Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii. Nianze kwa kusema hili suala la utekelezaji duni wa bajeti kwa kweli ni tatizo kubwa ambalo lisipopatiwa ufumbuzi itatuwia shida sana. Kwa sababu naona na najiuliza kweli kwamba ni kwa nini tunakaa kwenye hili Bunge na kupoteza muda mwingi namna hii na kufanya uchambuzi kama tunavyofanya na Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mpango pale anakuja na yote haya aliyokuja nayo, lakini mwisho wa siku kunakuwepo na utekelezaji mpaka wa sifuri kwenye baadhi ya maeneo ambayo ni ya msingi sana kama ilivyorejewa hapa na watu mbalimbali kama kilimo na umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, sasa hii inaondoa maana ya Bunge hili, vilevile na nimekuwa nikisema mara kwa mara kuna tatizo la kutumia fedha vibaya. Kama unapeleka fedha zile zinazoitwa za matumizi ya kawaida na OC ambazo hakuna kazi inayokwenda kufanyika. Kwa sababu hizi fedha tunazotoa kama matumizi ya kawaida ni ili zikafanye mambo fulani fulani ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, kama hili jambo halitarekebishwa kama Wabunge na chini yako tutakuwa sisi tunatumia fedha za wananchi ambao ni walipa kodi vibaya. Kwa hiyo ningekuomba sana tuweze kuungana kwa pamoja kama Wabunge tuwaulize Serikali tatizo liko wapi, kwa nini wasije na bajeti ambayo ni ina uhalisi inayotekelezeka ili tukipitisha hapa tunajua kwamba tumefanya kitu ambacho kinakwenda. Wengine ni waathirika wakubwa wa huu utekelezaji duni wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, nina miradi kule kwenye Jimbo langu, miradi ya barabara 2016/2017, barabara moja ambayo inatoka Kiboroloni inakwenda Kikarara inapita kule Suduhi mpaka kule Kidia imetengewa fedha shilingi bilioni 2.5 haikuja hata shilingi. Mwaka 2017/2018 ikatengewa fedha shilingi milioni 810 haijaja hata shilingi. Safari hii nimeona tena Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi ameitengea shilingi bilioni moja na yenyewe sijui niseme itakuja tena sifuri au namna gani.

Mheshimiwa Spika, umesoma kule kwetu unajua kwamba barabara zetu kujengwa kwa kiwango cha lami si luxury ni suala la lazima. Kwa sababu ya hali halisi ya aina ya udongo wetu kule. Vivyo hivyo tuna mradi mmoja wa Telamande - Old Moshi toka mwaka 2012 unazungumzwa kwenye makabrasha yote haujaanza mpaka leo. Sasa katika hali ya namna hii naona ni fedheha kwa Serikali na hata kwa Bunge lako ambalo linakaa hapa na kutumia fedha nyingi kiasi hiki kupitisha vitu ambavyo kimsingi sijui niseme havipo au ni hewa au ni namna gani. Kwa hiyo ni vizuri tukawaomba Serikali wakija hapa watueleze ni kwa nini mambo yanakwenda hivi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni sekta binafsi. Sekta binafsi ni kichocheo kikubwa na ni engine mahali popote pa uchumi. Leo asubuhi uliuliza hapa ni kwa nini Kenya wako kama walivyo, ni kwa sababu wanaheshima na commitment kwa private sector. Sisi katika Taifa letu tunazungumza kila siku kitu kinachoitwa PPP, niulize leo ni mradi gani ambao unaendeshwa kwa huo utaratibu wa PPP, hakuna! Hata hivyo, tunashindwa kufanya mambo kwa sababu hatuwapi fursa watu wa sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, katika Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji tumekuwa na ziara juzi hapa huko Nyanda za Juu Kusini, Njombe, tukakuta wawekezaji wanalalamika. Wakati wanapoagiza vitu kwa ajili ya kuwekeza hapa kuna unafuu wanaopewa wa kodi, lakini wanaambiwa na Serikali walipe fully, walipe kodi zote halafu wa-claim. Hizo pesa hazirudishwi na hata zikirudishwa zinarudishwa baada ya muda mrefu sana, jambo ambalolinaondoa imani kwa Serikali, linaondoa imani kwa wawekezaji na sekta binafsi. Sasa wenzetu huko duniani hawako hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuna kiwanda cha Chai kule Njombe na nasikia Mheshimiwa Rais anakwenda huko, ni vizuri wanadai bilioni 8.2, hawajarudishiwa. Tanga wanadai bilioni 17 hawajarudishiwa, tulipita wakati fulani kule Mwadui tukakuta hivyo hivyo bilioni 12. Sasa katika hali ya namna hii tutakuwa hatujengi uchumi wetu na hatuwatendei haki watu wa sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, mfano mwingine mzuri kuna Wakala wa Mbolea, walifanya kazi hapa wanadai zaidi ya bilioni 64, lakini kirahisi tu Serikali imesema hawadai baada ya uhakiki. Ukienda kuwauliza mpaka leo watu wanadaiwa na mabenki na mbolea zilikwenda, lakini shauri ya technicalities tu unakuta kwamba wameambiwa hawadai. Sasa hali kama hii kwa kweli haiwezi ikatupeleka mahali pazuri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kuwa na miradi mingi na ambayo kila siku tunaanza miradi mipya, wamezungumza watu hapa asubuhi. Tuna miradi kwa mfano, tukienda kwenye eneo la umeme, tuna uchumi ambao tulihubiriwa sana uchumi wa gesi. Hivi ni tatizo gani limeingia kwenye kile kitu tulichokuwa tunazungumza habari ya uchumi wa gesi.

Mheshimiwa Spika, nasikia mpaka leo tunafanya utilization ya 6.8 basi katika uchumi wa gesi na pesa zote ambazo tumewekeza. Sasa katika hali ya namna hiyo ni jambo ambalo linaacha maswali mengi. Pia kuna suala la Mchuchuma na Liganga, kuna suala la bwawa la Kidunda yote haya yangetupa umeme.

Mheshimiwa Spika, sasa kama watu hawa wangeamua wakashika mambo machache na wakayafanyia kazi kwa ukamilifu leo tusingekuwa tunaenda kuhangaika na vitu kama Stiegler’s Gorge, ambayo mimi na naomba iinge kwenye record kwamba siungi mkono hilo suala la Stiegler’s Gorge kwa sababu ni jambo ambalo linakwenda kuleta athari kubwa sana kwa uoto wetu wa asili na wanyama wanaoishi kule Selou na sioni ni kwa nini. Kwa sababu tungefanyia kazi vyanzo hivi vya umeme ambavyo tunavyo tungeweza tukafika mbali zaidi.

Mheshimiwa Spika, mwisho niseme kwamba chema chajiuza kibaya chajitembeza, hivi kweli hizi sifa zote tunazoandika huku hatuwezi kuacha tu historia ikaja ikasema tuliyoyafanya na ambayo tumeshindwa kuyafanya?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.