Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, naomba nichangie kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na uwezo wa kuchangia leo.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nashukuru na kupongeza jinsi Wizara inavyojipanga kwa kuleta mabadiliko katika mfumo wa kukusanya mapato na kusimamia matumizi. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watalaam wa Wizara hii kwa kazi nzuri sana wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya maeneo naomba nishauri ili kuboresha utendaji kazi na kuleta ufanisi zaidi katika Wizara ya Fedha na taasisi zilizoko chini yake. Pakiwa na ufanisi katika Wizara hii ya Fedha, basi ufanisi katika Wizara zote utapatikana.

Mheshimiwa Spika, kwanza naishauri Serikali ikae pamoja na kufanya pendekezo la kubadilisha mfumo wetu wa bajeti pamoja na budget cycle. Nashauri tungepanga bajeti yetu ya matumizi baada ya kufanya makusanyo. Leo hii tunapanga matumizi ndipo tunatafuta hayo mapato. Tusipofikia malengo ya kukusanya kwa ajili ya matumizi tuliyopanga inaonekana tumefanya vibaya.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali iangalie namna ya kuibadilisha budget cycle. Leo hii baada ya bajeti mbalimbali kuandaliwa na kuletwa Bungeni, muda wa kufanya mabadiliko makubwa hayapo, kama kuna upungufu hakuna namna ya kuboresha.

Mheshimiwa Spika, hata Bungeni, Kamati ya Bajeti ingekaa kuanzia mwezi wa tisa hadi kumi na mbili (Septemba hadi Desemba) ili kuishauri Serikali pamoja na kupata maoni ya Serikali kabla ya kufanya maamuzi. Hii italeta utulivu (harmony) kwa sekta binafsi na wawekezaji wataweza kujua sera ya kikodi, tozo na ada mbalimbali na kujipanga kabla badala ya kapata taarifa za kushtukiza.

Mheshimiwa Spika, pia nashauri kutokana na malalamiko mengi yanayotokea kutokana na urasimu unaojitokeza katika suala la uhakiki, ningependa Serikali iangalie namna ya kuunganisha mifumo ya utoaji wa taarifa baina ya Wizara ya Fedha na Wizara zote hasa katika maeneo ya mapato na matumizi ili madai yanapokuwa yanatolewa (lodged) katika hatua ya kwanza kupitia Wizara yoyote au taasisi, Wizara ya Fedha iweze kuiona na waanze kuifanyia kazi mapema. Ikifika hatua ya Wizara ya Fedha kupitia Hazina kufanya maamuzi, watakuwa wana taarifa zote na pia watakuwa wameomba ufafanuzi mapema. Mifumo iwe integrated, hii ni pamoja na Ofisi ya AG.

Mheshimiwa Spika, pia nashauri mifumo hii iwe na design mapema ili ziendane na wakati na pia ziweze kuwa na uwezo wa kuingiliana (design, integrated systems). Naomba pia nishauri tuwekeze zaidi kwenye utafiti na maendeleo (research and development). Utafiti utasaidia kujua mwenendo wa biashara na uzalishaji, kujua gharama za uzalishaji ili kuweza kupanga mipango na sera bora ya fedha na kodi.

Mheshimiwa Spika, nashauri tuwekeze zaidi kwenye elimu ya kodi na mifumo yake. Tuboreshe Chuo chetu cha Kodi na kuwekeza zaidi kwenye elimu ya uhasibu, haki za walipa kodi, haki ya kujua nini ni sahihi na nini siyo sahihi. Leo hii wahasibu, mawakala wa kutoa mizigo katika bandari na mipakani (accountants and clearing agents) wakifanya makosa, adhabu inakuwa ya mteja na mara nyingi maafisa wachache wa TRA wanashirikiana na hawa wahasibu na wakala wa kutoa mizigo kwa maslahi binafsi kuwaumiza wateja wao.

Mheshimiwa Spika, pia nishauri task force ya kodi ifanye kazi yake mwaka mzima, wawe na ofisi ya kudumu na wakutane na wadau wa Kamati ya Bajeti. Hii itafanya waweze kujua kila sekta kwa undani. Pia muda wa kutosha kufanya utafiti iwe full- fledged office. Pia task force hii iwe na wajumbe zaidi wa sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, muhimu kuliko yote ni elimu kuanzia ngazi ya msingi juu ya ulipaji wa kodi, faida zake na elimu juu ya matumizi yake.

Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja.