Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba hii katika Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba niipongeze Serikali kwa ujumla, Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yote kwa bajeti hizi mbili ambazo wametuletea ambazo zina akisi taswira ya maendeleo ya Taifa letu kwa ujumla. Nawapongeza sana kwa sababu bajeti hizi zimegusa maeneo mengi ambayo yamewagusa wananchi wetu katika sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nianze kwa kupitia ukurasa wa 14 wa kitabu cha Mheshimiwa Waziri ambapo alikuwa ameongelea sana changamoto ambazo zilitukumba hasa katika utekelezaji wa bajeti iliyopita. Changamoto hizo amezitaja hapo, mojawapo ikiwa ni ajira. Tatizo hili la ajira Waheshimiwa Wabunge wengi waliotangulia wameshalizungumza kwamba tunao wahitimu laki nane lakini wanaopata ajira Serikalini ni elfu arobaini tu. Natambua sana kwamba Serikali ndiye mwajiri mkubwa na pamoja na kwamba ni mwajiri mkubwa hawezi akaajiri wahitimu wote ambao wanakuwa wamehitimu katika vyuo vyetu.

Mheshimiwa Spika, tunazo sekta nyingi ambazo zingeweza zikawachukua wanafunzi hawa kwa taaluma hizo ambazo wameshazipata. Moja ya sekta ambazo mimi naiona ni sekta ya kilimo. Sekta ya kilimo ambayo kwa bahati mbaya sana pia imetengewa bajeti ndogo sana katika bajeti ya mwaka 2018/2019 ambayo ni sawa na 0.4 ya bajeti nzima ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sekta ya kilimo ndiyo inayoajiri wananchi wengi sana, zaidi ya asilimia 65. Ni sekta ambayo inagusa wananchi wengi hasa wa vijijini, sawa na kule kwenye Jimbo langu ambako nilipotoka mimi. Hata hivyo utaona kwamba uwekezaji katika sekta ya kilimo umekuwa ni mdogo sana. Matokeo yake tumekuwa na tatizo la ajira, matokeo yake tumekuwa na umaskini mkubwa na mpaka sasa kwa mujibu wa takwimu za Mheshimiwa Waziri hapa tunao maskini wa zaidi ya asilimia 26.4. Tatizo hili ni kubwa, wananchi wengi bado wanaishi chini ya dola moja.

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo ambalo linatufanya tuanze kuangalia katika kuwekeza katika sekta ya kilimo ambayo inaweza kabisa ikawagusa wananchi wengi na ikawaondoa wananchi wengi katika dimbwi la umaskini tulionao. Kwa hiyo, ningeishauri sana Serikali ijaribu kuangalia namna ya kuwekeza katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano, katika Jimbo langu la Singida Kaskazini sisi ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya mahindi, mtama, vitunguu na alizeti. Tunacho kiwanda kikubwa sana cha alizeti Afrika Mashariki ambacho kiko pale Mount Meru; hakina malighafi za kutosha na wananchi wengi wanashindwa kuhamasika kulima kwa sababu wanategemea zaidi tu kilimo cha mvua. Hakuna kilimo cha umwagiliaji ambacho kinaendelea. Ziko skimu za umwagiliaji ambazo hazijafanya kazi kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, nitatolea mfano skimu moja ya umwagiliaji iliyopo katika Kata ya Msange ambayo tangu mwaka 2009 ilishafanyiwa upembuzi, wananchi walishalipwa katika maeneo yaliyozunguka katika lile bwawa, ni skimu ambayo inatarajiwa kuwa na hekari elfu tatu na kuhudumia wananchi zaidi ya elfu kumi.

Mheshimiwa Spika, skimu hii ya umwagiliaji ilianza kutengewa fedha, ilionekana inahitaji fedha zaidi ya bilioni 1.3 tangu bajeti ya 2009/2010. Hadi ninavyoongea hivi sasa skimu hiyo haijafanyiwa chochote hatujapata fedha na wananchi wameendelea kubaki na mpaka sasa tulianzisha tu skimu ndogo ya ekari 25 ya umwagiliaji wa matone ambayo kwa kweli haijaweza kutoa tija kwa wananchi wa Kata ya Msange Maghojoa na Mwasauya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ombi langu kwa Serikali ni kuweka uwekezaji mkubwa katika sekta ya kilimo ambayo inaweza kuwagusa wananchi walio wengi. Tukiwekeza katika kilimo tutakuwa tumewekeza katika kuongeza ajira kwa vijana wetu. Tutakuwa vile vile tumeongeza Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati tunaongea ukuaji wa uchumi wa asilimia saba, sekta ya kilimo yenyewe inakuwa kwa asilimia 3.7. Ukuaji huu ni mdogo mno na ndiyo maana hali ya umaskini inashindwa kuondoka na wananchi wetu wanazidi kuwa maskini kila siku na hata ukiangalia huduma ambazo wanaendelea kuzipata kule vijijini tunashindwa kwa sababu mapato yetu ni madogo na Serikali haina uwezo wa kuhudumia miradi mingi ya maendeleo. Kwa hiyo, nataka niiombe sana Serikali kuwekeza sana katika hilo.

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa 61 mpaka 62 ya kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri wameweka tozo. Toza ushuru wa forodha wa asilimia 25 badala ya sifuri (0) na 10 katika mafuta ghafi ya kula mfano wa alizeti, mawese, soya, mizeituni na kadhalika. Hili ni jambo zuri na lengo hapa ni kujaribu kulinda viwanda vyetu vya ndani. Hata hivyo, tunajiuliza, tozo hizo kwa bidhaa zinazoingia kutoka nje ambazo tumeweka zinawezaje sasa kuwa-encourage wananchi wetu wakaweza kuongeza kipato na kuongeza uzalishaji? Tutakuwa na viwanda vikubwa kama ambavyo tulivyo navyo installed capacity sasa ni kubwa, lakini malighafi zilizopo ni ndogo. Hadi sasa kwa mfano alizeti tunazalisha kati ya tani laki mbili na nusu mpaka tani laki tatu; lakini kiwanda cha Mount Meru pale Singida kinahitaji zaidi ya tani milioni mbili kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, sasa tunahitaji kuwekeza katika mbegu bora zinazotoa mafuta mengi, tunahitaji kuwekeza katika kuwapa wananchi mbegu zilizo bora ili waweze kuongeza tija katika uzalishaji huo. Tukifanya hivyo tutakuwa tumefika mbali na wananchi wetu tutakuwa tumewasaidia sana.

Mheshimiwa Spika, liko jambo lingine ambalo linaambatana na hilo, hasa kwenye upande wa chakula cha mifugo, mfano kuku, ng’ombe na mifugo mingine ambacho kinatokana na mashudu ya alizeti, mashudu ya pamba, Soya na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu lilipitisha zero VAT katika chakula cha mifugo. Hilo ni jambo jema na lengo lake lilikuwa ni katika kuweza kuwasaidia wafugaji. Hata hivyo, tunalo tatizo kwamba zipo malighafi za chakula cha mifugo. Kwa mfano, mashudu ya alizeti, mashudu ya pamba bado yanatozwa VAT kwa sababu msamaha uliotolewa ulikuwa peke yake kwenye HS code ya 23.09 ambao haugusi mashudu haya ambayo yanazungumzwa. Sasa hivi tunavyoongea mashudu haya yanakwenda Kenya yanatengenezwa chakula cha kuku kwa sababu kunakuwa na zero VAT unapo-export, halafu chakula hicho kinarudi tena Tanzania na sisi ndio tunakuja kununua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wawekezaji wengi wanaona bora kuwekeza Kenya wakachukua malighafi Tanzania na hatimaye kurudisha chakula hicho Tanzania na sisi tunashindwa kulinda viwanda vyetu, tunakosa ajira na tunakosa mapato. Kwa hiyo niombe sana Serikali iweze kuondoa VAT katika mazao haya ambayo ni input kubwa kwa asilimia 80 katika utengenezaji wa chakula cha mifugo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana.