanya wanaenda kuanzisha zone maalum kwenye maeneo fulani fulani, kule Eastern Cape, wanazo hizi karibu saba na maeneo haya yameweza kuzalisha ajira karibu 150,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uzalishaji kwenye eneo hili leo hii wanazungumzia mapato yanayotokana na sekta ya ufugaji wa samaki ya shilingi bilioni 115, sisi hatuzitaki hizi? Wenyewe wamejipanga ndani ya miaka miwili ijayo waweze kufikia mapato yanayotokana na ufugaji wa samaki yanayofikia shilingi bilioni mita tano, sisi hatuzitaki hizi? Mheshimiwa Dkt. Mpango tusaidieni watu wa Ukanda wa Pwani, hizi jitihada mnazotuambia tuanzishe standi za mabasi, masoko, tuwezesheni sisi kwenye ufugaji wa samaki kuanzisha Aquaculture Special Economic Zone, tuweze kupiga bao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine, Bunge hili liliridhia tuingie kwenye matumizi ya sarafu moja kwa Ukanda wote huu wa Afrika Masharika. Sijaona kwenye bajeti hii tumeelezwa vipi. Nafikiri ni vizuri kila tunavyokwenda tuwe tunapeana taarifa kwamba maandalizi ya kuelekea huko tumefikia wapi tukijipima na wenzetu. Vilevile tuelezane vihatarishi tunavyoviona, maana taarifa zilizopo wenzetu Kenya wameshafikia ukomo wa kukopa nje. Kila wanavyokopa wamekuwa wakiambiana kwamba deni linahimilika, hii iwe changamoto kwetu kwamba tukope vizuri tusifike huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye eneo la umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.