Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia. Nawashukuruni sana. Waheshimiwa Wabunge wote kwa pande zote mbili kimsingi ni kama wameunga mkono hoja yangu na hoja ya Wabunge wa Mkoa wa Dodoma ya kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuamua Dodoma kuwa jiji. Kimsingi ni kama wamepongeza na wameunga mkono hoja hii nawashukuruni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tulileta hoja hii? Tulileta hoja hii ya kuomba azimio hili lipitishwe na Bunge kwa sababu ni utaratibu wa kawaida wa mabunge duniani. Pale ambapo Serikali imefanya jambo zuri, ni jambo zuri la kidiplomasia pia kuungwa mkono na Bunge lake ili kuonesha kwamba Bunge na Serikali viko pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uamuzi wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi ulifanywa mwaka 1973, ni miaka 44 mpaka 2017. Rais huyu wa Awamu ya Tano baada ya kupita Marais wengi, yeye ameamua kwa vitendo kwamba tunahamia Dodoma, Serikali inahamia Dodoma mambo ambayo tayari yameshafanyika. Kwa hiyo, tunapotaka kupongeza ni kwa sababu sisi Wabunge wa Dodoma tunaona faida inayopatikana na ninyi wenzetu Wabunge mnaona yanayoendelea kwamba Dodoma inashamiri na inaenda kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoona matembe yaliyokuwa karibu na mji yanaondoka, tunapoona watu wanazidi kujenga nyumba bora, tunapoona miundombinu mbalimbali inazidi kuimarishwa, tunapoona idadi ya watu inaongezeka, tunapoona Wabunge badala ya weekend kuondoka kwenda Dar es Salaam mnabaki Dodoma, sisi mlitaka tufanye nini badala ya kuomba tupitishie Azimio hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tumeomba Azimio hili lipitishwe na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuunge mkono, kwa sababu Rais huyu amefanya jambo kubwa na sisi Wabunge wa Dodoma tunataka Watanzania wafahamu kwamba Wabunge wa Dodoma tumefurahishwa na jambo hili na tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Afrika ijue kwamba Wabunge wa Dodoma na wananchi wa Dodoma tumefurahishwa na jambo hili, tunataka dunia ijue kwamba Wabunge wa Dodoma na Watanzania kwa ujumla tumefurahishwa na jambo hili na ndiyo maana tunaleta azimio hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam ilipotangazwa kuwa jiji ilikuwa haijakidhi vigezo na ile siku ya Uhuru ikatangazwa Dar es Salaam kuwa Jiji. Ilikuwa haina hata vigezo hata kimoja. Tuna Jiji la Mbeya, Jiji la Tanga, Jiji la Arusha na Jiji la Mwanza. Ni vigezo vipi vilivyokamilishwa ilhali ikiwa Dodoma iwe nongwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakata niseme tu Waheshimiwa Wabunge, mimi nimewaomba na Wabunge wa Dodoma tunawaomba wenzetu Wabunge muunge mkono azimio hili kumpongeza Mheshimiwa Rais na yale yote mliyoyasema Waheshimiwa Wabunge na kwenye maazimio
tumesema; kwenye Azimio namba mbili tumeiomba Serikali kuongeza rasilimali fedha kwa ajili ya ujenzi miundombinu mbalimbali ili kukidhi vigezo hivyo ambavyo vina upungufu. Kwa sababu hakuna kitu ambacho kimekamilika hata katika miji mingine ambayo imetangazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa Dodoma kwa sababu ya hadhi yake ya Makao Makuu ambayo hakuna anayebisha hata mmoja, basi hivi vyote tunaamini vitakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, nasi wananchi wa Dodoma na kwa niaba ya wenzangu Wabunge wa Dodoma, hususan Mheshimiwa Spika ambaye ameruhusu Azimio liweze kusomwa, tunasema hivi, zawadi yetu kwa Mheshimiwa Rais Magufuli itakuwa ni kubwa mwaka 2020, ndiyo ahadi tunayoitoa kwake. Tunamshukuru kwa haya makubwa anayoifanyia Dodoma, tunamshukuru kwa kututoa gizani na sasa ametuweka kwenye mwanga. Ninawaomba kwa sababu na nyie Waheshimiwa Wabunge wote ni sehemu ya maendeleo ya Dodoma, mtuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja tena.