Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo, lakini pia niendelee kushukuru kwamba nimepata fursa ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la kwanza na kila mwaka naendelea kushauri hivyo; tubadilisheni mfumo wa bajeti yetu, badala ya kupanga matumizi kwanza, tukusanye kwanza halafu ndiyo tupange matumizi, ndiyo tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ndani ya Bunge tubadilishe mfumo wa Budget Cycle yetu. Badala ya kipindi hiki ambacho tunakuja kukaa, hakuna tunachoweza kubadilisha, tungekuwa tunakaa kwanza tunakubaliana kwamba haya yapitishwe, haya yapande, halafu ndiyo tukija huku inakuwa ni kupitisha tu, mambo yote tunakuwa tumewekana sawa. Hapo ndiyo tutakuwa na mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwamba mwaka huu hawakupandisha kodi katika maeneo mengi, isipokuwa zile ambazo zinatoka nje ya nchi ili kulinda viwanda vya ndani. Kwenye excise duty hawajapandisha kabisa, lakini lengo ni kuhakikisha kwamba tunakusanya mapato zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri kwamba wangewekeza zaidi kwenye maeneo ambapo watapata mapato yasiyo ya kikodi, hapo ndiyo uchumi wetu utakua. Fedha hizo tungewekeza kwenye maeneo ya miradi ambayo returns zake ziwe zinakuja kwa haraka, tutapata mapato. Hata kwenye ukusanyaji wa kodi, tusiwe tunapandisha viwango vya kodi au tozo badala yake tutanue wigo, watu wengi zaidi walipe kodi. Kila Mtanzania akilipa kodi, nina uhakika tutakusanya kodi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote naendelea kushauri hapa kwamba sekta isiyokuwa rasmi inaendelea kukua.

Zamani ilikuwa asilimia 50, sasa hivi iko asilimia 70. Iko siku tutafika asilimia 100 kutokana na ada, tozo, kodi, ushuru; yaani ni utitiri umejaa. Tumeambiwa wanaleta blue print, lini wataileta? Lini itafanya kazi? Ukiondoa kitu kimoja kwa mwaka mmoja, hujasaidia viwanda vya ndani, wala hujasaidia uzalishaji wa ndani. Kazi ya kwanza ilitakiwa hizi kodi, ada na tozo mbalimbali wangezifanyia kazi wangeona uchumi wetu unakua na uzalishaji wa ndani (local production) ungekua haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vyetu havikui, uzalishaji wetu hata huko kwingine haukui kutokana na hizi tozo, kodi, ada na ushuru mbalimbali, ni kubwa sana. Hiyo yote haihusiani na Wizara ya Fedha tu, Wizara zote kila moja ambayo inahusika ilitakiwa wakae pamoja waziondoe. Hii blue print bado wanachelewa sana kuileta, tusitegemee tutakuwa na maajabu kwenye viwanda. Viwanda vyetu haviwezi kukua hata siku moja haya yasipobadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kabla ya hizo Kanuni zote ambazo Mawaziri wamepewa mamlaka, ikiwezekana Bunge tubadilishe sheria au sijui nimefikiri vibaya, ila ilitakiwa Kanuni zije hapa kabla hazijaruhusiwa kwenda kuwa printed kwenye Government Gazette ili kabla Waziri yeyote hajapandisha tozo yoyote, sisi Wabunge tuwe tunajua kwamba hii sasa inaenda kupitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii hapa wamekaa kimya wote kwa sababu hata bajeti hii ikiwa ndogo, kwenye tozo kule kwenye Kanuni anaenda kupandisha anavyotaka. Hiyo ndiyo inafanya ukuaji wa uchumi wetu udumae kabisa; badala ya kwenda positive inarudi inakuwa negative. Kwa hiyo, naomba hizo Kanuni sisi kama Wabunge wote tuziangalie upya, kabla ya kufika kwenye Finance Bill, kama kuna marekebisho tufanye hayo marekebisho kwa sababu tutaendelea kumlaumu Waziri wa Fedha, nyingine haziko kwake, ziko kwa Mawaziri wengine wote na kila mmoja anang’ang’ania tozo zake au ada zake asiziteremshe. Kila akiamka kila akipenda anapandisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hiyo ndiyo itafanya uchumi wetu ukue kama hizo kanuni zote zitakuwa zinapitia Bungeni. Ninavyojua, sheria inasema jambo lolote ambalo inahusu kupandisha kodi yoyote au tozo yoyote, lazima lipitie Bungeni. Sasa sijui lini imebadilika? Sasa naomba hilo lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwamba wamekuwa na tax amnesty. Nampongeza sana kwa hilo, watu wengi wataenda kulipa. Ila naomba tunge-extend isiwe tu kwenye tax administration kwa upande wa kodi ambazo wanakusanya kama TRA, wangeweka kwa upana wote, yaani kwenye Regulatory Boards zote, watu wanadaiwa vitu vya ajabu ajabu. Watu wanaamka kule wanadai vitu vya miaka 10 nyuma. Wangeweka kwamba zote wangezisamehe kwa muda wa miezi sita tuanze moja. Nina uhakika tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, hapa tulikubaliana kwamba Local Government Development Grant ambayo Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania wote ndiyo tunaitegemea huko kwenye Halmashauri zetu. Tumekubaliana hapa watatoa fedha za Elimu na Afya kutokana na ile miradi tuliyopanga; lakini nimepitia Volume IV, sioni mahali imetajwa kabisa Local Government Development Grant.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya reallocation mwezi wa Saba, Nane na wa Tisa hizi pesa hazitakuja, tutaumia. Lazima wote tukubaliane kwamba hapa ifanywe reallocation na tuone kwenye hii bajeti kwamba Local Government Development Grant iwepo na hizo fedha ziendelee kuja. Hizo ndiyo zinatusaidia huko kwenye kujenga Zahanati, Vituo vya Afya, kujenga na shule. Tusipofanya hivyo, tutaumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauripia kwenye utafiti, tufanye reallocation tuhakikishe kwamba kunakuwa na pesa kwenye utafiti. Hatuna! Pesa kwenye utafiti tunategemea wafadhili wa nje, tunaweka pesa kidogo sana. Mtu wa nje akikuletea pesa, anapeleka mahali ambapo naye ana maslahi yake, hapeleki mahali ambapo sisi tunapahitaji. Kwa hiyo, kwenye utafiti tuwekeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tunashukuru wameondoa kodi kwenye taulo za akinamama, animal feeds na kwenye maziwa, lakini wameondoa VAT, yule mtu hawezi kudai import taxes. Naomba tukifika kwenye Finance Bill waje na measures kwamba tunafanyaje ili viwanda vya ndani viweze kupona bila wao kukusanya import taxes au kupata refund, itakuwa importers wanapata faida badala ya wazalishaji wa ndani. Hapa tutakuwa hatujasaidia wazalishaji wa ndani, tutakuwa tumewasaidia wale ambao wana-import ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze kwamba wameweza kupunguza income tax kwa viwanda vipya kwa Sekta ya Ngozi na Sekta ya Madawa. Naomba hata vile vya zamani wangewaruhusu wapate 20 percent. Siyo kwenye hiyo tu, viwanda vyote vipya, sekta zote wangewapa tu hiyo tax incentive ya 20 percent kwa sababu ni ndogo, hakuna kiwanda ndani ya miaka mitano kitakuwa na faida kubwa. Kwa hiyo, hawatapoteza sehemu kubwa. Kwa hiyo, kama ni ndogo, itakuwa ni moja katika maeneo ambayo watapata tax incentive.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la ETS. Namwomba Mheshimiwa Waziri, ndani ya hizi siku chache apate takwimu sahihi ya idadi ya chupa au idadi ya units ambazo tunazalisha nchini, halafu apige hesabu na hizo bei ambazo tulipewa kama bei elekezi ambayo wanategemea kupiga hizo stamp. Ni bora wangepandisha asilimia tano kwenye ushuru kutokana na inflation kuliko kwa hizo bei ambazo tumepewa. Lengo hapa ni kuhakikisha kwamba wale wote ambao hawaoneshi records zao vizuri au wana- under declare tuweze kuwapata. Ila lengo siyo kwamba hao tuwakomeshe na kupandisha gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la ETS tumeifanyia kazi vizuri, naye ana uwezo wa kupata units ngapi tunazalisha kwa mwezi na kwa mwaka halafu kutokana na hiyo, sisi tulivyopiga hesabu, stamp haitakiwi kuzidi shilingi moja au shilingi mbili. Kwa hesabu zetu, tunazalisha zaidi ya units bilioni tano kwa mwezi. Ukipiga kwa miezi 12 ni bilioni 60 mara shilingi mbili ni 120 billion, inatosha hiyo kurudisha uwekezaji wake pamoja na kupata faida. Kwa hiyo, kwenye stamp hii kwenda shilingi kumi na tatu, ni bora angepandisha asilimia tano kwenye inflation kuliko hizo rates. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye pombe kali. Bado huko kuna udanganyifu mkubwa unafanyika kwenye suala la uzalishaji na ndiyo maana kuna watu wanaweza kuuza bei ya chini kuliko gharama za uzalishaji kwa sababu kuna upotoshaji. Hapo sisi tunaamini kuna zaidi ya shilingi bilioni 400 au 500 zinazopotea. Ni eneo ambalo nashauri walifanyie kazi na wataweza kupata kodi nyingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naendelea kusisitiza Sh.50/= kwa kila lita ya mafuta yanayoingia nchini, hiyo ndiyo itakuwa ukombozi wetu. Naomba Waheshimiwa Wabunge wote safari hii tuifanyie marekebisho sheria na tuombe hiyo Sh.50/=, ndiyo mahali ambapo tumeona kuna mafanikio kwa ile Sh.50/= tuliyoiweka mara ya kwanza na REA imefanikiwa kutokana na hiyo.