Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nzuri ya kuweza kuchangia bajeti ya Serikali itakayotekeleza mpango wa mwaka unaokuja, kwa sababu bila bajeti mpango ulioletwa mbele yetu utakuwa ni vigumu sana kutekelezwa. Naomba nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kutoa maelekezo kila wakati ya kuimarisha uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mnyimi wa fadhila bila kutambua kazi nzuri ya Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango; Naibu Waziri, Dkt. Kijaji; Katibu Mkuu, wataalam wote wa Wizara ya Fedha kwa kuchukua ushauri na kuufanyia kazi na wote umeoneshwa kwenye bajeti hii ilivyokuwa nzuri. Ahsanteni sana na Mungu awaongezee afya na nguvu ya kuweza kutekeleza hayo yote ambayo mmeyaweka kwenye bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri aone umuhimu wa kutekeleza yote ambayo yako kwenye bajeti kwa sababu kutekeleza hayo ndiyo yanayofanya maendeleo yawepo na matumizi ya fedha za Serikali ziende kwenye kuleta ustawi wa jamii. Ukiangalia mwaka uliopita, mwaka 2017/2018, utaona kwamba Wizara ilitengea kila sekta kiasi fulani cha fedha na mwenyewe Mheshimiwa Waziri ameeleza kwamba kwa miradi ya maendeleo ni asilimia 45 tu imetolewa katika fedha zilizotengwa. Kwa hivyo utekelezaji bila shaka utakuwa umeenda kwa asilimia hiyo.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia bajeti vile vile kwa matumizi ni asilimia 80 imetumika. Kwa kiasi hicho matumizi yameenda vizuri kwa sababu ukitaka kuonesha kwamba mpango uliowekwa ni mzuri unaweza tu ukapungua kwa asilima 15 au ukawa zaidi kwa asilimia 15, ikiwa zaidi ya hivyo ni kwamba mipango yetu haitaenda kama tulivyoweka. Kwa hivyo, kwa sababu Mheshimiwa Waziri mwenyewe ametambua hili nina hakika kwa mwaka 2018/2019, mambo yatakuwa tofauti na nategemea kwamba miradi ya maendeleo imetengewa tayari itatolewa hela zaidi na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi utaenda kama ulivyotengemewa na nitashukuru sana kuona hilo linatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, tuangalie fedha zilizotolewa kwa ajili ya miradi zinalipwa kwa nani, kwa sababu kama ma- contractor wanaotoka nje na hela ni za bajeti ya Serikali tukiwalipa kama hatuna masharti ya hela hizo kubakia ndani ya mabenki yetu, ni kwamba hela hizo zitakwenda kujenga uchumi wa watu wengine. Kwa hivyo nategemea ma- contractor watakaopewa kazi watakuwa ni hawa wa ndani ambao wakipata hela, fedha zao zitabakia ndani ya uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo ambayo pengine hatutapata contractor wa ndani; kwa mfano kwenye reli hii ambayo inatengenezwa watakuwa wametoka nje, lakini Mheshimwa Waziri wa Fedha aweke masharti fedha hizo zikae kwenye mabenki yetu kwa muda ili nazo zichangie katika ujenzi wa uchumi wetu, kwa sababu Serikali mpaka sasa ndiyo businessman mkubwa. Kama kweli mipango yake haitapangiliwa vizuri kufikia uchumi wa viwanda na kipato cha kati itakuwa ngumu sana kama hatutakuwa waangalifu sana. Ndiyo maana nasema tuone nani anapewa miradi mbalimbali ili fedha zinazotolewa za Serikali zizunguke ndani ya nchi.

Nilikuwa nasema tuwaangalie ma-contractor ambao tunawapa miradi yetu wawe ni wale ambao wataendelea kuangalia mzunguko wa fedha unabaki ndani ya nchi yetu na kujenga uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, sekta binafsi ina nafasi kubwa sana ya kuchangia uchumi wa nchi yetu na Mheshimiwa Waziri amelisema hilo kwenye hotuba yake; nampongeza na namshukuru kwa kutambua sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua hili Serikali imeweka mazingira wezeshi ya kisera, kisheria na naomba na ya kitaratibu iwekwe. Daima nimesema kuweni na one stop centre kwa ajili ya sekta binafsi kuwekeza kwa urahisi. Ukitaka kuijua hiyo iko Rwanda. Rwanda kuna Rwanda Development Center ambapo TBS sijui TFDA na kila mtu yuko kwenye ofisi moja anapoenda mwekezaji hachukui siku moja inachukua hata masaa ameshapata leseni na kibali cha kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba hizo sheria na utaratibu pamoja na sera iweze kurahisisha uwekezaji wa sekta binafsi ambayo ni muhimu sana. Napongeza Serikali kwa hili lakini naomba ifanyike kwa matendo kuliko ilivyo kwenye hotuba. Jukumu la sekta binafsi ni kutumia mazingira haya ili kuwekeza; naomba mwone bajeti hii ni nzuri na hotuba ya Waziri ni nzuri na sekta binafsi iweze kuwekeza. Naomba sera na sheria ziwe zinatabirika (predictability) wawekezaji wanachotaka wajue wakiweza leo waliyoyaona leo yatakuwepo mwaka ujao na hasa ifikie miaka mitatu au zaidi ili wasiwe na wasiwasi, tuondoe wasiwasi huo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naipongeza Serikali, kwa mfano kuondoa VAT au kuondoa tozo na kodi mbalimbali kwenye pembejeo na kwenye zana za kilimo na Waziri mwenyewe kwenye hotuba yake amesema kilimo kimepewa kipaumbele; isiwe ni kwa kusema tu naomba tufanye kwa matendo, kama walivyoondoa tozo mbalimbali na kodi mbalimbali kwenye pembejeo na kwenye zana za kilimo zitasaidia sana wawekezaji kuwekeza kwenye kilimo. Hakuna investment inayohitaji fedha kama kilimo. Naomba watakapokuwa wamewekeza mazao yatakayopatikana yaweze kushindana na mazao katika nchi nyingine za East Africa au Afrika Mashariki na za SADC.

Mheshimiwa Spika, tulienda Iringa tukakuta wamezalisha chai nzuri na ina hadhi ya juu kweli kweli na ubora wa hali ya juu. Hata hivyo, ukienda sokoni Kenya inauza zaidi kuliko sisi kwa sababu ya vivutio vilivyowekwa. Naomba sana tunavyopeleka nje basi nasi tuangalie mazao yetu ya kilimo yanataka nini ili tuweze kushindana kwenye soko. Kwa hiyo, naomba sana Sera na Sheria ziwe na uhakika na ziwe zinatabirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile napenda kushukuru sana kuona kwamba malighafi zinazokwenda kwenye viwanda hazitozwi kitu chochote, kwa sababu kwenye bidhaa za mwisho tunaweza tukatoza kodi ili tuwe na viwanda ambavyo vitachakata mazao ya kilimo na malighafi nyingine ambazo zinapatikana Tanzania. Siyo hivyo tu, viwanda hivi vitafanya watu walime zaidi kwa uhakika wa soko na kwa hivyo Watanzania wengi watapata ajira kwenye kilimo na viwanda.

Mheshimiwa Spika, naomba niungane na akinamama wenzangu kupongeza kuondoa tozo na kodi mbalimbali kwenye taulo za kike. Huko ni kudhamini uzazi kwa sababu chimbuko la uzazi ni hedhi. Kwa hivyo, taulo hizo zitakavyopunguzwa bei iende moja kwa moja kwa wanaotumia si kwa wale ambao watakuwa hapa katikati. Kwa hivyo, naomba Wizara ya Afya na Wizara ya Viwanda Biashara na Masoko; wataona kwamba taulo hizi zinawapa manufaa wale watakaozitumia na siyo wale watakaotengeneza na wale ambao watauza.

Mheshimiwa Spika, vile vile naomba niungane na wenzangu, tunasema Tanzania inatakiwa kuwa nchi ya viwanda na yenye kipato cha kati. Nami nataka niwaambie katika viwanda kuna viwanda mama au viwanda vya msingi, kuna viwanda vya Kati kwa ukubwa lakini vile vile kuna viwanda ambavyo vitatengeneza bidhaa zitakazotumika kwa kuliwa au kwa matumizi mengine. Naomba tuone viwanda vya msingi vinapewa kipaumbele; na Mheshimiwa Waziri amesema atatoa kipaumbele kwenye mradi wa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie, hakuna kitu ambacho hakitegemei chuma nchi hii. Huwezi kuwa na tairi bila chuma, huwezi kuwa na baiskeli bila chuma, huwezi kuwa na jembe bila chuma na tukiacha kuona umuhimu huo tutakuwa tunajenga uchumi wa wale wenye chuma kule nje na wa kwetu hauendelei kwa sababu tumeacha makusudi kutekeleza mradi wa Linganga na Mchuchuma.

T A A R I F A . . .

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Spika, Liganga na Mchuchuma iko maeneo ambayo hayajaendelea hata kidogo. Linganga na Mchuchuma zitakapotekelezwa watu watapata miradi na watapata kazi za kufanya. Mama ntilie watapika, vijana wataajiriwa na wakulima watalima kwa sababu watakaokuwa kule watakula. Kwa hiyo naomba sana, Mheshimiwa Waziri Bajeti ijayo au hapo katikati tutakapofanya review aseme Liganga imeanza kutekelezwa, tutamshukuru sana na tutamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mhehimiwa Spika, Kampuni ya General Tire tulifunga kwa sababu ilikuwa inasimamiwa na wawekezaji kutoka nje na walikuwa wanachukua hela zetu hatujui wanapeleka wapi na matairi yalikuwa hayatengenezwi. Serikali ikasimamisha, tukasema tutafute wawekezaji walipatikana, sasa tunajiuliza hiki ni kitu gani kiko hapa katikati? Hakuna tairi zinazotoka Arusha; tungefurahi kuona tairi zinatoka ili na sisi uchumi wetu uwe rahisi.

Mheshimiwa Spika, viwanda si kazi rahisi, viwanda vinataka taknolojia, utaalam, ufanisi na tija, viwanda ni soko la rasilimali ambazo zinatokana na maeneo yetu kama mazao ya kilimo, madini na mengine kama misitu; kwa hivyo tutakavyoanzisha viwanda mjue kwamba rasilimali zinazotoka Tanzania zitakuwa zinapewa thamani kubwa humu nchini badala ya kwenda hivi hivi.

Mheshimiwa Spika, tanzanite ikitengenezwa mikufu, pete, ikitengenezwa mambo mengine ya vito itakuwa na thamani kubwa zaidi Tanzania kuliko kwenda Jaipur au Marekani na South Afraica. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwenda kuweka kipaumbele kule Manyara ambako tanzanite inapatikana na kuweka ukuta ambao utahakikisha kwamba mnada utakapofanyika pale Wakenya watakuja pale badala ya Watanzania kupeleka tanzanite Kenya na badala ya Tanzania kupeleka tanzanite South Africa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini hii bajeti ilivyoandikwa ni nzuri sana. Hata hivyo, naomba sana mazao ya kilimo yasiwe na kodi mbalimbali jamani, yafike kwenye soko ili tuweze kushindana vizuri. Soko zuri na la uhakika ni viwanda vyetu; kama hakuna kodi viwanda hivyo vitatumia malighafi rahisi na bidhaa zitakazotokana na viwanda zitakuwa ni rahisi zitashindana na viwanda vya Kenya vya Malawi na South Africa.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo nakushukuru sana na naomba sana kwamba wananchi wa Hanang ni wakulima wa mbaazi iliyokosa soko; mahindi yakafungiwa mipaka watu wakawa maskini, lakini safari hii imefungua mipaka naomba tusaidiane kuona wakulima wanapata soko wa Kibaigwa, huko wa Hanang, Kiteto na maeneo yote hasa wale wa kusini wanaolima mahindi mengi sana na mahindi yana bei nzuri isipokuwa ni sera tu inakosesha wananchi kupata bei nzuri; naomba sana.

Mheshimiwa Spika, wananchi wengi Watanzania asilimia 80 wanalima, sera zikiwa nzuri na hasa za kodi zitasaidia sana wakulima kuwa na masoko na wataendelea kulima na kwa sababu wakilima bila masoko ni sawasawa na kutupa shilingi chooni na hilo halikubaliki.

Mheshimiwa Spika, nimesahau kusemea Serikali kwa kufunga mipaka na kuona wananchi walivyodidimia, lakini watafurahi sana wakisoma hotuba hii na kuona kwamba inatekelezwa. Mungu awape afya, nakushukuru na nakupongeza Waziri.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na Mungu akubariki. Naunga mkono kwa nguvu zote hotuba ya Waziri wetu wa Fedha.