Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana nami kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti yetu hii ya mwaka huu. Nianze na jambo la kwanza la ugatuaji wa madaraka, yaani D by D na Halmashauri. Niliwahi kuwa Diwani, kwa hiyo, nazungumza kitu ninachokifahamu na umuhimu wa Halmashauri hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iwe kwenye record kabisa kwamba Mheshimiwa Dkt. Mpango atakuwa Waziri wa kwanza na Serikali hii kuua Halmashauri za nchi hii. Nchi hii ina vijiji 18,000. Jimbo langu peke yake lina vitongoji 500. Hawa watu mwaka 2017 walianza na waraka wa kuzuia Madiwani kuwachukulia Watumishi wa Halmashauri hatua. Ilikuwa namba moja kuua Halmashauri zetu. Wakaja na kuondoa pesa zote kutoka Halmashauri kupeleka Hazina then Benki Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wakaja kuchukua vyanzo vyote vya Halmashauri ikiwemo mabango na property tax wakapeleka kwenye ukusanyaji wake. Wakaja na mfumo wa kuondoa ripoti za Halmashauri kutoka quartely kwenda kwenye nusu mwaka na sasa kwenye kitabu chake hiki anaanzisha Akaunti ya Pamoja, kwamba pesa zote ziwe zinakusanywa zinawekwa kwenye akaunti. Tarime tukitaka kufanya matumizi asubuhi, tunampigia simu Mheshimiwa Dkt. Mpango ndiyo atuletee tuzibe tundu la choo lililobomoka kwenye Kijiji ha Kemakorere, kwenye Kitongoji cha Nyangasare; vijiji 18,000. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Sera ya Afya ya nchi hii ilivyo, tukiwa na zahanati kwenye kila kijiji, tuna zahanati 18,000. Tukienda na shule, tuna shule 18,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye Kata tuna Kata zaidi ya 7,000. Tukiwa na Kituo cha Afya kila Kata, tuna Vituo vya Afya 7,000. Bulb ikiharibika kwenye nyumba ya mtumishi wa zahanati ya kitongoji fulani, tuombe pesa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Mpango, Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanataka ku-centralize waongoze nchi hii kutoka Dodoma, hii siyo Rwanda na hawataweza.

La kwanza hilo. Kwa sababu, wame-copy kutoka Rwanda, kutoka Namibia na kutoka Uganda. Rwanda ni mkoa kama Mkoa wa Mara. Tarime peke yake nimesema tuna vijiji 88. Hii nchi ina vijiji 18,000; Mheshimiwa Waziri atakaa hapo awe anapigiwa simu kwamba tundu la choo limeharibika kijiji fulani anapeleka pesa, anaweza hilo? Wasitake kuua nchi hii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna kichaka Serikali hii imekuwa ikitumia kwa miaka yote kufanya ufisadi, ni kichaka cha umeme. Hapa kwenye ukurasa wa nane, katika kitabu cha Mheshimiwa Dkt. Mpango hiki, anasema, nampongeza Rais kwa ujenzi wa umeme wa Megawatt 2,100 sijui wa Bonde la Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufisadi mkubwa wa umeme Richmond ulikuwa ufisadi wa umeme wa CCM; Tegeta Escrow ufisadi wa umeme wa CCM; Songas, ufisadi wa umeme wa CCM; na mpaka leo nchi hii haijawahi kupata umeme wa kudumu. Leo ukiwauliza hata Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango na Mawaziri wote hao, kulikuwa na kelele kubwa sana hapa kuhusu wizi wa Tegeta Escrow.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bunge na Bunge lilikaa mpaka usiku wa manane hapa, likataja watu. Leo walioko gerezani, nami nataka Mheshimiwa Waziri aje anijibu; ni Harbinder Singh na Rugemalila peke yao. Je, hao ndiyo walioiba bilioni 309 za nchi hii? Nataka waje watujibu hapa. Kwa sababu anatengeneza ufisadi mwingine wa kwenda kuiba pesa za Watanzania zaidi ya shilingi bilioni 10 kwenye Stieglers Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nimuulize Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango, hivi ni utaratibu wa kawaida, leo wanakwenda kwenye nishati wanaonesha kwamba wanahitaji shilingi bilioni 700 kwa ajili ya mradi ambao hatujui na Bunge hili halijui ukamilishwaji wake utakuwa wa shilingi ngapi? Total amount ya kukamilisha ule mradi ni kiasi gani ili tujue tunapoidhinisha shilingi bilioni 700 bado Bunge hili litadaiwa kiasi gani ili ule mradi ukamilike? Sasa wanataka kuanza kuleta shilingi bilioni 700, kesho shilingi bilioni 800, keshokutwa shilingi bilioni 900 Tegeta Escrow, Escrow nyingine na Richmond nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Gujarat India, juzi walisema linakwenda kuzalisha umeme wa Megawatt 5,000 kwa umeme wa Solar kwa gharama ya Dola bilioni 3.384 ambazo ni sawa na shilingi trilioni saba. Mimi, Mheshimiwa Kitandula na Waheshimiwa Wabunge wengine mwaka 2017 tulikwenda Marekani na hii initiative ya Power Africa, tumekuwa na Mheshimiwa Kitandula pale na Waheshimiwa Wabunge wa CCM walikuwepo; nchi hii ina potential ya umeme kutoka kwenye Solar na kwenye wind. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wind peke yake ukichukua Makambako, Singida na Same, tuna uwezo wa kupata umeme Megawatt 24,000. Solar ambayo India wanatumia shilingi trilioni saba kupata Megawatt 5,000 sisi tunakwenda kutumbukiza shilingi trilioni 10 kwenye Megawatt 2,100
ambazo India wamepata zaidi Megawatt 2,900 zaidi kwa bei ya chini ya shilingi trilioni mbili. Huo umeme hautapatikana, wataua viumbe hai pale Selous, wataua pori la Selous na hawatakaa wapate huo umeme wa Megawatt. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mheshimiwa Dkt. Mpango aje atuambie hapa, dunia nzima kwenye viwanda wanatumia umeme wa gas na wanatumia nuclear power. Mheshimiwa Waziri viwanda vyake hivyo vya kutumia umeme wa maji ambao alikuwa na Bwawa la Kihansi, Hale na Mtera, hayakudumu hata miaka 30 ukajaa udongo mle na hayafanyi kazi. Atuambie hilo bwawa lao la Stieglers Gorge la shilingi trilioni 10 za Watanzania life span yake ni miaka mingapi? Ili tuweze kulinganisha hizi shilingi trilioni 10 na life span ya hilo bwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anakuja hapa anatuambia SGR, hawawaambii Watanzania ukweli. Mapato yetu kwa mwaka mmekusanya maximumly wamepata shilingi trilioni 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mishahara ni shilingi trilioni saba, deni la nje shilingi trilioni tisa, wana nakisi ya shilingi trilioni mbili. Hizo pesa za SGR ambazo wanasema ni za kwao za ndani, ziko wapi kwenye hizi shilingi trilioni 14? Wawaambie watu ukweli, SGR wamejenga wapi hata mita moja? Watuoneshe! Wanaenda wanaweka vizimba, wanazindua. Wale Wakandarasi wameshindwa kuwalipa hata petrol, wameondoka. Wawaambie Watanzania ukweli. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anakaa hapa anakuja anatudanganya hapa eti tunamsifia Mheshimiwa Rais kwa kujenga ukuta wa Mererani, hivi watu pale wanaiba kwa mikataba au wanaiba kwa kupora Tanzanite na kuondoka nayo? Wale wale ambao
tuliwalalamikia; wale wale waliolalamikiwa na wachimbaji wadogo wa Mererani wamewarudisha mle mle ndani ya ukuta, yaani ni jambo la ajabu! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamewapa nini? Watuambie Mheshimiwa Dkt. Mpango. Watuambie kwamba wanawadanganya Watanzania; leo anakuja hapa anatuambia apandishe bei ya bidhaa. Sisi kwa mfano, tunaishi mpakani, tuna advantage hiyo ya kuishi mpakani. Leo sukari kutoka Kenya Sh.1,200/= Tanzania pale Sirari. Sukari ya kutoka Kagera Sugar Sh.2,200/=, anataka mtu wa Tarime aumie kwa expense yako? Mfuko wa cement wa Bambuli Sh.4,000/=, mfuko wa cement wa Twiga Sh.22,000/=, hawataki Mtanzania wa Tarime anunue mfuko Kenya? Kama wanataka viwanda vyao vishindane, vilete cement kwa bei competitive na ya Kenya, Watanzania wenyewe wachague watanunua wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawawezi kuzuia Watanzania kupata vitu vya bei rahisi na vyenye ubora eti kwa expense ya viwanda vya Wahindi ambavyo siyo vya Serikali hii. Siyo vya kwao, wao hawana hata kiwanda cha nanii; ana viwanda cha tofali, cherehani tano, sijui viwanda vya maandazi, hivyo ndivyo wanavyoweza Serikali ya Awamu ya Tano. Hakuna viwanda vingine, hakuna.