Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii muhimu ya kuchangia bajeti muhimu iliyo mbele yetu; bajeti ya kujenga Tanzania ya Viwanda. Kwa kweli ukiiangalia bajeti, ukiisoma utaona kwamba sasa tumeanza kupaa kuelekea Tanzania ya Viwanda kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa kwenye bajeti, kila mtu anapotazama bajeti, mwingine atapendelea kuona ni fedha kiasi gani zimetengwa na zinaenda wapi? Kwa mchumi atapendelea kuangalia Sera za Kikodi zinasemaje na zinaweza kusaidia nchi namna gani? Hilo ndilo jambo kubwa sana kwenye bajeti. Ndiyo maana nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Wasaidizi wake kwa bajeti nzuri ambayo imewasilishwa na ukiisoma kwa kina na viambatisho vyake, ni bajeti nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda tu nitoe angalizo kidogo tu, hasa kupitia kwa Mheshimiwa Waziri, awaambie watalaam wake kila jambo linalowasilishwa hapa Bungeni tunasoma kila nukta nakila koma; na mtu mwingine anaweza akasoma kitu kidogo akakitumia kuonesha kwamba bajeti haiko sawa, kumbe ni makosa tu kidogo labda ya Wasaidizi wameshindwa kuweka mambo sawa.

Mheshimiwa Spika, nitatoa mfano tu, halafu naomba Mheshimiwa Waziri awaelekeze Watalaam wake na Wasaidizi wake wawe kila jambo linaloletwa ndani ya Bunge hili wahakikishe liko sawa. Vinginevyo linaweza likawa jambo dogo halafu mtu akaanza kushughulika na hilo ikaonekana bajeti yote haina kitu, kumbe ni uzembe wa mtu mmoja kwenye dawati fulani. Huu ni mfano tu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ukisoma kitabu cha Mipango kinaeleza vizuri tu kwamba akiba ya fedha za kigeni, tuna fedha za miezi mitano (5.4). Ukisoma kitabu kingine hiki cha Hali ya Uchumi wa Taifa katika mwaka 2017, hawa wanatuonesha tuna fedha ya miezi sita. Sasa sita na 5.4 ni vitu viwili tofauti. Sasa makosa madogo madogo kama haya yakikutana na wenzetu wa upande wa pili kule, wanaweza wakashughulika nayo ikaonekana ni jambo kubwa kumbe ni uzembe kidogo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, bajeti ni nzuri na nisingependa kupoteza muda kwa vitu vidogo vidogo kama hivyo. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tujikite kwenye mambo ya msingi na namwomba Mheshimiwa Waziri na Naibu wake wawambie Wasaidizi wao wawe wanaangalia vitu hivi visije vikatupotezea muda bila sababu ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitazungumzia kuhusu PPP (Public Private Partnership), naona ni jambo muhimu sana hili. Ni jambo muhimu sana kwa sababu ukiangalia changamoto tuliyonayo, kilio tulichonacho ni kwamba fedha za maendeleo haziendi kwa wingi kama tulivyotarajia, lakini ukiangalia na shughuli za maendeleo tulizonazo, mahitaji ya maendeleo tuliyonayo nayo ni makubwa; tunaingia kwenye Rufiji, tunahitaji fedha nyingi, standard gauge tunahitaji fedha nyingi.

Mheshimiwa Spika, miradi hii kama tungejipanga vizuri, tunaweza tukatafuta fedha kutokana na vyanzo vingine na kwa hiyo, tukatoa unafuu mkubwa sana kwenye bajeti kujikita kwenye shughuli nyingine za maendeleo na shughuli nyingine. Nadhani ni eneo la kuangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ili tulifanye, tunayo Sheria ya Public Private Partnership. Sheria ile ukiisoma inatoa vivutio lakini haivutii sana wawekezaji kupenda kuingia kwenye Public Private Partnership. Katika Bunge hili tutakuwa tumefanya jambo kubwa kama sheria hiyo Mheshimiwa Waziri akiona inafaa, ikaletwa tukajaribu kuongeza vivutio vitakavyotusaidia kuhimiza watu kuingia kwenye Public Private Partnership. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tulifanye hili, kwa sababu tusipofanya hivyo, tutajikuta miaka mitano inaisha, Watanzania wanaendelea kulalamika kwamba hawaoni fedha kwenye mifuko, tutajikuta tunaendelea kuwa na miradi mikubwa, ambapo utekelezaji wake ni gharama. Kwa kweli mtu akiangalia kwenye mfuko kama fedha haioni, hata uelezee uchumi vipi Mheshimiwa Mpango itakuwia ngumu sana kueleza. Maana watu wanaangalia je, akipeleka mkono kwenye mifuko kuna kitu?

Mheshimiwa Spika, nakumbuka kwa mara ya kwanza nilipogombea Ubunge katika hotuba ya kwanza nikaeleza sera za uchumi zilivyo, mfumuko wa bei na kadhalika. Baadaye kuna Mwalimu mmoja wa Shule ya Msingi moja pale, akaja akasema, kijana unaongea vizuri mambo ya uchumi haya, lakini mbona hatukuelewi? Unazungumza vizuri, mfumuko wa bei na kadhalika, lakini mbona hatuelewi Mheshimiwa?

Mheshimiwa Spika, Katibu wa Chama wa Wilaya yangu Mzee Kamaleki, akaniambia, Mheshimiwa Kamala, unajua kule ulikuwa unafundisha, sasa huku umerudi kwa watu. Sasa unachofundisha darasani na kwa watu, lazima viendane. Nikamwuliza, tunafanyaje? Akasema, wewe subiri nikuoneshe, angalia ninavyoomba kura, mimi Mheshimiwa Kamaleki Masikini Lufufu nisikilize vizuri, kwa style hii ukifanya kama ninavyofanya mimi, watu watakuelewa. Kwa hiyo, taratibu nikabadilika. Kwa hiyo, nikajua kuna kile kilicho kwenye vitabu, lakini kuna kile cha kutekeleza, ni vitu viwili tofauti kabisa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mpango naomba aliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo PPP, nitaenda haraka. Kuna mifano mingi tu. Kwa mfano, ukienda Johannesburg pale, utakuta mradi mkubwa wa Gautrain unaounganisha Johannerburg na Pretoria wa train, wamejenga kwa PPP. Ukienda Marekani unafahamu Mheshimiwa, unaenda mara nyingi kule, New York pale utakuta daraja linalounganisha Manhattan na Queens wamejenga kwa PPP. Naomba Mheshimiwa Mpango waliangalie. Hii PPP, tuleteni ile sheria tuongeze vivutio itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka nilipokuwa Balozi kule Brussels, nilimpigia simu Mheshimiwa Mpango tukazungumza na aliniambia kwamba alikuwa na miradi ya kielelezo, tukazungumza. Nikamwambia nilikuwa nimeandaa mkutano mkubwa kule, bahati mbaya hakuweza kuja. Sasa bahati nzuri sasa ni Waziri wa Fedha, hiyo miradi najua bado anayo na bahati nzuri nami niko hapa, hebu alete miradi yake hapa na Mheshimiwa Spika atalifanyia utaratibu nitarudi tena Brussels niiuze sasa kama Mbunge. Haya yanawezekana; na ile miradi najua bado anayo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo miradi tukiifanyia kazi itatusaidia sana kupaa. Hatuhitaji kutumia shilingi, unahitaji tu utoe fedha kidogo, unipe per diem kidogo hapa, Mbunge anaenda first class, usisahau; haendi economy. Sasa Balozi huwezi kumweka economy. Tukienda hivyo, tutauza hii miradi na nchi itaenda. Ule mradi wa Mkulazi, tunazungumzia mambo ya Kitaifa. Pale Mkulazi kuna mashamba tu, kiwanda bado hawajaanza kujenga. Jana usiku nilikuwa nazungumza na Maafisa Magereza wako pale, wakasema Mheshimiwa pale Mkulazi bado hatujaanza kujenga, kuna store tu peke yake…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nimalizie kwa kuunga mkono kwa uamuzi wako kuhusu malighafi, kuhusu Crude Palm Oil, ile kodi ya 25% na 35% hatua alizochukua Mheshimiwa Waziri ni sahihi na naomba asiyumbe. Kwenye bajeti amesema kwa mwaka mmoja; isiwe kwa mwaka mmoja, iwe kwa miaka yote. Kwa sababu tunataka kujenga Tanzania ya Viwanda. Yuko sahihi, aendelee kufanya hivyo hivyo, asiyumbe na wala asiogope, kwa sababu najua jambo hili lina changamoto nyingi, lakini asimame imara na sisi Wahesimiwa Wabunge tuko imara, tutasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.