Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuipongeza sana Serikali kuanzia na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa hatua thabiti anazochukua za ujasiri na uthubutu wa hali ya juu katika kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi yetu sasa zinanufaisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Naibu wake na Watendaji wote wa Wizara kwa hotuba nzuri sana mbili zote ambazo zimetolewa ambazo kwa kweli zimeonesha jinsi gani Serikali imekuwa sikivu, imezingatia masuala muhimu ambayo Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiyatoa mara kwa mara, lakini imejielekeza sasa katika suala zima la uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa pongezi sana kwa sababu nimeona jinsi ambavyo hii bajeti kwa kweli safari hii imefurahisha Umma mzima wa Watanzania. Kuna mambo machache tu ya kurekebisha ambayo yako chini ya uwezo wao na naamini kabisa watayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, nataka nianze kuzungumzia suala zima la amana pamoja na mikopo kwenye benki zetu. Bado kuna hatua kubwa sana inahitajika kufanyika katika kuelimisha wananchi wa Tanzania matumizi ya benki kwa maana ya kuweka akiba na mikopo. Bado benki zetu zinafanya kazi kwa kiwango cha chini sana kwa maana ya kuwafikia wananchi wengi ambao wanahitaji huduma hizo.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna suala zima la huduma za kifedha kutumia mitandao. Hii ingekuwa ni fursa kubwa sana kwa benki sasa kujiunga katika huduma kama hizo kurahisisha kuwafikia wananchi kwa huduma za kifedha kwa maana ya amana pamoja na mikopo.

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye suala hilo hilo la mikopo, kutokana na taarifa tulizopokea bado tuna tatizo kubwa la mikopo kwa sekta binafsi haliendi vizuri na hata kwa benki zenyewe. Hii imedhihirika kutokana na sababu kubwa za mikopo chechefu ambapo tumekuwa tukielezewa ambayo vilevile kwa upande mmoja inatokana kwanza, pengine na jinsi ambavyo benki yenyewe imekuwa ikitoa mikopo hiyo lakini kwa kiasi kikubwa inatokana na Serikali na Taasisi zake kushindwa kulipa Wakandarasi na watoa huduma wengi na hivyo kuwasababishia wao kushindwa kulipa mikopo yao benki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili naomba sana Serikali ilifanyie kazi kwa sababu uchumi unategemea sana mzunguko wa fedha. Sasa kama kuna fedha iko mahali imetumika lakini hairudi, inasababisha wafanyabiashara, wazalishaji wadogo na hata hao wanaoambiwa wamefunga maduka au wamehamia wapi na wapi, inatokana na kuwa labda wameshindwa kumudu sasa kuendesha biashara bila kurudishiwa madeni ambayo wanaidai Serikali. Napenda sana hilo lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna suala zima la uwekezaji kwenye miradi ya umma au miradi ya kimkakati. Kwa muda mrefu sana humu ndani tumekuwa tukizungumzia miradi ya kimkakati ambayo kwa msingi wake, hii ndiyo ingezindua au ingefufua au ingechangamsha sana viwanda vyetu. Miradi ya chuma, makaa ya mawe, magadi (soda ash); hii ni miradi ambayo inajenga msingi wa viwanda. Sasa bila hii kuanzishwa na kuendelezwa tutashindwa hata kuendeleza viwanda ambavyo tunavitegemea.

Mheshimiwa Spika, tuna mradi wa Kilimanjaro machine tools, huu ulishindwa kuendelea kwa sababu huko nyuma ilibidi chuma kiagizwe kutoka nje, sasa tuna chuma nchini, kiendelezwe ili viwanda kama hivi sasa vianze kuchonga vipuri tunavyohitaji kwa ajili ya viwanda vyetu. Kwa hiyo, unaona moja kwa moja kuna muunganiko mzuri sana sasa hivi katika nchi yetu wa kiuchumi ambao utawezesha viwanda kukua kwa haraka sana. Tungependa sasa kuona jinsi ambavyo hii miradi ya kimkakati inaanza kufanya kazi. Tumeisikia kwa muda mrefu, tunataka sasa ianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna suala zima ambalo nataka kuipongeza sana Serikali, wamejikita katika kuhakikisha kuwa kilimo, maji na miundombinu ya uwekezaji wa kwenye nishati unapewa kipaumbele. Hii vilevile ni misingi mizuri kwa ajili ya viwanda. Sasa kwenye kilimo nataka kuishauri Serikali, tusifanye kazi kwa mazoea. Kilimo kinahitaji mapinduzi makubwa sana ili kiwe kweli kilimo kitakacholeta tija. Tunatakiwa kuwekeza asilimia 10 ya mapato yetu kwenye kilimo peke yake. Hiyo ndiyo itatuwezesha sasa kukuza kilimo katika yale mazao ya msingi ambayo tunajua yatatusaidia katika viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mifano ya nchi kama Vietnam. Vietnam mpaka mwaka 1990 walikuwa wanaagiza chakula nje. Sasa hivi katika nchi 10 au 20 zinazozalisha mazao ya kilimo kwa wingi, Vietnam na yenyewe imo ndani. Wameboresha kilimo chao na uzalishaji wao na ufugaji kwa ku-modernize, kwa kutumia teknolojia, kwa kutumia ubia na nchi zilizoendelea ili kuhakikisha kuwa wananchi wao wanazalisha kwa tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kwa nini tusifanye hivyo? Sasa hivi tumeingia kwenye uhusiano wa Kidiplomasia na Israel. Israel wana teknolojia ya hali ya juu katika masuala haya ya maji, umwagiliaji na kilimo. Tunaweza tukaungana nao. Hii siyo ngumu sana, kwa sababu vijana wetu wakienda kule au wao wakija kwetu, moja kwa moja tunaweza tukajikuta tunakuza kilimo chetu.

Mheshimiwa Spika, tuna mazao tayari yanaonyesha tija kubwa sana. Kwa mfano, korosho, ufuta, mbaazi, nafaka za aina mbalimbali na dengu; sasa hivi tunahitaji kupeleka pia uzalishaji mkubwa kwenye kilimo cha mawese na alizeti. Yote haya ni mazao yanayotakiwa yapewe kipaumbele zaidi ya yale mazao ya kawaida ambayo tulikuwa tumezoea kuzalisha ya kahawa na mazao mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuki-diversify namna hii tutakuta kilimo chetu kinachangia pato kubwa zaidi kuliko ilivyo sasa hivi. Ni lazima sasa hivi tujipambanue na kilimo kama njia kubwa ya kuingia kwenye viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile biashara ni eneo ambalo tumekuwa tunakua vizuri, siyo Tanzania peke yake, lakini Afrika Mashariki, Afrika na hata dunia nzima. Tanzania tuko katika nafasi nzuri sana kwa sababu tuna maeneo makubwa ya mipakani. Cross border trade bado ni eneo zuri sana kwetu sisi Watanzania, lakini limegubikwa na mambo mengi ya urasimu ambayo yanafanya isiwe rahisi kwa biashara kuendeshwa kati ya mipaka yetu.

Mheshimiwa Spika, tuna matatizo ya watu wa customs, tuna matatizo ya uwezo mdogo wa kusimamia masuala haya, tuna matatizo ya rushwa, tuna matatizo ya bureaucracy, yaani licensing na zile taratibu nzima za kufanya biashara kati ya nchi na nchi bado hazijawa nzuri hata katika Kanda ambazo tayari tuko katika umoja. Kwa mfano, East Africa, tujaribu sasa kuondoa zile non-tariff barriers ambazop ndiyo zinazoturudisha nyuma, tuanze kufanya biashara sisi wenyewe kwa wenyewe. Tuachane na mambo ya kukimbizana na nchi za nje ambao wanatuletea vikwazo vingi sana. Tuna fursa kubwa sana sisi Waafrika kwa Waafrika kufanya biashara pamoja.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.