Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia azimio hili na nianze kwa kueleza masikitiko yangu kuhusiana na azimio hili kwa sababu kwa maoni yangu ni azimio ambalo kwa kweli ni lenye ubaguzi kwenye nyanja nyingi. Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema ni azimio lenye ubaguzi kwa sababu kwanza ukiangalia hili azimio, linataka kufanya historia kama inaanza leo kwamba Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ndio ambaye amefanya hili Jiji la Dodoma au huu Mji wa Dodoma kuwa ndiyo Makao Makuu na kuwezekana kuwa Jiji. Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato wa kuifanya Dodoma ikawa kama ilivyo leo na Mheshimiwa Simbachawene amerejea hapa kwamba wakati Mheshimiwa Rais anazungumza kwenye Mkutano wenu Mkuu, alizungumza kwamba vipo vitu ambavyo vimeshawezesha sasa Dodoma kuwa ni mahali panaweza kuwa Makao Makuu. Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo azimio hili lingekuwa na maana sana na ningeliunga mkono kama lingetambua vilevile watu wengine ambao wamefanya mambo makubwa mpaka tukawa jinsi tulivyo leo. Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu wamejenga hili Bunge, wako watu waliojenga barabara za kuja Dodoma, wako watu waliojenga Chuo Kikuu cha Dodoma. Hivi leo Rais Dkt. Magufuli amefanya nini ambacho ni muujiza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais, Mheshimiwa Magufuli ametangaza, tena ametangaza bila kuzingatia sheria. Amepoka mamlaka ambayo sio yake.

Siyo, nenda karejee Sheria ya Mipango Miji kifungu cha 7(2) uone nani mwenye mamlaka ya kutangaza Mji kuwa Jiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunataka kuonesha Bunge hili kufanya kwamba fedha anazotumia Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli ni za kwake za mfukoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili ni lazima lijirudishe mahali pake liwe na hadhi na kwamba ndilo linaloombwa pesa. Serikali inapaswa kuja hapa kuomba pesa na siyo sisi Wabunge kuwa ni chombo cha kushangilia na kupongeza wajibu wa mtu anaopaswa kufanya. Hilo ndilo sikitiko langu la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikitiko la pili ni aina ya ubaguzi unofanywa katika kutekeleza mambo mbalimbali katika nchi. Sisi Moshi tulifanya michakato yote ya kuwa jiji kwa zaidi ya miaka mitano na tumetumia fedha nyingi za ndani na za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba Mheshimiwa Rais siku moja kabla ya Mei Mosi ya mwaka 2017 alikuja akakaa mahali na watu ambao sisi watu wa Moshi hatuwajui, akaamua kufuta mchakato mzima wa Moshi kuwa Jiji. Sasa hili sijambo la kushangilia. Ni jambo la kusikitisha. (Makofi)

Mhesimiwa Mwenyekiti, la mwisho, mpango huu ni mpango wa kukurupuka. Ni mpango ambao unasababisha mateso makubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nieleze kwa masikitiko makubwa kwamba mwezi uliopita tumepoteza watumishi watatu wa TIC wakiwa wanakuja Dodoma.