Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kupata nafasi nichangie Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote ningependa kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri ambayo inafanya kupitia Wizara ya Fedha, lakini kwa namna ya kipekee nimshukuru Mheshimiwa Waziri Dkt. Philip Mpango pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi nzuri ambayo wanawafanyia Watanzania. Pia nitoe shukrani kwa viongozi wengine wa Wizara, Katibu Mkuu, Dotto James, Naibu Makatibu Wakuu, Dkt. Kazungu, Bi. Amina Shabani na Bi. Susan Mkapa kwa kazi nzuri wanayotufanyia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha ni Wizara muhimu sana. Ni Wizara muhimu kwaasbabu kila mtu anaangalia fedha, kila mtu anataka fedha kwa hiyo, ni vigumu sana kwa watu wengi kuona mazuri yanayofanyika. Lakini mazuri yapo na mazuri haya utayaona kama utaamua kuangalia takwimu za utendaji wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka uliopita Wizara hii ilipanga kukusanya kama Wizara shilingi bilioni 522 lakini ikakusanya shilingi bilioni 655, utendaji wa asilimia 126, takwimu zinaongea na kama kila Wizara ingeweza kufanya performance ya asilimia 126 tungekuwa pazuri zaidi. Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri kazi yenu tunaiona, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ina jukumu moja kubwa muhimu la kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi unakua, uchumi unaongezeka na hilo likifanikiwa ndipo faida ya kukua kwa uchumi itakwenda kwa kila mtu. Kwenye hilo Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri mmefanya kazi nzuri, uchumi wetu unakuwa kwa asilimia 7.1 mwaka uliopita kutoka asilimia 7.0 mwaka uliotangulia. Kwa hiyo, kama nilivyosema takwimu zinaongea, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia mmefanyakazi nzuri katika kudhibiti mfumuko wa bei. Tutaongea mengi, tutawapiga mawe, tutawatukana, lakini takwimu hiyo inawabeba kwamba mmefanya kazi nzuri. Mfumuko wa bei umeshuka kutoka 5.3 mwaka 2017 kufikia 3.8 mwezi Aprili, 2018. Hii ni kazi nzuri mnayoifanya ninyi mkiongozwa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu niongee suala la umaskini. Wizara hii inahusishwa sana na suala la umasikini wa wananchi. Watu wengi wamesema sana kuhusiana na suala la umasikini lakini umaskini ni suala la kitaalam.

Mheshimiwa Spika wenzetu wachumi mimi siyo mchumi, lakini wenzetu wachumi wameweka vigezo na viashiria vya kupima umaskini siyo suala tu kwamba mimi sina hela mfukoni hapa nikajiita maskini siyo sahihi, kuna viashiria vya kitaalam. (Makofi)

(i) Kuna kiashiria cha umri wa kuishi; wastani wa umri wa kuishi kwa Mtanzania umeongezeka, hicho ni kipimo cha umaskini. Unavyoongeza wastani wa kuishi wa Mtanzania maana yake maisha yake yameboreka, maana yake umaskini umepungua. (Makofi)

(ii) Kingine ni vifo vya watoto chini ya umri wa miaka mitano, kwenye kigezo hicho pia Wizara hii imefanya vizuri katika kuondoa umaskini, lakini muhimu zaidi ni upatikanaji wa huduma za kijamii. Hiki ni kipimo kikubwa sana cha umasikini katika nchi husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaongelea huduma ya afya, huduma ya elimu, huduma ya miundombinu mbalimbali. Na tunajua huduma ya afya imeboreka sana na inaedelea kuboreka, tunajua elimu sasa ni elimu bure. Sisi tunafurahia elimu bure lakini ni Wizara yako ambayo inatoa fedha kwa ajili ya elimu bure hii. Hiki ni kipimo ambacho lazima tukiangalie kwenye kupima umaskini. Tunaongelea miundombinu Waheshimiwa Wabunge hapa ni mashahidi kila mtu anapata barabara ya lami katika Jimbo lake, kuna ujenzi wa reli ya standard gauge unajengwa. Hivi ndivyo vipimo vya umasikini ambavyo inabidi tuvitumie na kwenye hilo Wizara hii imefanyakazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu niongelee kuhusu suala muhimu sana, suala hili ni la ulipaji kodi, sisi Watanzania tunakuwa na tabia ya kuchangua mifano kutoka kwenye nchi zilizoendelea ambayo inatunufaisha katika hoja ambayo tunaitaka kwa wakati ule. Moja ya kitu ambacho tunapenda kuiga sana sisi Watanzania ni demokrasia ya nchi za Magharibi. lakini niwaombe Waheshimiwa Wabunge na wannachi wa Tanzania, tuige kitu kimoja, ulipaji kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tofauti kubwa ya nchi zilizoendelea na nchi maskini na nchi maskini ni katika ulipaji kodi. Endapo tunaiga hilo na tukakubali kwamba sasa ni wakati wa kulipa kodi kwa hiari ndipo tutaweza kujenga uchumi wa nchi yetu. Chanzo kikubwa cha mapato ya Serikali yoyote duniani ni ulipaji kodi na usipolipa kodi sheria za kodi ni kali sana. Tunaongelea hapa rufaa zilizopo kwenye Baraza la Kodi, lakini kwa wenzetu kesi kama za kodi hata hazichukui muda zinakwisha haraka, aliyekwepa kodi atafilisiwa na anachukuliwa hatua kali za kisheria. Kwa hiyo, niwaombe Watanzania tuige ulipaji wa kodi wa nchi zilizoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kuna suala la elimu ya kodi. Watu hawawezi tu kuibuka kulipa kodi pasipokupewa elimu ya kodi. Katika mitaala yetu ya elimu kuanzia shule za msingi, sekondari mpaka chuo kikuu tuhakikishe somo la kodi liwe somo la lazima. Usitake mtu mzima umwambie leo alipe kodi wakati kuanzia shule ya msingi hujamfundisha kodi ni nini kwahiyo ni vizuri elimu ya kodi iweze kuchukua nafasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, binafsi kupitia Tamasha la Maji Maji Selebuka ambalo naliandaa mimi, tunafanya mdahalo wa shule za sekondari kuhusiana na elimu ya kodi kila mwaka kwa kushirikiana na TRA. Niwapongeze watu wa TRA kwa kushirikiana na mimi katika kutoa elimu ya kodi kwa wanafunzi wa shule za sekondari wa Mkoa mzima wa Ruvuma. Ni vizuri juhudi hizi sasa zikasambazwa na kuenezwa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la michezo ya kubahatisha (gaming activities). Wengi wameliongelea hili na madhara yake kwa vijana lakini naomba niliongelee kama chanzo cha mapato ambacho kinaweza kikatusaidia sana kuendeleza michezo. Huku nyuma, fedha zilizokuwa zinatokana na gaming activities ilikuwa ni chanzo cha mapato kwa ajili ya timu zetu za Taifa.

Mheshimiwa Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja.