Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia katika hii Wizara yetu muhimu ya Fedha. Nianze kwa kuipongeza Wizara, Waziri mwenyewe, Naibu Waziri, lakini pamoja na Wataalam wote, wanafanya kazi vizuri sana. Pia napenda niipongeze Serikali kwa ujumla kwa niaba ya wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ambalo ndiyo Jimbo la Mbeya Vijijini, kwa kweli utekelezaji wa bajeti iliyopita ilikuwa nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya pamoja na kutengewa bilioni moja na nusu kwa ajili hospitali ya Wilaya lakini tuna vituo vya afya vitatu vinavyoendelea na tuko kwenye hatua ya umaliziaji sasa hili. Kuna Kituo cha Afya cha Ilembo, Santilia pamoja na Ikukwa. Tuko vizuri na tunaendelea vizuri tunategemea nafikiri kama kwa kazi hii Serikali itaendelea kutupa pesa zaidi kwa ajili ya kumalizia zaidi ya vituo 50 vya zahanati zetu ambazo ziko katika hatua nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye barabara nako Serikali kwa kweli imefanya vizuri kwenye Halmashauri yangu. Kuna barabara nyingi ambazo zimejengwa pamoja na jiografia yetu ambayo ina changamoto nyingi, lakini tunaishukuru Serikali kwa sababu mpaka sasa hivi kuna utekelezaji wa barabara za lami za kilomita 27 ambazo zimetoka kwenye barabara tulikuwa na barabara zenye kilomita mbili tu, sasa kuongezewa mpaka 27 kwa kweli inabidi tuishukuru Serikali. Pamoja na hiyo tuna kilomita kama 47 ambazo ni za barabara ya mchepuko. Tunaiomba sasa Serikali ikamilishe hizo barabara kwa haraka mno kwa sababu zinapita maeneo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye umeme Serikali imefanya vizuri kwenye Halmashauri yangu, kwenye elimu nayo tunashukuru sana tumepewa pesa kwa ajili ya miundombinu ya shule za msingi na shule za sekondari naishukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye maji napenda nimshukuru kwa kipekee Waziri wa Maji amefanya kazi kubwa sana. Tulikuwa na changamoto za utekelezaji lakini mpaka sasa hivi kuna miradi mingi ya maji ambayo inaendelea. Kwenye Mji Mdogo wa Mbalizi sasa hivi tumeunganishwa na Jiji, kwa hiyo tuna uhakika wa kupata maji namwomba Waziri ahakikishe kuwa asije akatuangusha. Sasa hivi tunaenda kiangazi tuhakikishe maji yanamwagika Mbalizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kwenye mradi wa Mbawi Jojo, mradi wa Haporoto Itimu, Haporoto Idimi, Izumbwe Iwindi, Horongo Itimu Mwampalala, Shongo, Igale, Swaya na Rupeta pamoja na Mshewe Muvwa, Njelenje Mapogoro na Mjele. Hii ni miradi muhimu namwomba sana Mheshimiwa Waziri aikamilishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye bajeti ya mwaka huu, wenzangu wameongelea sana kipaumbele ukiangalia namba moja ni kilimo. Ukiangalia Serikali imetenga kiasi gani kwenye kilimo huwezi kuziona. Nilikuwa najaribu kuangalia bajeti ya Kenya kwa sababu katika vitu vingine hivi lazima tujilinganishe linganishe. Wenzetu wa Kenya wamefanya nini? Wana vipaumbele vinne katika kipaumbele kimojawapo ni hifadhi ya chakula hawajaita kilimo. Wametenga nini kwenye hifadhi ya chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia dash board ya bajeti ya Kenya. Kwenye kilimo hifadhi ya chakula (food reserve) wametenga bilioni 32; kwenye nafaka wametenga bilioni 43; kwenye nafaka tena wametenga bilioni 20; kwenye umwagiliaji wametenga bilioni 192; na kwenye subsidy ya mbolea wametenga bilioni 97. Kwa jumla kwenye kilimo wametenga bilioni 409. Sasa hizo ukiangalia kwenye bajeti ya Waziri huwezi kuziona mara moja zimefichwa wapi. Tungeomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ili wananchi wajue ni namna gani wakulima tunawajali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kinaenda pamoja na miundombinu. Tuna tatizo sana la usafirishaji wa mbolea.

Leo hii kupeleka mbolea Mbeya kwa tani ni Sh.90,000 mpaka Sh.120,000. TAZARA quotation yao ni laki moja na ishirini kwa tani, lakini barabara ni elfu tisini kwa tani. Sasa unajaribu kuangalia kwa nini kuna tatizo hili. Ukija kwenye Reli ya Kati mpaka Tabora ni elfu sabini lakini kwa barabara ni zaidi ya laki moja na ishirini. Ningeomba sana Serikali ingechukua jukumu ni namna gani tuiboreshe TAZARA ili tuweze kuwakomboa wakulima. Tukipunguza bei ya mbolea tutakuwa tunamsaidia mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nafikiri limeongelewa kwa kiasi kikubwa na wenzangu waliotangulia ni suala la hii akaunti ya Treasury Single Account. Ningependa kupendekeza kwa Serikali ingeangalia kwa uangalifu sana, hizi hatua inazozichukua wakati mwingine zinaweza kutupeleka mahali pabaya. Kwa sababu ukichukua pesa zote za Halmashauri benki ambazo zimefungua matawi zitabakiwa na nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iangalie NMB, CRDB, na NBC, pesa nyingi ambazo wanazo kwenye Halmashauri zetu kule, kwenye Wilaya zetu ni pesa za Serikali. Ukizikusanya zote hizi unazipeleka Benki Kuu na Benki Kuu ni kwa ajili shughuli za benki siyo retail banking. Shughuli za Benki Kuu ni Benki kwa Serikali na Benki wa Mabenki, hata wenzetu waliochukua hatua za kufungua hii Treasury Single Account hawakwenda kwenye Halmashauri, kwa sababu imegundulika kuwa katika hizo nchi kulikuwa na abuse kubwa sana, kulikuwa na ubadhirifu mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia na madhumuni ya hii Tresuary Single Account ni kwa ajili ya ukwasi liquidity, cash management siyo kwa ajili ya financial control, kwa sababu huwezi ukahamisha responsibility za Maafisa Masuuli kuzipeleka kwa Waziri wa Fedha. Hii Wizara watashindwa kui-manage. Waziri ali-make reference nyingi tu, ningependa vilevile aende kumsoma mtu mmoja anaitwa … (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.